TAARIFA YA MWAKA YA SHUGHULI ZA KAMATI KWA KIPINDI CHA JANUARI, 2022 HADI JANUARI, 2023

1  SEHEMU YA KWANZA 1.0 UTANGULIZI 1.1 Maelezo ya Jumla Mheshimiwa Spika, Kwa niaba ya Kamati ya Kudumu ya Bunge 2 1.2 Muundo wa Taarifa Mheshimiwa Spika, kanuni ya 142 ya kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Juni, 2020, imeweka masharti kuhusu Muundo wa Taarifa ya Kamati. Kwa kuzingatia masharti hayo, naomba kutambulisha muundo wa Taarifa kwa kutaja sehemu kuu kama ifuatavyo: - (i) Sehemu ya kwanza ni utangulizi inaotoa maelezo ya jumla, ikiwemo msingi wa shughuli za Kamati, njia na mbinu zilizotumika pamoja na orodha ya shughuli zilizotekelezwa; (ii) Sehemu ya pili inafafanua shughuli zilizotekelezwa na uchambuzi kwa yaliyojitokeza wakati wa utekelezaji. Aidha, sehemu hii inabainisha mafanikio na changamoto zilizojitokeza; (iii) Sehemu ya tatu inatoa maoni ya jumla na mapendekezo ili kuliwezesha Bunge kuamua; na (iv) Sehemu ya nne inahitimisha na kutoa hoja kwa hatua ya Bunge lako tukufu kujadili na kufanya uamuzi. 1.3 Msingi wa Shughuli zilizotekelezwa na Kamati Mheshimiwa Spika, Msingi wa shughuli zilizotekelezwa na Kamati kwa kipindi cha mwaka mmoja unatokana na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Kanuni za Bunge Toleo la Juni, 2020. Katiba ambayo ni mwongozo mkuu wa uendeshaji wa Nchi, imebainisha lengo kuu la Serikali na kuonesha madaraka na jukumu la Bunge. Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Juni, 2020, zimeweka utaratibu wa utekelezaji bora wa madaraka ya Bunge unaowezesha kufuatilia shughuli za umma ili kufanikisha lengo kuu la Serikali. 3 Mheshimiwa Spika, Ibara ya 8 (1) (b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inatambulisha lengo kuu la Serikali la kuwezesha ustawi wa wananchi. Aidha, Ibara ya 96 ya Katiba inalipa Bunge uwezo wa kuunda Kamati za namna mbalimbali kwa ajili ya utekelezaji bora wa madaraka yake. Vilevile, Ibara ya 63(2) ya Katiba imeipa madaraka ya kuisimamia na kuishauri Serikali kwa niaba ya wananchi. Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 6(8) cha Nyongeza ya nane ya Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Juni, 2020, Jukumu la Kamati ya Miundombinu ni kuisimamia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi pamoja na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 7 (1) cha Nyongeza ya Nane ya Kanuni za Bunge, kimebainisha majukumu ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kama ifuatavyo: - (i) Kushughulikia bajeti za Wizara inazozisimamia; (ii) Kushughulikia miswada ya sheria na mikataba inayopendekezwa kuridhiwa na Bunge iliyo chini ya Wizara inazozisimamia; (iii) Kushughulikia Taarifa za utendaji za kila mwaka za Wizara inazozisimamia; na (iv) Kufuatilia utekelezaji unaofanywa na Wizara hizo. Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo, katika kipindi cha Januari 2022 hadi Februari, 2023, Kamati ilitekeleza shughuli zifuatazo: - 4 (i) Kujadili taarifa za utekelezaji wa bajeti za Wizara na utendaji wa taasisI inazozisimamia kwa kipindi cha nusu mwaka (Julai – Desemba, 2022) kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa Bajeti; (ii) Kutembelea na Kukagua miradi ya maendeleo chini ya Wizara inazozisimamia iliyotengewa fedha kwa mwaka wa fedha 2021/2022; na (iii) Kuchambua taarifa za utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2021/2022 na makadirio ya bajeti ya mwaka 2022/2023 za Wizara inazozisimamia. 1.4 Njia iliyotumika Mheshimiwa Spika, Kanuni ya 142 ya Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Juni, 2020, imeweka masharti yanayotaka taarifa ya Kamati inayoingia Bungeni ibainishe njia au mbinu iliyotumia. Kwa msingi huo, naomba kulijulisha Bunge kuwa Kamati ilitumia njia na mbinu zifuatazo: - (i) Kujadili masuala ya sekta na kuibua ajenda za kuweka kwenye ratiba ili kuwasilisha kwa Spika kwa ajili ya kuidhinishwa; (ii) Kufanya uchambuzi wa taarifa zilizowasilishwa na kutathimini mambo yaliyoripotiwa kwa kuoanisha na mtazamo wa wananchi kuhusu ustawi wao; (iii) Kudadavua maudhui ya taarifa zote zilizowasilishwa ili kupata utoshelevu wa maudhui kwa kulinganisha na mahitaji ya uelewa wa Kamati kuhusu jambo linahusika; (iv) Kutembelea baadhi ya maeneo na kuona hali halisi kwa lengo la kulinganisha yaliyoripotiwa na hali halisi uwandani; na 5 (v) Kujumuisha mambo yanayobainika kwenye vikao wakati wa majadiliano na mahojiano ili kuorodhesha mambo makuu ya kutolewa maoni na ushauri. Mheshimiwa Spika, naomba kulihakikishia Bunge lako tukufu kuwa njia na mbinu hizo ziliisaidia Kamati kupata matokeo yanayoripotiwa katika taarifa hii. Aidha, uthabiti wa maudhui ya taarifa hii umetokana na njia na mbinu hizo. Naliomba Bunge lako tukufu liipokee na kuijadili taarifa hii kwa kuzingatia ufanisi wa njia na mbinu zilizotumika. 