DC MBEYA ALIKOLOGA



Na Pendo Fundisha Mbeya.

MKUU wa Wilaya ya Mbeya, Munasa Nyiremba Sabi,amesababisha mtafaruku mkubwa kwenye vituo vya kupigia kura baada ya kuandaa mawakala na kuwajaza vituoni kwa tiketi ya chama cha NRA huku wakiwa ni wanachama wa CCM.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika vituo mbalimbali umegundua kuwepo na mawakala waliosimamiwa na mkuu wa Wilaya hiyo baada ya kuwaita kwenye chuo  kikuu cha Mzumbe na kuwapatia barua za uwakala ambazo zimekataliwa na Tume ya uchaguzi kutokana na dosari zilizojitokeza.
Baadhi ya vituo vilivyotembelewa na gazeti hili, viliwakuta mawakala wa NRA ambao ilibainika kuwa hawajaapishwa wala kuthibitishwa na tume ya Uchaguzi wala kuapa hali iliyotiliwa shaka na mawakala wa CCM na Chadema ambao hawakufahamu uwepo wa mawakala hao.
Katika kufuatilia sakata hilo, iligundulika kuwa barua za utambulisho zilitolewa na Mkuu wa Wilaya kwa kuandaa kundi la vijana wanaokitii chama hicho lakini barua ya utambulisho ilitolewa ikionyesha kuwa ni mawakala wa NRA.
Kwamujibu wa taratibu mawakala wote waliokuwa kwenye vituo vya kupigia kura walikuwa na barua za utambulisho toka kwenye vyama vyao na barua ya Tume iliyowaidhinisha kuwa mawakala kwa kula kiapo cha utii na kupata ridhaa ya kufanya kazi hiyo.
Msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Mbeya mjini, Dkt. Samweli Lazaro alipohojiwa kuhusu tukio hilo alisema kuwa chama hicho hakina mawakala kwa kua Tume ya uchaguzi haijapata barua za kuwatambulisha mawakala hao wala kutoa barua za Tume za kuwathibitisha kufanya kazi hiyo.
“Ofisi yetu kama Tume haina taarifa  na chama hichi cha NRA, kwani hatujapokea barua ya aina yoyote na wala mawakala hao hawajaapishwa hivyo sisi hatuwatambui,” alisema Lazaro.
Aidha, baadhi ya mawakala wa NRA ambao walikutwa na barua hizo, wakiwa ndani ya vituo vya kupigia kura na baadhi yao kuhojiwa, walimtaja Mkuu wa Wilaya hiyo Munasa Sabi kuwa ndiye aliyewakabidhi barua hizo na kuwaandikia Kata wanazotakiwa kwenda kusimamia zoezi hilo huku akitambua wao ni wanachama wa CCM.
 Nuru Leonard aliyekutwa katika kituo cha Ilemi A akiwa na barua yenye kumbukumbu namba NRA/HQ-PARTY AGENTY/2015 iliyosainiwa na Hassan K Halmas kuwa ni katibu Mkuu wa chama hicho ikimtambulisha wakala huyo ambaye alipohojiwa alisema kuwa yeye ni wakala wa CCM.
Utambulisho huo, ulishitukiwa na wakala halisi wa CCM aliyekuwa katika kituo hicho bila kujua kwamba mwenzake anayemkana ni pandikizi la chama chake kwenye kituo cha kupigia kura.
Wakala mwingine wa NRA Witnes Nguwila kituo cha mtaa wa Masewe alipohojiwa alisema kuwa yeye ni mwana CCM na kwamba waliitwa na Mkuu wa Wilaya katika Chuo Kikuu cha Mzumbe na kukabidhiwa barua hizo pamoja na kulipwa posho ya shilingi 40,000 pamoja na kuelekezwa kazi watakayoenda kuifanya ikiwa ni kuhakikisha wanapiga kura kwa kujaza fomu maalum kama mawakala.
Samweli Mwandishe, aliyekutwa katika kituo cha Irowe namba moja naye akiwa na barua ya NRA na alipohojiwa na waandishi wa habari mbele ya askari polisi alijibu kuwa yeye ni mwanaCCM na yupo kwenye kituo hicho kama wakala wa NRA.
Akijibu tuhuma zilizotolewa dhidi yake Mkuu wa Wilaya hiyo Munasa Nyiremba Sabi alisema kuwa uongozi wa chama hicho ndio uliomfuata na kumuomba awasaidie kupata mawakala kwakua katika Jiji la Mbeya hawana mawakala waliowapata.
“Nakiri kufanya kazi hiyo kwakua nilifuatwa nikaitwa nikaenda kwenye chuo cha mzumbe ambako niliwasaidia kupata mawakala huku zoezi zima likiwa chini ya usimamizi wangu kama nilivyoombwa,”alisema.
Hata hivyo,mbali na hali hiyo iliyojitokeza kwa ujumla maeneo mengi yenye vituo vya kupigia kura vipatavyo 608 katika Jiji la Mbeya ilikuwa shwari na wananchi baada ya kushiriki zoezi hilo wengi walirejea makwao kuendelea na shughuli zao.
Mwisho.

Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.