MIGUNA MIGUNA NA SAKATA NA SERIKALI YA KENYA



 Dk. Miguna pichani   asimulia alivyojikuta Dubai
DUBAI, UAE
MWANASHERIA na mwanaharakati wa upinzani wa Kenya, Miguna Miguna, ambaye kwa sasa amelazwa katika Hospitali ya Dubai amesimulia namma alivyojikuta nchini hapa.
Dk. Miguna pia ameitaka jumuiya ya kimataifa kuingilia arudi Kenya kwa vile anateseka.
 “Niliamka nikiwa hapa Dubai na bila kitu. Nahitaji jumuiya ya kimataifa na kila mtu kuingilia kati suala hili,” Dk.  Miguna alisikika akimwagiza mmoja wa wanasheria wake kwa simu kuvijuza vyombo vya habari vya kimataifa.
Mwanasheria huyo alisisitiza atapanda tu ndege itakayoelekea Nairobi, si vinginevyo.
“Sitarajii kukubali kupanda chochote, kwa sababu ni kinyume na matakwa yangu. Mimi ni mgonjwa na siwezi hata kutembea, walichukua miwani yangu na walichukua kila kitu,” alisema akiwa hospitali.
Akisimulia jinsi alivyoamka asubuhi na kushangaa kujikuta akiwa Dubai, Muungano wa Falme za Kiarabu (UAE), Dk. Miguna alisema:
“Mimi ni abiria niliye katika eneo la kusubiria kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dubai, UAE.
Nimepitia vipimo vya msingi, ambavyo vimethibitisha nililazimishwa kwa nguvu kupanda ndege chapa EK722 ya Shirika la Ndege la Emirates kutoka Nairobi kuja Dubai, ambayo iliwasili asubuhi hii ya leo (jana).
Karibu wahuni 50 wenye silaha wakiongozwa na askari polisi aliyevalia kiraia wa Kisomali, ambaye aliwaongoza Jumatano kuvunja kwa nguvu katika choo nilichokuwa nimeshikiliwa kinyume na sheria kwenye Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyatta.
Bila kujitambulisha, waliniangusha chini kwa nguvu, walinishikilia na kukaa juu yangu wakati kundi la wahuni wengine wanne tofauti waliponichoma sindano yenye vimiminika visivyofahamika katika nyayo zote mbili, mikono na pande zote za mbavu na mwili mzima ukapoteza mawasiliano.
Leo, saa 11:25 asubuhi (jana), baada ya Emirates kutua na abiria kushushwa, nilipata fahamu na kumwuliza mtu aliyeketi kando yangu, ambaye pia alionekana kuwa mmoja wa maofisa walionisindikiza, “tuko wapi?” nilimuuliza, akanijibu kwamba tulikuwa Dubai.
Mara wanaume watatu waliovalia jaketi za njano sare za Air Emirates walichomoza na kunifuata na kwa sauti ya jeuri walinitaka nishuke kutoka kwenye ndege.
Yule anayechukiza zaidi alijitambulisha mwenyewe kama “Njihia”, alidai kwamba lile fungu la karatasi aliloshikilia mkononi zilikuwa ‘nyaraka’ zangu.
Nilimwambia sitoambatana naye kwenda popote; kwamba sina hati yangu halali ya kusafiria ya Kenya na yeye ni mhalifu tu aliyeniteka, aliyenilevya na kuniondoa kwa nguvu kutoka Kenya kinyume na matakwa yangu na kukiuka amri mbalimbali za mahakama.
Niliwaambia wafanyakazi wa Air Emirates kuwa kumsafirisha mtu asiye na fahamu na aliyechomwa sindano za kumlevya kama mimi kutoka Kenya hadi Dubai bila kuwapo nyaraka zozote za kuhalalisha hilo ni kosa la jinai.
Pamoja na jaribio lao la kutaka kunilazimisha kwenda kituo cha polisi na Idara ya Uhamiaji Dubai, nilikataa na kushinikiza nionane na daktari.
Baada ya mvutano mrefu, nilipewa ruhusa ya kuonana na daktari ambaye amenifanyia vipimo vya msingi na kuthibitisha simulizi yangu hii.
Vipimo zaidi hasa vya sumu vinahitaji niondoke uwanja wa ndege, kitu ambacho naweza tu kukifanya nikiwa na hati yangu halali ya kusafiria ya Kenya, nyaraka ambayo wahuni wameninyang’anya isivyo halali na kuiharibu wakikiuka agizo la Jaji Kimaru.
Nina maumivu makali kushoto mwa kifua changu, mkono wa kushoto, kiwiko cha kulia na mguuni.
Naamini hawa wahuni wamenichoma sindano na vimiminika vya sumu.
Lakini pia, nimeweka wazi kwa mamlaka za Uhamiaji za Muungano wa Falme za Kiarabu kwamba siwezi na kamwe sitaenda popote isipokuwa tu Kenya.
Nimegoma kuondoka eneo la kimataifa la uwanja wa ndege.
Lazima nirudi Kenya kama raia wa Kenya, uraia wa kuzaliwa kama ilivyoelezwa na amri mbalimbali za mahakama.
Mheshimiwa Jaji Odunga alitoa amri Machi 28 (juzi) zikiwatia hatiani ya kutenda kosa Matiang’I, Kihalangwa na Boinett kwa kosa la jinai la kuidharau amri halali na kuwataka wajitokeze kwa hukumu jana saa nne kamili asubuhi.
Jaji Odunga pia aliagiza niachiliwe mara moja bila masharti yoyote na nihudhurie mahakamani leo saa nne kamili (jana).
Hata hivyo, si Matiang'i (Fred, Waziri wa Mambo ya Ndani), Kihalangwa (Gordon, Mkuu wa Idara ya Uhamiaji) wala Boinnet (Joseph, Inspekta Jenerali wa Polisi) waliofika mahakamani jana.
Nilipanga kutoa taarifa ya athari nilizopata wakati wa hukumu dhidi ya Matiang’i, Kihalangwa na Boinett chini ya Jaji Odunga. Natumaini kupewa fursa hiyo hivi karibuni.
Mimi sina hatia. Uhalifu wangu pekee ni kumwapisha Raila Odinga kuwa ‘Rais wa Watu’ Januari 30, 2018; Naongoza Vuguvugu la Taifa la Mapinduzi (NRM) ili kuleta haki za uchaguzi na kuhitimisha utawala mbaya na usio fanisi na tumedhamiria kuwaondoa madikteta kutoka nyadhifa wanazoshikilia isivyo halali!
Wakati nikirudi Kenya, iwe leo (jana) au kesho (leo), nawataka Wazalendo wa Kenya kubakia imara, kutoogopa chochote linapokuja suala la wavunja sheria na utawala wa kiimla na usio halali wa Uhuru Kenyatta na William Ruto.
Madikteta lazima waanguke, hakuna kujisalimisha, hakuna kurudi nyuma,” alimaliza Dk. Miguna huku akijitambulisha kama Jenerali wa NRM.
mwisho