6 SEHEMU YA PILI 2.0 SHUGHULI ZILIZOTEKELEZWA NA UCHAMBUZI WA MATOKEO 2.1 Ufafanuzi wa Jumla Mheshimiwa Spika, katika kufuatilia sekta hizo Kamati ilitekeleza shughuli zifuatazo: - 2.1.1 Ufuatiliaji wa Maazimio ya Bunge katika taarifa ya Mwaka 2021/ 2022 i) Sekta ya Uchukuzi a. Mamlaka ya Bandari Tanzania Mifumo ya TEHAMA inayotumiwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania iboreshwe ili kuimarisha ulinzi wa mizigo pamoja na miundombinu ya Bandari. b. Vyuo vilivyo chini ya Sekta ya uchukuzi Serikali iviwezeshe kifedha vyuo hivyo, pamoja na kuimarisha miundombinu yake kwa kutumia mpango kabambe wa kuendeleza vyuo. c. Ujenzi wa Reli ya kisasa Serikali ione umuhimu wa kipande cha Reli cha Tabora – Kigoma katika kukuza uchumi wa Taifa letu. d. Ujenzi Reli uzingatie hali ya jiografia ya maeneo Ujenzi wa Reli nchini unapofanyika, tahadhari kubwa ichukuliwe ili kuepusha uharibifu wa mazingira na miundombinu ya reli. 7 e. Ununuzi wa vichwa na mabehewa ya Treni Upungufu wa vichwa 45 vya treni pamoja na mabehewa imekuwa ni changamoto inayoathiri ufanisi na mchango wa sekta kwenye maendeleo ya ustawi wa uchumi wetu. Mheshimiwa Spika, Utekelezaji wa Mapendekezo Sekta ya Uchukuzi ni kama ifuatavyo: - a) Katika sekta hii kuna baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na Bunge yamefanyiwa kazi kwa asilimia ndogo na mengine yanaendelea kutekelezwa, Hivyo basi, hakuna mapendekezo yaliyotekezwa kwa asilimia mia moja. b) Mapendekezo ya Bunge yanayoendelea kufanyiwa kazi ni kama yafuatayo: - (i) Uboreshaji wa Mifumo ya TEHAMA inayotumiwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania Mheshimiwa Spika, Awamu ya kwanza ya mfumo huo umekamilika. Mawakala wa forodha wapatao 877 wamesajiliwa na wanatumia mfumo. Aidha, Uboreshwaji na mafunzo ya mfumo huo kwa awamu ya kwanza, upande wa Zanzibar umeanza na unategemea kukamilika mwishoni mwa mwezi Machi 2023. Mfumo wa pamoja wa Kieletroniki wa uondoshwaji wa shehena Bandarini (Tanzania Electronic Single Window System - TeSWs) unategemewa kukamilika mwezi Juni, 2023. 8 (ii) Kuwezeshwa kifedha na kuimarisha miundombinu ya Vyuo vilivyo chini ya Sekta ya Uchukuzi Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuongeza fedha kwa vyuo vya DMI na NIT kama ifuatavyo: -  Kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Chuo cha DMI kilitengewa Shilingi bilioni 2.48 ikilinganishwa na mwaka 2022/2023 ambapo Chuo hicho kimetengewa Shilingi bilioni 3.90 sawa na ongezeko la asilimia 57. Aidha, Serikali kupitia Mamlaka ya Bandari (TPA) itanunua kifaa cha kufundishia manahodha na wahandisi wa Meli (simulator), tayari Shilingi bilioni 3.6 zimetengwa katika mwaka huu wa fedha kwa ajili hiyo.  Chuo cha NIT kilitengewa jumla ya Shilingi bilioni 35.66 katika mwaka 2021/2022 ikilinganishwa na Shilingi bilioni 39.05 katika mwaka 2022/2023, sawa na ongezeko la asilimia 9.5. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Chuo cha NIT kilitengewa bajeti ya jumla Shilingi bilioni 9.53 kwa ajili ya ununuzi wa Ndege mbili (2) za injini moja (1) za kufundishia marubani. (iii)Ujenzi wa Reli ya Kisasa kipande cha Tabora - Kigoma kipewe kipaumbele Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TRC imesaini mkataba na Kampuni ya CCECC na CRCC kutoka China mnamo tarehe 20 Desemba, 2022 kwa ajili ya Ujenzi wa Reli ya Kisasa ya SGR kwa Kipande cha Tabora – 9 Kigoma (Km 506). Mkataba huo utatekelezwa kwa muda wa miezi 42. (iv)Ujenzi wa Reli uzingatie hali ya jiografia ya maeneo Mheshimiwa Spika, Serikali imeeleza kuwa itaendelea kufanya upembuzi yakinifu kabla ya kuanza kutekeleza miradi yote mikubwa ikiwa ni pamoja na miradi ya SGR, uboreshaji wa Bandari na ujenzi wa Meli. (v)Ununuzi wa vichwa na mabehewa ya Treni Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa vitendea kazi vya Miter Gauge Railway (MGR) Ununuzi wa Mabehewa 22 wenye mkataba wa dola 14,964,852.34, manunuzi ya vipuri vya ukarabati wa mabehewa 600 ya mizigo yenye thamani ya shilingi 2,135,620,191.97 na mabehewa 37 ya abiria kwa Dola za Marekani 3,655,099.76. Hadi kufikia Januari, 2023, Serikali imepata mkopo kutoka Exim Bank ya Korea wenye jumla ya Dola za Marekani milioni 346.73 kwa ajili ya ununuzi wa vitendea kazi (vichwa vya treni na mabehewa). Mheshimiwa Spika, katika sekta hii ya ujenzi Kamati imeridhika na kasi ya utekelezaji wa Mapendekezo yaliyotolewa na Bunge kwani kamati ilifuatilia na kubaini hakuna mapendekezo ambayo hayajafanyiwa kazi kabisa. 10 ii) Sekta ya Ujenzi a. Ujenzi wa viwanja vya ndege Serikali ione umuhimu wa kuiachia Mamlaka ya Viwanja wa Ndege Tanzania (TAA) kazi ya Ujenzi na Usimamizi wa Viwanja vya Ndege. b. Ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya mabasi yaendayo haraka Dar es Salaam (BRT) Serikali ione namna ya kutatua changamoto ya mradi huu ili ulete matokeo yaliyokusudiwa. c. Vyuo vilivyopo Sekta ya Ujenzi Serikali iandae mikakati ya kuboresha miundombinu, vifaa vya kufundishia na mazingira ya kujifunza katika vyuo hivyo na kuviongezea bajeti. d. Nyumba za Magomeni Kota TBA waongezewe fedha za kwa ajili ya kuendeleza uwekezaji kwenye eneo lililo wazi la Magomeni kota. Mheshimiwa Spika, Utekelezaji wa Mapendekezo katika sekta ya ujenzi ni kama ifuatavyo: - a) Kamati imebaini kuwa yapo mapendekezo ya Bunge yaliyofanyiwa kazi na mengine yapo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji. Hivyo hakuna mapendekezo yaliyofanyiwa kazi kikamilifu; b) Mapendekezo ya Bunge yanayoendelea kufanyiwa kazi ni kama ifuatavyo: - 11 (i) Kuhusu Ujenzi wa viwanja vya ndege kuachiwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi iliunda Timu ya Wataalam kutoka Wizara mbalimbali kwa ajili ya kupitia na kubaini iwapo kama kuna muingiliano wa majukumu kati ya TAA na TANROADS ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Katibu Mkuu Kiongozi yaliyotokana na taarifa ya CAG. Timu ilikamilisha na ilitoa ushauri kuwa, kuna haja ya majukumu ya ujenzi wa viwanja vya ndege kurudishwa TAA kutoka TANROADS. (ii) Kuhusu ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya mabasi yaendayo haraka Dar es Salaam (BRT) ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa Mheshimiwa Spika, TANROADS inaendelea kushirikiana na wadau wengine zikiwepo taasisi za Serikali kama DART ili kufanya pembuzi yakinifu zinazozingatia mazingira halisi na hatimaye utekelezaji wa miradi yenye manufaa. (iii) Kuhusu Vyuo vilivyopo Sekta ya Ujenzi Mheshimiwa Spika, Bajeti ya mwaka 2022/2023 imeongezeka kwa asilimia 10 ambapo ukarabati na ujenzi wa majengo mapya umetengewa jumla ya Shilingi bilioni 6. Usanifu kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Taasisi ya Ujenzi (ICoT) Morogoro pamoja na tawi la Mbeya umekamilika. Ukarabati wa majengo katika kampasi ya 12 Mbeya, unatekelezwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA). Ujenzi umefikia asilimia 47.5. (iv) Nyumba za Magomeni Kota Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa jambo hili bado unaendelea kwani Serikali imeendelea na mchakato wa kurekebisha kanuni zinazoendesha TBA ili kuruhusu uwekezaji shirikishi. c) Mheshimiwa Spika, katika sekta hii ya Ujenzi, Kamati imeridhika na kasi ya utekelezaji wa Mapendekezo yaliyotolewa na Bunge kwani kamati ilifuatilia na kubaini kuwa, hakuna mapendekezo ambayo hayajafanyiwa kazi kabisa. Kamati inatoa pongezi kwa Serikali kwa kuona umuhimu wa kutatua changamoto. iii) Sekta ya Mawasiliano a. Uhalifu wa kimtandao TCRA ishirikiane na Jeshi la Polisi kukabiliana na tatizo hilo. b. Kupungua kwa miamala ya simu Serikali iisimamie TCRA kukutana na wadau na watoa huduma ili kutatua changamoto hizo. c. Udhibiti hafifu wa huduma za usafirishaji wa mizigo, vipeto na vifurushi nchini Serikali ije na Kanuni zitakazosimamia kumbukumbu za kielektroniki za usafirishaji wa mizigo, vifurushi na vipeto; na kuisimamia TCRA ambaye ni mtoa leseni ili kuondoa tatizo hilo. 13 d. Changamoto za shughuli za Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) Serikali itenge fedha zaidi kadiri inavyowezekana kwa ajili ya Mfuko huu (UCSAF); pamoja na kuisimamia Kampuni ya Mawasiliano Tanzania (TTCL) kukamilisha miradi ya ujenzi wa minara. e. Madeni makubwa kwa Shirika la Posta Tanzania (TPC) Serikali ilisaidie Shirika la Posta liweze kulipwa madeni yake mapema; na isimamie na kuitaka TCRA kulilipa fedha Shirika hilo ikiwa ni kamisheni kutokana na mapato wanayopata ya ada ya leseni ya wasafirishaji wa mizigo. f. Changamoto ya madeni ya TTCL na uendeshaji wa Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa Serikali isimamie Kampuni ya Mawasiliano ya Simu (TTCL) ili iweze kulipwa madeni yake, kukamilisha Kanuni za uendeshaji wa Mkongo wa Taifa, kutoa fedha kwa TTCL na kufanya marekebisho ya sheria ya manunuzi ili kuruhusu TTCL iweze kununua vifaa vilivyotumika kutoka makampuni mengine. a) Mheshimiwa Spika, mapendekezo yaliyotolewa na Bunge yanaendelea na utekelezaji, hivyo basi, hakuna mapendekezo yaliyotekezwa kikamilifu; na b) Mheshimiwa Spika, Mapendekezo ya Bunge yanayoendelea kufanyiwa kazi ni kama ifuatavyo: - 14 (i) Kuhusu Uhalifu wa kimtandao Mheshimiwa Spika, Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na uhalifu wa kimtandao na inaendelea kuchukua hatua. (a) Serikali imeanzisha timu maalum inayojumuisha wataalam kutoka vyombo vya Ulinzi na Usalama, Ofisi ya Mwendesha Mashtaka - DPP na TCRA; (b) Serikali inahamasisha zoezi la uhakiki wa laini za simu (namba) na kuwa laini zote ambazo hazitahakikiwa mpaka ifikapo tarehe 13 Februari, 2023 zitafungiwa; (c) Kesi 42 zipo katika upelelezi, ambapo kesi 6 upelelezi umekamilika (zinaenda mahakamani hivi karibuni) na kesi 36 upelelezi unaendelea. TCRA pia ilichukua hatua za kukabiliana na uhalifu wa kimtandao kwa kusimamisha usajili kwa mawakalahuru kwenye maeneo yanayoripotiwa kuwa na idadi kubwa ya matukio ya wizi wa kimtandao. (ii) Kupungua kwa miamala ya simu Mheshimiwa Spika, TCRA imeendelea kufuatilia kwa ukaribu mienendo ya miamala ya fedha inayopita katika mitandao ya simu. Kwa kipindi cha Julai hadi Disemba 2022, idadi ya miamala ya fedha ilipanda kutoka 349,952,830 kwa mwezi Julai, 2022 hadi kufikia miamala 410,741,783,982 kwa mwezi Disemba, 2022. Pia idadi ya watumiaji wa Mobile Money iliongezeka toka 15 38,407,233 mwezi Julai mpaka 40,953,496 kwa mwezi Disemba. (iii) Udhibiti hafifu wa huduma za usafirishaji wa mizigo, vipeto