WAZIRI MKUU MWIGULU ALIFUNGA BUNGE NA KUWATAKA WATANZANIA WATUNZE AMANI
HOTUBA
YA MHESHIMIWA DKT. MWIGULU LAMECK NCHEMBA (MB.), WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA
MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUAHIRISHA MKUTANO WA TATU (3) WA BUNGE LA 13 LA
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA TAREHE 26 JUNI, 2026
JIJINI DODOMA
1.
Mheshimiwa Spika, awali ya yote ninamshukuru
Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa fadhili zake zilizotuwezesha sote kuiona
siku hii muhimu katika historia ya Bunge la 13. Kama mnavyofahamu, tumekutana
leo kwa ajili ya kuhitimisha mkutano wa Tatu ambao ulikuwa mahsusi kwa ajili ya
kupokea na kujadili bajeti ya serikali.
2.
Mheshimiwa Spika, nimesema leo ni siku muhimu na ya
kihistoria kwa sababu, hii ni Bajeti ya kwanza ya Serikali kupitishwa na Bunge
la 13 baada ya uchaguzi mkuu wa 2025. Hongereni sana waheshimiwa Wabunge!
3.
Mheshimiwa Spika, kwa unyenyekevu mkubwa, ninaomba
nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maono na uongozi wake thabiti wakati
wote wa kipindi cha mkutano huu wa Tatu (3) wa bunge la bajeti. Wakati wote
amekuwa akinipa maelekezo yenye tija na kuifanya kazi yangu kuwa nyepesi.
4.
Mheshimiwa Spika, sina shaka nyote mtakubaliana
nami kuwa utayari wake na hamasa kubwa aliyokuwa nayo katika kuwatumikia
watanzania imekuwa ni mfano wa kuigwa. Pia, hulka yake na ustahimilivu wake
umekuwa faraja kwetu sisi wasaidizi wake, watumishi wote wa umma na Watanzania
wote kwa ujumla.
5.
Mheshimiwa
Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Balozi Dkt. Emmanuel John
Nchimbi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano wake
alionipatia wakati wote nikitekeleza majukumu yangu. Busara zake na weledi wake
umekuwa msaada na mfano wa kuigwa katika utendaji kazi Serikalini.
6.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumshukuru
sana Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti
wa Baraza la Mapinduzi kwa ushirikiano mkubwa alionipatia wakati wote.
Kadhalika, ninatoa shukrani kwa Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla, Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar na Ofisi yote ya Makamu wa Pili wa Rais kwa
ushirikiano wakati nikitekeleza majukumu yangu.
7.
Kipekee
nitumie nafasi hii kukushukuru sana wewe binafsi Mheshimiwa Mussa Azan Zungu,
Mbunge wa Ilala, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hakika umeendelea
kudhihirisha uzoefu wako kwenye shughuli za Kibunge na umekuwa tafsiri sahihi
ya kiongozi shupavu na mwenye uweledi mkubwa katika kuliongoza Bunge hili la 13.
8.
Mheshimiwa
Spika,
uzoefu wako wakati wote umeendelea kuwa na tija kubwa katika utendaji wa
shughuli za serikali bungeni. Ninakushukuru sana kwa namna ulivyoendesha
mijadala yote ya bajeti za kisekta katika mkutano huu wa tatu pamoja na
kupitisha makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2026/2027.
9.
Mheshimiwa Spika, vilevile, nitumie nafasi hii
kutoa shukrani kwa Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini na
Naibu wa Spika pamoja na Mheshimiwa Najma Murtaza Giga (Mbunge wa Viti Maalum),
Mheshimiwa Deodatus Philip Mwanyika Mbunge wa Njombe Mjini na Mheshimiwa Cecilia
Daniel Paresso, (Mbunge wa Viti Maalum) kwa nafasi zao za Wenyeviti wa Bunge.
Wakati wote mmekuwa mkinipa ushirikiano wa kutosha wakati mlipokuwa mkimsadia
Mheshimiwa Spika katika shughuli za kuendesha Bunge hili tukufu.
