Polisi wapekua nyumba ya Mbunge Lema
JESHI la
Polisi mkoa wa Arusha jana limefanya upekuzi wa zaidi ya Saa 1 katika nyumba
anayoishi Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini Godbless Lema (Chadema) iliyopo Njiro
mjini hapa.
Lema anaedelea
kushikiliwa na polisi mkoani hapa kwa ajili ya mahojiano tangu Alhamisi baada
ya kukamatwa akiwa bungeni Dodoma na kusafirishwa hadi mkoani hapa.
Aidha, Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Arusha Charles Mkumbo akizungumza na MTANZANIA Jumapili kwa
njia ya simu jana, ili kupata uhakika wa habari za kupekuwaliwa nyumbani kwa
kiongozi alisema, hawezi kutoa taarifa za mambo ya kipelelezi.
"Hayo ni
mambo ya kiuchunguzi hatuwezi kutangaza taarifa leo tunamhoji au kupekua mtu
nyumbani kwake hapana. Hatuwezi kutoa taarifa za kila kitu
tunachofanya,"alidai Kamanda Mkumbo.
Hata hivyo Mke
wa mbunge huyo Neema Lema, akizungumza kwa njia ya simu alidai kwamba ni kweli
askari polisi wakiwa na magari manne, askari wenye silaha wakiongozana na OC
CID Damass Massawe walifika nyumbani kwake kupekua.
"Sikuwepo
nyumbani kwa wakati huo. Nilikuwa nje kidogo ya mji eneo la Kisongo kumuona dada
yangu, wakati wao wakipekua. Lakini taarifa zote nimezipata kwamba wamepekua nyumba
nzima kasoro chumba tunacholala kwani nilikifunga na kuondoka na ufunguo,"
alidai Neema na kuongeza:
"Kwa
kweli hawakuondoka na kitu chochote. Lakini pia hawakusema wanatafuta nini, na
ili tu uone hakuna wanachokitafuta ni kwamba tangu juzi walipoanza kumshikilia
mpaka leo (jana) walikuwa hawajamhoji," alidai.
Wiki iliyopita Lema akiwa bungeni mjini Dodoma mara baada ya kumalizika kwa vikao kwa Bunge alitiwa nguvuni na jeshi la polisi kisha kusafirishwa usiku hadi mkoani Arusha kwa ajili ya kuhojiwa dhidi ya tuhuma zinazodaiwa kumkabili.
Akithibitisha kushikiliwa na kuhojiwa kwa Lema, ofisini kwake juzi mjini hapa Kamanda
Mkumbo alisema, ni kweli kiongozi huyo alikuwa anaendelea kushikiliwa katika mahabusu iliyopo kituo Kikuu cha Polisi mjini hapa.
"Ni kweli
tunamshikilia yupo mahabusu, tunaendelea kumhoji kuna mambo bado tunakamilisha
ya kiuchunguzi,tukimaliza kumhoji tutamfikisha mahakamani,"alisema Kamanda
Mkumbo
Novemba Mosi,
Mwaka huu Lema alikamatwa na polisi akidaiwa kutoa lugha zenye uchochezi dhidi
ya Rais Dk. John Magufuli, katika mikutano yake hadhara ya Jimbo ambapo
alihojiwa na kuachiwa kwa dhamana.
Akifafanua madai
hayo Kamanda Mkumbo alisema zipo baadhi ya tuhuma ambazo hawakuwa wamemuhoji.
Hivyo kukamatwa kwake ni muendelezo wa upelelezi kabla hawajamfikisha mahakamani."Tunamshikilia Lema hatutampa dhamana mpaka tumalize kumhoji, kuna masuala tulikuwa hatujamhoji juzi na akimaliza kuhojiwa atapelekwa mahakamani,"alidai.
Alisema wanaendelea kumhoji Lema kwa tuhuma za kutoa lugha zenye uchochezi dhidi ya Rais Dkt. Magufuli, kupitia mikutano ya hadhara aliyoifanya katika jimbo hilo.
“Alitoa lugha
zenye uchochezi kinyume cha sheria na baadhi ya maneno aliyotoa yenye uchochezi
ni kama “Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiendelea kugandamiza
dekomrasia siasa za ugandamizaji taifa litaingia katika umwagaji wa damu,”alinukuu
Kamanda Mkumbo na kuongeza:
\
“Nchi hii
inaandaliwa kwenda katika utawala wa kidikteta na pia aliwataka wananchi wawe
tayari kwa lolote na waache kabisa uoga kwani uoga ni dhambi mbaya kuliko
dhambi zote duniani,” alisema.
Comments
Post a Comment