na vifurushi nchini; Mheshimiwa Spika, Hatua zimechukuliwa kwa kuanza kupitia Kanuni za Usafirishaji wa Mizigo, Vifurushi na Vipeto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuongeza umadhubuti wa mfumo wa udhibiti. Aidha, usajili wa watoa huduma hizo unaendelea ukiwa na lengo la kupata taarifa za watoa huduma wote katika Sekta ya Posta. (iv) Madeni makubwa kwa Shirika la Posta Tanzania Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na Shirika la Posta imewasilisha Wizara ya Fedha na Mipango andiko la kuomba kufutiwa deni la muda mrefu la kodi kiasi cha Shilingi Billioni 26.8 Hii itakuwa njia ya kuisaidia Posta katika kukusanya madeni, Wizara kwa kushirikiana na Shirika la Posta imeandika barua kwenda taasisi za umma zenye madeni kuwataka kulipa madeni hayo. (v) Changamoto za shughuli za Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote - UCSAF Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga jumla ya Dola za Marekani milioni 30 kupitia fedha za mradi wa Tanzania ya Kidigitali ambazo ni mkopo kutoka Benki ya 16 Dunia ili kutekeleza miradi ya kufikisha huduma za mawasiliano vijijini. Fedha hizo zitawezesha ujenzi wa minara mipya takribani 380 na kuongeza nguvu ya minara 488. (vi) Changamoto ya madeni ya TTCL na uendeshaji wa Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa Mheshimiwa Spika, Wizara imewasilisha madeni hayo Wizara ya Fedha na Mipango kwa ajili ya kufanyiwa uhakiki na mara utakapomilika malipo yatafanyika. Wizara imekamilisha taratibu za kukabidhi majukumu ya usimamizi, uendeshaji na uendelezaji wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwa TTCL na taratibu za kuwasilisha Waraka wa Baraza la Mawaziri kuwezesha TTCL kumiliki Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano zinaendelea. c) Mheshimiwa Spika, Kamati ilielezwa kuwa hakuna Mapendekezo ya Bunge ambayo hayajatekelezwa kabisa. Kamati inaendelea kusisitiza kuwa mapendekezo ya Bunge yafanyiwe kazi kikamilifu ili kupunguza changamoto zilizopo. 2.1.2 Uchambuzi wa Bajeti za Wizara na Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo Mheshimiwa Spika, Kamati ilibaini mambo yafuatayo katika Sekta ya ujenzi: - 17 (i) Kulijitokeza suala la fedha zinazotolewa kulipa madeni ya miradi ya nyuma badala ya utekelezaji wa miradi mipya. Kamati ilishauri kwamba katika maombi ya fedha, Serikali itofautishe fedha itakayotumika kulipa madeni na ya utekelezaji wa miradi mipya; na (ii)Changamoto ya kuwa na miradi mingi kuliko uhalisia wa fedha. Kamati inaona ni vyema Serikali ikaweka mkakati wa kutekeleza miradi michache kwa ufanisi kuliko miradi mingi isiyotekelezeka Pamoja na kuwa ilitengewa bajeti. 2.1.3 Ziara za ufuatiliaji wa Miradi ya Maendeleo Mheshimiwa Spika, tarehe 13 – 20 Machi, 2021, Kamati ilizingatia masharti ya Kanuni ya 117 (1) ya Kanuni za Bunge na kutembelea miradi inayotekelezwa na Wizara zilizo chini yake. Kamati ilitembelea mikoa mitatu ambayo ni Simiyu, Mwanza na Kagera na kukagua miradi ya Ujenzi wa Reli ya Kisasa – kipande cha Isaka - Mwanza (Lot 1V), Ujenzi na ukarabati wa Meli kwenye Maziwa Makuu, Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, Ujenzi na ukarabati wa Vivuko, Maegesho na Utekelezaji wa mradi wa Postikodi na Anwani za Makazi, Ujenzi wa Miundombinu ya Viwanja vya Ndege, Ununuzi wa Rada, vifaa na ujenzi wa miundombinu ya hali ya hewa na Mradi wa Ujenzi wa barabara na Madaraja. Mheshimiwa Spika, Katika ziara hiyo, Kamati ilibaini mafanikio na changamoto ambazo ziliwasilishwa kwenye taarifa yake. Ni rai ya kamati kuwa zitapatiwa ufumbuzi wa haraka. 18 2.1.4 Uchambuzi wa Taarifa za Utendaji Mheshimiwa Spika, naomba kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa utaratibu wa kupokea na kujadili taarifa za kutoka Serikalini unaiwezesha Kamati kulisaidia Bunge kutekeleza majukumu yake ya kuisimamia Serikali kwa mujibu wa Ibara ya 63 (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 2.1.5 Uchambuzi wa Mswada na Maazimio Mheshimiwa Spika, Kamati ilipata fursa ya kuwasilisha taarifa yake bungeni kuhusu Muswada wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi ambao ulipitishwa na Bunge na kusainiwa kuwa sheria rasmi na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 27 Novemba, 2022. 2.2 Uchambuzi wa Matokeo Mheshimiwa Spika, Kamati ilitoa taarifa ya ziara kwa miradi mbalimbali iliyokagua na kutembelea kupitia taarifa ya Kamati inayohusu utekelezaji wa bajeti ya Wizara hizo kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023. Mheshimiwa Spika, Aidha, ziara hizo zilifanyika kwa Lengo la kuhakiki shughuli za umma zilizotekelezwa katika sekta zinazosimamiwa na Kamati kwa kuzingatia matarajio ya wananchi. 