10.
Mheshimiwa Spika, ninatoa shukrani zangu za dhati
kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa kufanya kazi kubwa kipindi chote cha
utekelezaji wa shughuli za Mkutano wa tatu mahususi wa kupitisha mpango na
bajeti. Waheshimiwa wabunge mmefanya kazi kubwa, hakika mnastahili pongezi.
11.
Mheshimiwa Spika, maoni, ushauri na michango yenu
katika mkutano huu yamekuwa yakitoa mwelekeo sahihi katika mipango na utendaji
wa shughuli za Serikali na imegusa moja kwa moja maisha ya wananchi wote. Pia
ninawapongeza kwa kazi kubwa mliyoifanya tarehe 23 Juni, 2026 ya kupitisha kwa
kura ya ndiyo Bajeti ya Serikali ya mwaka 2026/2027 ya shilingi trilioni 62.33
kwa kura za asilimia 97.66 Hongereni sana waheshimiwa wabunge na hiyo kazi
kubwa mliyoifanya na kwa imani mliyokuwa nayo kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia
Suluhu Hassan. Serikali ilijipanga, imesikiliza hoja zenu na kutoa ufafanuzi na
sasa ipo tayari kwenda kutekeleza Bajeti kwa kuzingatia yote mliyoshauri.
12.
Mheshimiwa Spika, ninaomba sasa nitumie nafasi hii
kuwapongeza Mawaziri, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Naibu Mawaziri, Wakuu wa
Mikoa, Katibu Mkuu Kiongozi, Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala, Naibu Makatibu
Wakuu, Watendaji Wakuu wa Taasisi za Serikali na Watumishi wote umma kwa
kufanikisha kupitishwa Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Pongezi za Teuzi na Chaguzi
Mbalimbali
13.
Mheshimiwa Spika, kama mtakavyokumbuka ninaomba
niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pongezi nyingi kwa Mheshimiwa
Emmanuela K. Mtatifikolo, Mbunge wa Jimbo la Ismani kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge
wa Jimbo hilo kufuatia uchaguzi mdogo uliofanyika hivi karibuni (wakati mkutano
huu ukiendelea). Ushindi huo, unadhihirisha kwamba wananchi jimbo la Ismani wana
imani kubwa na Chama cha Mapinduzi kutokana uongozi thabiti, sera makini pamoja
na Ilani ya Uchaguzi inayotekelezeka. Nitumie fursa hii kumkaribisha sana
Mheshimiwa Emmanuela K. Mtatifikolo na nimhakikishie kuwa Waheshimiwa Wabunge
wote tutampa ushirikiano mkubwa ili aweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu
ya kuwakilisha wananchi wa jimbo la Ismani.
14.
Mheshimiwa Spika, wakati mkutano wa tatu wa Bunge
ukiendelea, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania alifanya teuzi mbalimbali.
Teuzi hizo zilifanywa kwa lengo la kutekeleza na kuimarisha utoaji wa
huduma kwa wananchi na shughuli mbalimbali za serikali na mihimili mingine.
15.
Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 02 Mei, 2026 Mheshimiwa
Rais, alimteua Mheshimiwa Dkt. Evaline Wilbard Munisi (Mb.), kuwa Naibu Waziri,
Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano). Pia, Mheshimiwa Rais alimteua
Dkt. John Antony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.
16.
Mheshimiwa Spika, vilevile aliteua wakuu wa taasisi,
mabalozi na wateule wengine katika nafasi mbalimbali. Nitumie nafasi hii
kuwatakia wateule wote kila la heri katika utekelezaji wa majukumu yao mapya na
kuwakumbusha wajibu wao wa kutanguliza mbele maslahi ya Taifa letu mbele na kuwahudumia
watanzania wote.
Salamu za Pole
17.