Putin, Trump kukutana tena
MOSCOW, URUSI
RAIS wa Urusi, Vladimir Putin, yuko tayari kukutana na mwenzake wa Marekani, Donald Trump, licha ya uamuzi wa Washington wa kuwatimua wanadiplomasia 60 wa Urusi.
Msemaji wa Ikulu ya Urusi – Kremlin, Dmitry Peskov alisema: “Putin yuko tayari na Urusi yenyewe iko tayari kuendeleza uhusiano wa pande mbili kwa kulingana na uaminifu wa kila nchi, ikiwamo Marekani.”
Marekani na zaidi ya mataifa 20 yalitangaza kuwafukuza wanadiplomasia wa Urusi katika kile kinachoonekana ni kushikamana na Uingereza kuhusu mzozo wa mahasimu hao wa zamani wa vita baridi wa kumwekea sumu jasusi wa zamani wa nchi hizo.
Peskov amebainisha wanataraji mataifa yaliyoungana na Uingereza kufikiria upya juu ya uamuzi wao.
“Tuna matumaini nchi zilizoonyesha mshikamano na Uingereza na kuchukua uamuzi wa kufukuza wanadiplomasia wetu, zitatafakari iwapo tuhuma hizo ni za kuaminika. Hazitoshi kuwa ushahidi kwamba Urusi ilihusika na matukio ya Salisbury,” alisema Peskov.
Naye balozi wa Urusi nchini Australia, ameonya dunia inaweza kujikuta ikitumbukia katika hali ya vita baridi ikiwa mataifa ya magharibi yataendelea na chuki dhidi ya Moscow.
Uingereza tayari imewatimua wanadiplomasia 23 wa Urusi, ambayo nayo ikalipa kisasi kufukuza idadi sawa na hiyo ya wanadiplomasia.
Uingereza inadai kwamba Urusi ilitumia silaha ya kemikali kumshambulia jasusi wake wa zamani ambaye pia alikuwa jasusi wa Urusi, Sergei Skripal  kusini mwa Uingereza mapema mwezi huu.
Mwisho



Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.