2.2.1 Mafanikio na Changamoto Mheshimiwa Spika, naomba kulijulisha Bunge, matokeo ya uhakiki yanayoonesha mafanikio na changamoto kwa kila sekta kama ifuatavyo: - 19 a. Sekta ya Uchukuzi Mheshimiwa Spika, Kamati ilihakiki mchango wa sekta hii na kubaini mafanikio mbalimbali katika sekta hii. Serikali itaendelea kuimarisha na kuboresha miundombinu na huduma za reli, bandari, viwanja vya ndege, kununua ndege, meli za abiria na mizigo na kuboresha utabiri wa hali ya hewa nchini, Kama ilivyoeleza katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025, Ibara 59 (a) – (j). Mheshimiwa Spika, Katika Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 imeeleza kuwa Serikali kupitia Wizara mbalimbali imeweka mkakati mpya uitwao “Tekeleza sasa kwa matokeo makubwa”. Serikali imeeleza nia ya kuimarisha miundombinu ya usafiri hususan uboreshaji wa bandari ya Dar es Salaam pamoja na reli ya kati. Mheshimiwa Spika, Kamati ilibaini changamoto mbalimbali katika sekta ya usafiri na usafirishaji majini na usafiri wa Reli, mfano kuna uhaba wa wataalam wenye ujuzi na uzoefu, kuchelewa kulipwa fedha za ujenzi wa miradi hali inayozorotesha maendeleo ya sekta, uchumi wa nchi na wananchi. Mheshimiwa Spika, Kamati inatoa msisitizo kuwa changamoto hizo zifanyiwe kazi kikamilifu kwa ustawi wa wananchi. b. Sekta ya Ujenzi Mheshimiwa Spika, Kuna miradi mbalimbali ambayo Kamati ilipata nafasi ya kuitembelea katika kipindi cha mwezi Julai, 2022 – Mpaka Januari 2023 kama ifuatavyo: - 20 (i) Mradi wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha zege wa Itoni-Ludewa-Manda - Lusitu-Mawengi (Km 50.0) Mheshimiwa Spika, katika ziara hiyo, Kamati ilijulishwa mafanikio mbalimbali ya mradi huo kama ifuatavyo: - a) Ushirikishwaji wa wazawa katika mradi kwani umeajiri wafanyakazi 690 ambapo wazawa 650 sawa na asilimia 94; b) Mkandarasi ameleta wataalam mahiri na wenye uzoefu; na c) Mkandarasi ameongeza muda wa kufanya kazi hadi usiku na ameandaa mpango kazi mpya unaolenga kumaliza kazi kwa wakati; Mheshimiwa Spika, Kamati ilijulishwa changamoto zinazoukabili mradi huo kuwa ni pamoja na: - a) Fedha kutotolewa kwa wakati hali inayosababisha Kuongezeka kwa gharama za mradi kutokana na kuongezwa kwa muda kutoka miezi 28 - hadi miezi 69; b) Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Mawengi ambao ardhi yao imetwaliwa ili kupisha ujenzi wa mradi bado hawajalipwa fidia; c) Mvua nyingi zimeathiri utekelezaji wa mradi pia kuna uhalibifu wa mazingira kwenye chanzo cha maji kutokana na ukataji wa mlima; d) Maporomoko ya udongo kwenye maeneo yenye kina kirefu cha kuchimba kwa ajili ya kupitisha barabara; na e) Uhaba wa malighafi mfano saruji kutoka kwenye viwanda vya TWIGA na DANGOTE. 21 Mheshimiwa Spika, Serikali iimarishe usafiri wa maji katika Ziwa Nyasa ili kusafirisha madini yanayochimbwa Mkoani Njombe na kusaidia wananchi wanaoishi pembezoni mwa ziwa kunufaika na fursa za kiuchumi. (ii) Ujenzi wa nyumba 3500 za watumishi wa umma katika eneo la Nzuguni – Jijini Dodoma Mheshimiwa Spika, mradi huo ukikamilika utakuwa na manufaa mbalimbali kama ifuatavyo: - a) Mradi umewezesha wataalam wa ndani ya Wakala wa Majengo kujipatia uzoefu zaidi kwenye ubunifu na usanifu wa majengo; b) Wakazi wa Dodoma zaidi ya 100 wamenufaika na ajira rasmi na zisizo rasmi kama mafundi ujenzi, vibarua na mama lishe; c) Mradi umenufaisha viwanda kwani vifaa vyote vya ujenzi vinavyotumiwa kwenye mradi vinatoka kwenye viwanda hivyo; d) Awamu ya kwanza ya mradi una thamani ya shilingi bilioni 14, fedha hizo zimetolewa zote kwa asilimia 100; e) Utekelezaji wa mradi huu umepunguza uhalifu katika eneo la Nzuguni kwani kabla ya mradi eneo hilo lilikuwa maficho ya wahalifu; f) Mradi utapunguza changamoto ya uhaba wa nyumba kwa watumishi wa umma waliopo Dodoma; na g) Mradi utaongeza mapato ya Serikali. Mheshimiwa Spika, changamoto zinazoukabili mradi huu kuwa ni pamoja na: - 22 a) Ukosefu wa barabara ya kufika eneo la mradi na uhaba mkubwa wa maji; b) Kupanda kwa gharama vifaa vya ujenzi hali inayopelekea kuongezeka kwa gharama za utekelezaji wa mradi; na c) TBA wanadai fedha nyingi kutoka kwa wapangaji pamoja na kutolipwa fedha za ujenzi wa miradi mbalimbali ya Serikali. Mheshimiwa Spika, chimbuko la mradi huo ni utekelezaji wa maamuzi ya Serikali ya kuhamishia Makao Makuu Jijini Dodoma na hivyo kuongezeka kwa mahitaji ya nyumba za makazi kwa watumishi wa Umma. c. Sekta ya Mawasiliano Mheshimiwa Spika, Kamati imebaini mafanikio mbalimbali yaliyopatikana katika sekta hii, mfano kuandaliwa kwa mkakati wa miaka mitano (2021-2025) wa kuharakisha utekelezaji na matumizi ya Mfumo wa Anwani za makazi na postikodi, kuongeza kwa pato la Taifa na kuongeza matumizi ya TEHAMA nchini. Mheshimiwa Spika, Changamoto katika sekta hii zinaweza kusababisha malengo yaliyoelezwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025 yasitimie endapo kama hazitapatiwa ufumbuzi wa haraka. Kuchelewa kukamilika kwa mikataba na taratibu za manunuzi ya vifaa kwa ajili ya miradi mbalimbali, baadhi ya wakandarasi kutokuwa na uwezo wa kutekeleza miradi kwa kiwango kinachotakiwa, na miradi kutokamilika kwa wakati ni moja ya vikwazo vinavyoikabili Sekta hii. 23 Mheshimiwa Spika, Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025 ibara ya 61 (a) –(o) inaeleza kuwa Sekta hii imejikita zaidi katika kuimarisha ubora wa mawasiliano nchini na kuhakikisha wigo wa mawasiliano unaongezeka na kuwafikia wananchi wote. Aidha, Dira ya maendeleo ya Taifa 2020, imeeleza kuwa ukuzaji wa Teknolojia ya upashanaji Habari na Mawasiliano ni muhimu katika kuleta mageuzi ya kijamii na kiuchumi. 