Mheshimiwa Spika, wapo Watanzania wenzetu waliokumbwa
na majanga mbalimbali zikiwemo ajali za barabarani. Ninatoa pole kwa wananchi
wote waliopoteza wapendwa wao katika ajali hizo. Vilevile, ninatoa pole kwa
majeruhi wote na ninawaombea kwa Mwenyezi Mungu awape uponyaji wa haraka. Nitumie nafasi hii pia, kutoa pole kwa
waathirika wa majanga mengine yote yaliyotokea na hatujayataja.
2.0
SHUGHULI
ZA BUNGE
Maswali na Majibu
18.
Mheshimiwa Spika, leo
wakati tunahitimisha shughuli za mkutano wa tatu wa Bunge la 13, tumefanikiwa
kutekeleza masuala mbalimbali ikiwemo wajibu wa msingi kutunga sheria,
kupitisha bajeti na hoja mbalimbali zilizojitokeza. Shughuli hizo ni kujibu
maswali na hoja zilizowasilishwa na Waheshimiwa Wabunge; kujadili na kupitisha
Miswada ya Sheria ya Serikali; na kujadili na kutoa Maazimio mbalimbali. Katika
mkutano huu, maswali ya msingi 696 na ya nyongeza 2,591 na
maswali 31 ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu yaliulizwa na kupatiwa
majibu.
Miswada
19.
Mheshimiwa
Spika, kwa
upande wa miswada bunge lako tukufu katika Mkutano huu, Bunge lako tukufu
limepokea Miswada mitano (05) ambayo ilisomwa katika
hatua mbalimbali ambayo ni:
Moja: Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2026 (The Finance Bill,
2026), uliosomwa kwa hatua zote;
Mbili: Muswada wa Sheria ya Matumizi wa Mwaka 2026 (The
Appropriation Bill, 2026) , uliosomwa kwa hatua zote;
Tatu: Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya
Sheria Mbalimbali (Na. 02) wa Mwaka, 2026 [The Written Laws (Miscellaneous
Amendments) (No. 02) Bill, 2026], uliosomwa kwa mara ya kwanza;
Nne: Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya
Sheria za Kilimo wa Mwaka 2026 [The Agricultural (Amendments) Bill, 2026], uliosomwa
kwa mara ya kwanza; na
Tano: Muswada wa Sheria ya Kufuta Sheria ya
Tasnia ya Pareto wa Mwaka 2026, nao uliosomwa
kwa mara ya kwanza.
Azimio
20.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 61 na
107 hadi 112 za Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Februari 2023, na kwa
kuzingatia wajibu wa Bunge, Bunge lako tukufu lilipokea na kujadili Azimio moja
ambalo ni:
Azimio la Bunge kuhusu Kuipongeza
Timu ya Taifa ya Vijana Wanaume Chini ya Umri wa Miaka 17 yaani (Serengeti
Boys) kwa Kufuzu Fainali za AFCON 2026 na Kukata Tiketi ya Kushiriki Mashindano
ya Kombe la Dunia la Vijana Chini ya Umri wa Miaka 17 kwa Mwaka 2026. Nirejee kuwapongeza sana vijana
wetu kwa kuweka historia hiyo!
3.0
MAFANIKIO
NA VIPAUMBELE VYA SERIKALI
Mafanikio ya Utekelezaji wa Bajeti ya
Mwaka 2025/2026
21.
Mheshimiwa
Spika,
nitumie fursa hii kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu
Hassan, kwa uongozi wake thabiti na dhamira yake ya kuhakikisha fedha za umma
zinatumika kwa weledi mkubwa katika kutekeleza miradi ya maendeleo. Dhamira
hiyo imekuwa msingi wa mafanikio makubwa tunayoyashuhudia katika mwaka wa fedha
ambao tunaouhitimisha.
22.