2.3 Majumuisho ya Sehemu ya Pili Mheshimiwa Spika, uimarishaji wa miundombinu katika sekta ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ni uwekezaji muhimu hivyo basi, Serikali inatakiwa kuwa mstari wa mbele katika suala hili ili kujenga mtandao mzuri utaowezesha kuleta maendeleo mijini na vijijini katika kuimarisha ustawi wa wananchi na kuweka mazingira ya kukua kwa uchumi na maisha bora kwa kila Mtanzania kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 -2025 na Dira ya maendeleo ya Taifa 2025 inavyoeleza. Mheshimiwa Spika, Kamati inatoa rai kuwa changamoto zilizopo katika sekta hizo zikapatiwa ufumbuzi wa haraka ili kufikia malengo. 24 SEHEMU YA TATU 3.0 MAONI NA MAPENDEKEZO 3.1 Maoni ya jumla Mheshimiwa Spika, Wananchi wanayo matumaini makubwa yanayopaswa kutimizwa katika sekta zinazosimamiwa na Kamati hii kwani bado juhudi za Serikali zinahitajika katika kuboresha na kutatua changamoto. Kamati inatoa maoni yafuatayo: - 1. Upungufu wa watumishi na vitendea kazi imekuwa ni changamoto kubwa kwa baadhi ya taasisi na hivyo kuathiri utendaji kazi wa Taasisi hizo. Ni maoni ya Kamati kuwa Serikali iajiri watumishi wa kutosha; 2. Yafanyike marekebisho ya sheria ya Reli kuruhusu sekta binafsi kuwekeza katika kutoa huduma za reli; 3. Ucheleweshwaji wa malipo ya kodi ya pango kwa nyumba za TBA ambako kunasababisha Wakala kushindwa kutimiza malengo yake kutafutiwe ufumbuzi wa haraka; 4. Serikali iongeze bajeti ili kukabiliana na Ufinyu wa bajeti kwa taasisi zilizo katika Wizara kunakopelekea kukwamisha utekelezaji wa majukumu na miradi mbalimbali mfano TANROADS na Roadfund; 5. Kutokuwa na kanuni za uendeshaji kwa TBA, ni jambo linalopelekea TBA kushindwa kuendesha miradi kwa kushirikisha sekta binafsi, ni maoni ya kamati kuwa Serikali irekebishe kanuni hizo; 25 6. Serikali isimamie utekelezaji wa ulipwaji wa fidia kwa Wananchi waliopisha utekelezaji na miradi ya maendeleo; 7. Kuchelewa kutekeleza kwa baadhi ya miradi au kasi ndogo ya utekelezaji kunachangia miradi mingi kutokamilka kwa wakati. Mathalani, ujenzi wa minara, mradi wa reli ya kisasa kipande cha Dar es Salaam – Morogoro hali hii inakwamisha kufikia lengo lililokusudiwa. Ni maoni ya Kamati kuwa Serikali iwasimamie Wakandarasi ili wamalize miradi katika muda unaopangwa; 8. Serikali iendelee kusimamia ukamilishwaji wa mikataba na taratibu za manunuzi ya vifaa ili miradi iweze kutekelezwa kwa wakati; 9. Serikali isimamie Wakandarasi wanaotekeleza miradi Miradi chini ya kiwango; 10. Serikali iwasimamie Wasafirishaji binafsi wa mizigo na vifurushi ili waweze kutoa kamisheni au wawe Mawakala wa Posta; na 11. Ajira za TBC zitoe fursa kwa watu wenye vipaji kuliko kuangalia sifa za vyeti. 26 3.2 Mapendekezo Mheshimiwa Spika, Napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Sekta za Ujenzi, Uchukuzi, Habari na Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari. Taarifa hii imeeleza shughuli zilizotekelezwa na Kamati pamoja na kubainisha mafanikio na changamoto kama ilivyobainika wakati wa utekelezaji wa shughuli za Kamati, Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge katika Taarifa ya Mwaka 2021/ 2022. Aidha, Taarifa imeonesha jinsi Katiba, Dira ya Taifa 2025, na Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025 vinavyoelekeza kuhusu Sekta zinazosimamiwa na Kamati hii. Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo zipo changamoto zilizobainika na ambazo utatuzi wake utasaidia kuwezesha huduma bora, kukua kwa uchumi, maisha bora ya wananchi na maendeleo ya Taifa letu. Kwa sababu hiyo, naomba kutoa mapendekezo ya utatuzi wa changamoto kwa kila sekta kama ifuatavyo: - 3.2.1 Sekta ya Uchukuzi a) Uhaba wa Watumishi na Vitendea Kazi KWA KUWA, Uhaba wa watumishi na vitendea kazi katika sekta za usafiri wa anga, reli, hali ya hewa na usafiri kwa njia ya maji hali inayosababisha maendeleo ya sekta hii yasifikie malengo yaliyokusudiwa, NA KWA KUWA, changamoto hizo zinasababisha sekta ya uchukuzi kutotoa mchango unaokusudiwa kwa pato la Taifa. 27 KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali iajiri watumishi wa kutosha na wenye uzoefu, ili kukidhi mahitaji yaliyopo. b) Marekebisho ya sheria ya Reli ili kuruhusu uwekezaji KWA KUWA, umuhimu wa sekta ya reli kufanya marekebisho ya sheria ni mkubwa ili kuruhusu sekta binafsi kuwekeza katika kutoa huduma za reli nchini; NA KWA KUWA, changamoto hiyo inasababisha wawekezaji kutoka sekta binafsi kushindwa kuwekeza katika reli hivyo kuchelewesha na kurudisha nyuma ukuaji wa uchumi wa nchi, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali iharakishe mchakato wa marekebisho ya sheria ya Reli iliiweze kuruhusu sekta binafsi kufanya uwekezaji. 