Mheshimiwa
Spika, kwa
kuzingatia maono na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan,
Serikali ya Awamu ya Sita imepata mafanikio makubwa katika utekelezaji wa Ilani
ya Mwaka 2020 na Dira ya 2025 kupitia sekta mbalimbali. Mafanikio hayo yamebainishwa
kwa kina wakati nilipowasilisha Bungeni Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali
na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya
Bunge kwa Mwaka 2026/2027.
23.
Mheshimiwa
Spika, pia,
mafanikio hayo katika maeneo ya miundombinu, sekta za uzalishaji, huduma za
jamii na masuala mtambuka na yamebainishwa
kwa ufasaha na Mawaziri wa Kisekta kupitia bajeti za wizara zao katika kipindi
cha mwaka wa fedha 2025/2026. Mafanikio kwenye sekta na maeneo
hayo yameendelea kuwa faraja na ukombozi kwa wananchi wa kipato cha chini ikiwemo
wakulima, wafanyabiashara wadogo, waendesha bodaboda na mama/babalishe na
maeneo mengine. Haya yote ni matunda ya uongozi makini wa Mheshimiwa Rais na
dhamira yake ya dhati ya kustawisha maisha ya Watanzania kuwa ya staha na utu
bila kumwacha mtu nyuma.
Kuimarisha
Diplomasia Kiuchumi na Ushirikiano wa Kimataifa
24.
Mheshimiwa
Spika, ni
jambo la kujivunia kuona jinsi Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan,
alivyoendelea kuitangaza na kuiwakilisha vema Tanzania katika jukwaa la kimataifa.
Mheshimiwa Rais, ameendelea kuonesha uongozi wa hekima na kuendelea
kushirikiana na mataifa mbalimbali na asasi za kimataifa.
25.
Mheshimiwa
Spika,
Mheshimiwa Rais ameendelea kusukuma mbele ajenda ya diplomasia ya kiuchumi kwa
vitendo, akithibitisha kuwa Tanzania ni mshirika wa kuaminika katika biashara
na kiuwekezaji. Tumeshuhudia ziara za viongozi wenzake kutoka Ghana, Kenya,
Uganda, Rwanda, Singapore na hivi majuzi
kiongozi kutoka Namibia.
26.
Mheshimiwa
Spika, ziara
hizo zilifanikisha makubaliano pamoja na kusaini mikataba muhimu katika maeneo
ya biashara, uchukuzi, nishati na miundombinu. Aidha, Mheshimiwa Rais, alipokea
Hati za Utambulisho kutoka kwa Mabalozi wanane, akisisitiza umuhimu wa nchi za
Afrika kuongeza thamani ya rasilimali zake.
27.
Mheshimiwa
Spika,
Mheshimiwa Rais pia ameitangaza Tanzania kama kituo cha uwekezaji wa kimataifa
kupitia ziara zake za kikazi nje ya nchi. Akiwa amefanya ziara na kushiriki
mikutano ya kikazi na kiserikali katika nchi za Falme za Kiarabu (Dubai) na
Urusi. Akiwa nchini Urusi, Mheshimiwa Rais alitoa wito wa uwekezaji zaidi
katika Bara la Afrika, akiitangaza Tanzania kama lango la kimkakati la biashara
katika eneo lenye soko la zaidi ya watu milioni 500.
Kutunukiwa Shahada
ya Uzamivu
28.
Mheshimiwa
Spika, ni
heshima kubwa kwa Taifa letu kuona Mheshimiwa Rais akitunukiwa Shahada ya
Heshima ya Uzamivu na Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi kwa mchango wake
mkubwa katika elimu, ushirikiano wa kimataifa na urafiki kati ya mataifa haya.
Heshima hii hutolewa kwa nadra kwa viongozi wachache duniani, ni kielelezo cha
namna jamii ya Kimataifa inavyothamini uongozi wa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia
Suluhu Hassan. Tunampongeza kwa dhati Mheshimiwa Rais kwa heshima hii
inayotuangazia sote kama Taifa.