3.2.2 Sekta ya Ujenzi a) Changamoto ya Wapangaji wa nyumba za TBA kutolipa kodi kwa wakati KWA KUWA, imeonekana kuna changamoto ya ulipaji wa kodi kwa wapangaji wa TBA na kusababisha shirika kupata hasara na kushindwa kutekeleza miradi mingine; NA KWA KUWA, changamoto hiyo inasababisha TBA kushindwa kukusanya fedha ili iweze kujiendesha kibiashara, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba; TBA ifuatilie wadaiwa sugu, iwachukulie hatua za kisheria bila kumuonea mtu aibu, aidha ipeleke taarifa ya wadaiwa kwa msajili wa Hazina. 28 b) TBA Kuchelewa kulipwa fedha za ujenzi wa miradi kwa wakati KWA KUWA, kuna changamoto ya TBA kuchelewa kulipwa fedha za ujenzi wa miradi kwa wakati hali inayosababisha miradi kutofikia malengo; NA KWA KUWA, changamoto hizo zinaweza kuchelewesha miradi kutokamilika kwa wakati kama ilivyokusudiwa, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba; Serikali itoe fedha kwa TBA ili waweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. c) Changamoto ya Kanuni zinazoendesha TBA kutoruhusu uwekezaji mkubwa KWA KUWA imeonekana kuna mapungufu kwa TBA kutokuwa na kanuni zinazoruhusu kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi yake kunakosababisha ishindwe kufikia malengo yake; NA KWA KUWA, kutorekebisha kanuni hizo kunakosesha wakala kufanya uwekezaji mkubwa; KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba; TBA ifanye mchakato wa kurekebisha Kanuni zake kwa haraka ili iweze kushirikiana na Sekta binafsi katika kutekeleza miradi. d) Changamoto ya kuchelewa kulipwa fidia Ujenzi wa barabara ya Itoni – Ludewa - Manda - Lusitu-Mawengi KWA KUWA, kuna changamoto ya kuchelewa kulipwa fidia kwa wananchi wanaopitiwa na mradi, kunasababisha mradi huo kutofikia malengo kama yalivyoainishwa katika Ilani ya Chama cha 29 Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025 Ibara ya 55 (c) (I), NA KWA KUWA, changamoto hizo zinaweza kuchelewesha mradi na kuongeza gharama jambo ambalo linaongeza mzigo wa madeni kwa Serikali, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba; (i) Serikali iwalipe fidia Wananchi wa kijiji cha Mawengi ambao ardhi yao imetwaliwa kwa ajili ya kutekeleza mradi; na (ii) Serikali iongeze fedha kwa TANROADS ili iweze kutekeleza miradi hii ambayo ni muhimu katika ukuaji wa uchumi wa nchi na ustawi wa wananchi. e) Miradi kutokamilika kwa wakati KWA KUWA, Miradi kutokamilika kwa wakati kunakosababishwa na kutotolewa fedha kwa wakati hivyo, kupelekea ongezeko la gharama, NA KWA KUWA, changamoto hiyo inapelekea sekta ya ujenzi kutotoa mchango unaokusudiwa kwa pato la nchi na wananchi kwa wake, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali ilipe Wakandarasi kwa wakati ili waweze kukamilisha miradi ndani ya muda uliowekwa na kuepuka kupanda kwa gharama za ujenzi pamoja na riba. f) Kuongezeka kwa gharama za miradi KWA KUWA, kuna changamoto ya kuongezeka kwa gharama za miradi kunakosababishwa na kuongezeka kwa bei za vifaa 30 wakati wa utekelezaji kusababisha kupanda kwa gharama za mradi na kunarudisha nyuma maendeleo katika miradi; NA KWA KUWA, changamoto hiyo inapelekea kupanda kwa gharama za mradi na kutokamilika kwa wakati, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali isimamie mikataba ya TANROADS wanayoingia ili kusiwe na mabadiliko ya gharama wakati wa kutekeleza miradi. 3.2.3 Sekta ya Mawasiliano a) Kuchelewa kukamilika kwa mikataba na taratibu za manunuzi KWA KUWA, kuchelewa kukamilika kwa mikataba na taratibu za manunuzi ya vifaa kwa ajili ya miradi mbalimbali, kunasababisha sekta kutofikia malengo stahiki, NA KWA KUWA, Changamoto hizo zinaweza kuchelewesha miradi katika sekta hii kutokukamilika kwa wakati na kuongezeka kwa gharama za miradi jambo ambalo linaongeza mzigo wa madeni kwa Serikali, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali ikamilishe kwa wakati mikataba na taratibu za manunuzi ya vifaa kwa ajili ya miradi mbalimbali. b) Changamoto ya Miradi kutekelezwa chini ya kiwango KWA KUWA, kuna baadhi ya Wakandarasi kutokuwa na uwezo wa kutekeleza miradi kwa kiwango kinachotakiwa katika ujenzi wa minara na miradi mingine kunapelekea serikali kupata hasara; 31 NA KWA KUWA, Changamoto hiyo inaweza kusababisha miradi katika sekta hii kutokukamilika kwa wakati na kuongezeka kwa gharama za miradi jambo ambalo linaongeza mzigo wa madeni kwa Serikali, KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali isimamie kwa ukaribu Wakandarasi ambao hawana uwezo wa kutekeleza miradi kwa kiwango kinachotakiwa. c) Upotevu wa Mapato ya Serikali unaotokana na Shirika la Posta KWA KUWA, Serikali kupitia shirika la POSTA inakosa mapato yanayotokana na usafirishaji wa mizigo, vipeto na vifurushi vinavyosafirishwa na Makampuni binafsi ya usafirishaji; NA KWA KUWA, makampuni hayo hayatoi Kamisheni yeyote kwa Serikali, hali inayosababisha Serikali kukosa mapato; KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali iandae mkakati wa kupata kamisheni kutoka kwa wasafirishaji binafsi au kuwatumia makampuni binafsi kama Mawakala wa kusafirisha mizigo. d) TBC iajiri Wasanii wenye Vipaji KWA KUWA, TBC kuna watangazaji au wasanii wenye vipaji vizuri lakini hawana sifa za kupata ajira kwa mujibu wa taratibu