4.0
MAMBO
YALIYOTILIWA MSISITIZO KATIKA MJADALA WA BAJETI YA 2026/2027
Vipaumbele vya Sekta kwa Mwaka 2026/2027
29.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali inaendelea kulihakikishia Bunge lako na wananchi kwa ujumla kwamba vipaumbele
vya Bajeti ya mwaka 2026/2027 kwa kila Wizara za Kisekta vimezingatia maslahi
mapana ya Taifa. Bajeti hii, itaendelea kuimarisha uwekezaji katika sekta za
uzalishaji, miundombinu na huduma za jamii. Serikali imejipanga kuendelea kuimarisha
mikakati na mifumo mapato ya ndani na kupunguza utegemezi wa mikopo na misaada
kutoka nje. Mikakati moja wapo ni kupunguza utegemezi kutoka nje. Nimpongeze
mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa wasilisho la Bajeti hiyo!
Kuimarisha Uwezeshaji wa Makundi
Maalum
30.
Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla
wameshuhudia kusomwa kwa bajeti ya mwaka 2026/2027. Bajeti hiyo, inaenda kugusa
na kuweka mazingira wezeshi ya kuvutia urasimishaji wa sekta isiyo rasmi ambayo
inaajiri zaidi vijana na wanawake.
31.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza azma hiyo, Serikali kupitia
Mamlaka za Serikali za Mitaa inaenda kutenga asilimia 15 ya mapato yao ya ndani
badala ya asilimia 10 iliyopo sasa ya mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye
ulemavu. Kati ya asilimia 15 itakayotengwa, asilimia 10 itaelekezwa kwenye
mikopo ya wanawake, vijana na wenye ulemavu kwa uwiano kama ilivyokuwa awali.
Aidha, asilimia tano itatumika kwa ajili ya uwekezaji kwenye miradi ya ujenzi
na maboresho ya masoko na maeneo ya biashara na ujasiriamali ili kuvutia na
kuongeza fursa za ajira hususan kwa vijana, wanawake na makundi maalum.
32.
Mheshimiwa Spika, nizielekeze mamlaka za serikali za mitaa kutenga
maeneo ya wajasiriamali kwa kuzingatia urahisi wa kufikika na kuwezesha kufanya biashara kwa
tija. Hivyo, kupitia asilimia 5 ya uboreshaji wa miundombinu ya wajasiriamali,
pale inapohitajika halmashauri zilipe fidia wazidishe kufanya hivyo ili
kuwezesha upatikanaji wa maeneo yenye sifa kwa wajasiriamali kupata tija katika
shughuli zao ili tuache kufukuzana na wajasiriamali tuwapatie maeneo ya kufanya
biashara ili yakidhi tija zao.
33.
Mheshimiwa Spika, aidha,
kupitia utaratibu mpya wa utoaji mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya
ndani ya halmashauri. Ninazielekeza taasisi za fedha na waratibu wa mikopo hiyo
kuondoa masharti magumu yanayokwamisha wajasiriamali kunufaika na mikopo hiyo.
Mfano ulazima wa wahitaji kwa upande wa watu (walemavu) kuunda vikundi na
ulazima wa wahitaji kuwasilisha dhamana kubwa kama vile hati za nyumba kwa
asili ya biashara zao hawawezi kuwa nazo. Nitumie fursa kwa vijana kutumia hiyo
vizuri.
Maeneo Yaliyofanyiwa Maboresho ya
Kodi
34.
Mheshimiwa Spika, ili kuwavutia wajasiriamali, Serikali itatoa
msamaha wa kodi ya mapato kwa wafanyabiashara wadogo ambao ni wapya kwa kipindi
cha mwaka mmoja tangu tarehe ya kupata namba ya utambulisho wa mlipakodi. Hatua
hii itawezesha mama na baba lishe, waendesha bodaboda na bajaji, mafundi
seremala na wachomeleaji na wengine wenye shughuli ndogondogo n.k kuanzisha
biashara zao pasipo kuwepo changamoto ya kudaiwa kodi ndani ya mwaka mmoja,
muda huo unatoa fursa ya kujiimarisha katika biashara wanazozianzisha.
Mheshimiwa tumetolea mfano kwa wafugaji wenye ndama wao ili waweze kuwakuza na
kufanya biashara.
Kukamilisha Miradi na Programu za Maendeleo
35.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuweka nafuu mbalimbali za
kikodi zinazochochea matumizi ya nishati ya umeme na gesi asilia majumbani na katika
sekta ya usafiri ili kukabiliana na athari kutokana na migogoro mashariki ya
kati. Hivyo, Serikali itasamehe kodi kwenye vifaa vitakavyotumika katika vituo
vya kuchaji magari yanayotumia umeme na kupunguza ushuru wa forodha kutoka
asilimia 25 hadi asilimia 10. Nitoe rai kwa wawekezaji na sekta binafsi kwa
ujumla watumie fursa hiyo kuagiza mashine na vipuri vitakavyotumika kwenye
vituo hivyo.
Kuendelea Kuimarisha Sekta za Uzalishaji
36.
Mheshimiwa Spika, katika kutambua kuwa sekta ya kilimo nchini inabeba
makundi mengi katika uzalishaji na biashara, Serikali imeweka vivutio
mbalimbali vya kikodi ili kuhamasisha kilimo na matumizi ya mbegu za mafuta
zinazozalishwa nchini. Aidha, nafuu hii ni pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa
bidhaa hii kwa gharama nafuu na kulinda viwanda vya ndani vinavyochakata na
kuzalisha mafuta ya kula yanayotokana na michikichi, soya, karanga pamoja na
nazi.
37.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuweka mazingira bora kwa
kuhakikisha viwanda vya ndani vinazalisha na kuwa shindani dhidi ya bidhaa
zinazoingizwa nchini. Hatua hiyo, ni sehemu ya kuongeza kiwango cha Ushuru wa
Forodha kwenye bidhaa mbalimbali zinazoagizwa kutoka nje ya nchi kwa lengo la kulinda viwanda vya ndani na kuhamasisha uwekezaji nchini.
38.
Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa rai kwa Watanzania wote, kutumia
nafuu hizi za kikodi zilizotolewa na Serikali kufuatia hotuba nzuri iliyotolewa
na Waziri wa Fedha kwa kuongeza uwekezaji katika sekta ya uzalishaji kuliko
kufuata faida binafsi. Hatua hii, itaendelea kutanua wigo wa kutoa ajira kwa
vijana ambao kwa sehemu kubwa ndio wamekuwa kwenye changamoto ya ukosefu wa
ajira.
Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji
Nchini
39.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa sekta ya biashara na
uwekezaji nchini, Serikali imefanya maboresho katika sheria 55 ambapo pamoja na
mambo mengine ada na tozo 374 zimepunguzwa au kufutwa. Lengo la hatua hiyo, ni
kupunguza gharama za kufanya biashara, kuimarisha mazingira ya uwekezaji pamoja
na kuongeza usajili wa biashara na uwekezaji hapa nchini. Hizi ni hatua muhimu
za kuweka mazingira muhimu ya uzalishaji na kutoa tozo.
40.
Mheshimiwa Spika, serikali imezingatia maoni ya waheshimiwa wabunge
kuhusu kero ya wingi wa ada, tozo na adhabu zinazotolewa na mamlaka za
udhibiti wa ufanyaji biashara na
uwekezaji. Hivyo, Serikali imedhamiria kuanzisha mfumo jumuishi ili kutatua
kero hizo bila kuathiri majukumu ya msingi yanayofanywa na taasisi za udhibiti.
Sekta za Kimkakati Zilizoongezewa
Fedha
41.
Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa fedha zaidi kwa baadhi ya sekta za
kimkakati ili kuziwezesha kukamilisha miundombinu na kurahisisha upatikanaji wa
huduma muhimu karibu na maeneo ya wananchi. Lengo ni kukamilisha miundombinu ya
Reli ya SGR, ujenzi wa barabara, upanuzi
wa Bandari ya Dar es Salaam na viwanja vingine. Pia, itashusha gharama za
usafiri na usafirishaji na kuleta unafuu kwa mwananchi. Tutaweka nguvu kubwa
kwenye vipande vya reli ambavyo hajakamilika ili mpaka mwaka 2030 tuna na treni
kutoka da es salaam hadi mwaza.
42.
Mheshimiwa Spika, katika sekta ya madini, serikali imetenga fedha za
kuweka mazingira wezeshi kwenye ujenzi wa viwanda vya kusafisha dhahabu, nickel,
graphite, uranium na uboreshaji wa ramani za kina za madini nchini. Hatua
hiyo itavutia uwekezaji na kusaidia wachimbaji wadogo kupata masoko, teknolojia
na kuacha kuuza madini ghafi yanayopunguza thamani ya madini yao.
Hali ya Upatikanaji wa Nishati ya Mafuta Nchini
43.
Mheshimiwa Spika, nimpongeze waziri wa sekta na Serikali itaendelea
kusimamia mpango wa kupunguza makali ya
nishati ya mafuta. tangu kuanza kwa vita Mashariki ya Kati Serikali ilichukua
hatua za haraka kuhakikisha nishati ya mafuta inapatikana nchini. Serikali ilitoa
ruzuku ya shilingi bilioni 50 kwa mwezi Mei, 2026 na shilingi bilioni 90 kwa
mwezi Juni, 2026 ili kuwa na bei himilivu tofauti na
ilivyotarajiwa endapo ruzuku isingekuwepo. Serikali itaendelea kufanya tathmini
ya mwenendo wa bei za mafuta katika soko la dunia na kuchukua hatua stahiki ili
kupunguza athari na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta wakati wote.
Kuimarisha Mtiririko wa Fedha katika Mifuko ya Miradi ya
Maendeleo
44.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwapongeza waheshimiwa wabunge kwa
kuwa mstari wa mbele kuhakikisha wananchi katika majimbo yao wanapata maendeleo
kwenye sekta mbalimbali ikiwemo maji, barabara na umeme. Kwa umahiri mkubwa,
waheshimiwa wabunge wameishauri Serikali kuchukua hatua za haraka kuwezesha
sekta hizo kupata fedha kwa wakati.
45.
Mheshimiwa Spika, Serikali imepokea ushauri huo na itaendelea kuboresha
utaratibu wa utoaji wa fedha hizo kama ilivyoshauriwa. Kwa sasa asilimia 70 ya fedha
za mifuko ya maendeleo zitaelekezwa moja kwa moja kwenye mifuko husika ili
uweze kutekeleza majukumu yake ya kimsingi. Uamuzi huo utaongeza kasi na
uhakika wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kupanua wigo wa huduma za
jamii na kuongeza fursa za uzalishaji.
46.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha watendaji wa Taasisi
ambazo zitapelekewa fedha hizo kuhakikisha wanakamilisha miradi iliyokusudiwa tena
kwa kuzingatia thamani ya fedha na miradi iwe na uimara. Wakumbuke kuwa dhamira
na maelekezo ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ni kutekeleza kikamilifu miradi ya maendeleo kwa ajili ya
ustawi wa Watanzania. Serikali itachukua hatua kwa watendaji wote ambao
watashindwa kutekeleza maelekezo hayo.
47.
Mheshimiwa
Spika, kwa niaba ya Serikali, Wabunge
na Watanzania wote, ninaomba nitoe shukrani za pekee kwa Mheshimiwa Rais, Dkt.
Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutoa fedha za kutekeleza miradi ya
maendeleo kwa uwazi na uwajibikaji. Tumuombee Mungu aendelee kuwa na afya njema
na hekima zaidi ili aendelee kuiongoza nchi yetu kwa mafanikio makubwa. Ameendelea kuziongezea fedha taasisi za
ukaguzi ili waendelee kufanya ukaguzi wakati miradi inaendelea ikiwa ni dhamira
ya kuleta ustawi kwa watanzania.