za Serikali, na hali hiyo inasababisha shirika linashindwa kufanya ushindani na makampuni binafsi ya utangazaji ambayo yanazingatia vipaji; NA KWA KUWA, changamoto hiyo inasababisha kupunguza mvuto kwa wananchi ambao huvutiwa na vipaji hivyo, 32 KWA HIYO BASI, Bunge linashauri kwamba, Serikali iruhusu shirika la Utangazaji Tanzania - TBC kutoa ajira kwa watu wenye vipaji kulingana na matakwa ya soko. 3.3 Majumuisho Sehemu ya Tatu Mheshimiwa Spika, katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025 Ibara ya 55 (a) - (c) inaelezea kwamba” Serikali kuendeleza shughuli za ujenzi wa Miundombinu mbalimbali ili kuifanya sekta ya ujenzi ifikie malengo yake ya kuwezesha wananchi kuendelea na uzalishaji kwa ajili ya kuongeza kipato”. Kwa Sekta ya uchukuzi, Kamati inaendelea kusisitiza kuwa maboresho yaendelee kufanyika katika eneo la bandari, reli, viwanja vya ndege na meli vinahitajika ili kuweza kuboresha usafirishaji wa mizigo, bidhaa na abiria. Mheshimiwa Spika, Katika Sekta ya Mawasiliano kamati inatoa maoni kuwa, Serikali iendelee na maboresho ili kuwezesha huduma za mawasiliano kupatikana kwa asilimia 94 ifikapo 2025 kama inavyoelezwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020-2025 Ibara ya 60 (d). 33 SEHEMU YA NNE 4.0 HITIMISHO NA HOJA 4.1 Maelezo ya Kuhitimisha Mheshimiwa Spika, naomba kuhitimisha Taarifa hii kwa kuthamini utaratibu uliowekwa na Bunge wa kuzitaka Kamati za Kudumu za Bunge kuripoti shughuli zake kwa kipindi cha mwaka. Utaratibu huu unaliweka Bunge katika nafasi ya kutambua hali ilivyo katika sekta mbalimbali. Kwa kuwa Taarifa hizo zinatolewa katika Mkutano wa Mwisho kabla ya mkutano wa bajeti, ushauri wa Bunge kwa serikali unaweza kufanyiwa kazi kwa mwaka wa fedha unaofuata. Mheshimiwa Spika, kwa maelezo hayo, napenda kukushukuru tena kwa kunipa nafasi hii adhimu ili niweze kuwasilisha Taarifa hii mbele ya Bunge lako Tukufu. Naamini maelezo na ufafanuzi nilioutoa, utaliwezesha Bunge kujadili inavyostahili na kutoa ushauri kwa Serikali ili kuboresha shughuli na kuongeza tija katika sekta zinazosimamiwa na Kamati hii. Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, naomba kumshukuru kwa dhati Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa (Mb), Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi akishirikiana na Manaibu Mawaziri Mhe. Eng. Msongwe Geofrey Kasekenya (Mb) (Ujenzi), na Mhe. Atupele Fredy Mwakibete (Mb) (Uchukuzi) kwa ushirikiano mzuri wanaoutoa kwa Kamati. Vile vile, namshukuru Mhe. Nape Moses Nnauye (Mb) Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Eng. Kundo Andrea 34 Mathew (Mb), Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kuipa Kamati ushirikiano stahiki. Mheshimiwa Spika, nawashukuru pia Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kuwawezesha Mawaziri na Naibu Mawaziri kutoa ushirikiano kwa Kamati. Mwisho lakini si kwa umuhimu, namshukuru Ndg. Athumani Hussein Mkurugenzi wa Idara ya Kamati, Ndg. Gerald Magili, Mkurugenzi Msaidizi na Makatibu wa Kamati Ndg. Janeth Malangu na Ndg. Victory Mrema, pamoja na Ndg. Grace Samweli, Msaidizi wa Kamati kwa Shughuli za uratibu na kufanikisha kazi za Kamati kama ilivyostahili. Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nawashukuru Wajumbe wa Kamati hii kwa kujituma wakilenga kutoa ushauri unaofaa kwa Bunge. Kufanya hivyo kutaiwezesha Serikali kuboresha maeneo mbalimbali na kuendelea kukidhi matarajio ya wananchi kwa Serikali yao. Kwa kutambua mchango wao, naomba kuwataja kwa majina kama ifuatavyo: - 35 1. Mhe. Moshi Seleman Kakoso, Mb - Mwenyekiti 2. Mhe. Anne Kilango Malecela, Mb - Makamu Mwenyekiti 3. Mhe. Zuberi Mohamed Kuchauka, Mb - Mjumbe 4. Mhe. Abbas Ali Hassan Mwinyi, Mb - “ 5. Mhe. Miraji Jumanne Mtaturu, Mb - “ 6. Mhe. Sofia Hebron Mwakagenda, Mb - “ 7. Mhe. Ahmed Mabkhut Shabiby, Mb - “ 8. Mhe. Aeshi Khalfan Hilaly, Mb - “ 9. Mhe. Abdulazizi Mohamed Abood Mb - “ 10. Mhe. Eng.Mwanaisha N. Ulenge, Mb - “ 11. Mhe. Mohamed Maulid Ali, Mb - “ 12. Mhe. Innocent Edward Kalogeris, Mb - “ 13. Mhe. Mbarouk Juma Khatibu, Mb - “ 14. Mhe. Amina Ally Mzee, Mb - “ 15. Mhe. Rose Vicent Busiga, Mb - “ 16. Mhe. Ally Anyigulile Jumbe Mlaghila, Mb - “ 17. Mhe. Fredric Edward Lowassa, Mb - “ 18. Mhe. Stella Simon Fiyao, Mb - “ 19. Mhe. Innocent Sebba Bilakwate, Mb - “ 20. Mhe. Ghati Zephania Chomete, Mb - “ 21. Mhe. Ahmed Yahya Abdulwakil, Mb - “ 22. Mhe. Bahati Khamis Kombo, Mb - “ 23. Mhe. Angelina Adam Malembeka, Mb - “ 24. Mhe. Ahmed Ally Salum, Mb - “ 4.2 Hoja Mheshimiwa Spika, baada yakusema hayo, naliomba Bunge lako tukufu lipokee na kuijadili Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati 36 ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kwa kipindi cha Januari, 2022 hadi Februari, 2023, ili hatimaye kupitisha mapendekezo ya Kamati yawe ushauri wa Bunge kwa Serikali. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. Moshi Selemani Kakoso, Mb MWENYEKITI KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU 31 Januari, 2023

 

Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.