Masuala ya Ardhi
48.
Mheshimiwa
Spika, katika ziara nilizofanya maeneo
mengi nchini, kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusiana na migogoro
ya ardhi. Baadhi ya masuala yao yalifikishwa kwenye Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya
lakini hayakupata ufumbuzi kamili. Itakumbukwa kwamba, Mfumo wa Mabaraza ya
Ardhi ulianzishwa miaka ya nyuma wakati mahakama za hakimu mkazi na wilaya zikiwa
chache katika maeneo mengi.
49.
Mheshimiwa
Spika, kutokana
na uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali ya awamu ya sita, sote tumeshuhudia
ongezeko kubwa la mahakama za wilaya hapa nchini. Ili kuongeza ufanisi wa
kushughulikia maamuzi ya migogoro ya ardhi, katika mkutano ujao wa Bunge, Serikali
itawasilisha mapendekezo ya kuhamishia masuala hayo kutoka Mabaraza ya Ardhi kwenda
kwenye mfumo rasmi wa mahakama. Nitoe rai kwa watanzania wote tuache kuaminiana
na kutoa ardhi bila ya kufuata misingi ya kisheria.
Masuala ya Utoaji Haki
50.
Mheshimiwa
Spika, pia kwa nyakati mbalimbali, nimepokea
changamoto wanazokutana nazo baadhi ya wafugaji kwa mifugo yao kutaifishwa baada
ya kukamatwa kwenye maeneo yaliyohifadhiwa wabunge wengi wameongelea suala hilo.
Baada ya mashauri haya kuhitimishwa katika vyombo vya sheria kwa wafugaji
kupata ushindi na kuamriwa warejeshewe mifugo yao, taasisi husika
hazijatekeleza maamuzi ya mahakama na kuishia kuwaambia mifugo yao imekufa,
imepokea ama sababu nyingine. Vitendo hivi vinaidhoofisha sekta ya mifugo na kuwaacha
wananchi hawa katika ufukara.
51.
Mheshimiwa
Spika, Ili
kuimarisha misingi ya utawala wa kisheria na utoaji haki kwa wananchi, kupitia
mkutano ujao wa bunge, Serikali itawasilisha mapendekezo ya marekebisho ya
sheria zinazosimamia utaifishaji mifugo na mali kwenye maeneo yaliyohifadhiwa
tunakwenda kuifuta sheria inayotaifisha mifugo ya watanzania. Kwa sasa, Wizara
ya Fedha kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii wahakikishe wanatekeleza
maamuzi yaliyotolewa na mahakama ya kuwarejeshea wananchi mifugo yao na kama mifugo hiyo
ilikufa au kupotea walipe fidia kwa mifugo iliyopotea.
Ukamataji wa Mali na Mitaji ya Wajasiriamali
52.
Mheshimiwa
Spika,
katika maeneo mengi nchini, kumejitokeza vitendo vya baadhi ya watendaji wa
mamlaka za udhibiti na usimamizi wa sheria kunyang’anya bidhaa, mitaji na
vitendea kazi vya wajasiriamali mbalimbali. Vitendo hivi, havikubaliki na
vinarudisha nyuma jitihada za wananchi kujikwamua kiuchumi, licha ya serikali
kuweka mazingira mazuri ya kuwawezesha wananchi hao waweze kutekeleza majukumu
yao. Kama msimamizi wa shughuli za kiserikali nitaendelea kuchukua hatua kali
ili kukomesha tabia hii.
53.
Mheshimiwa
Spika, niendelee
kusisitiza maelekezo ya serikali kwa watendaji kuheshimu jasho la mtanzania,
shughuli zainazofanywa na mtanzania, mitaji na shughuli zinazofanywa na
wajasiriamali kote nchini. Dosari zozote zinazojitokeza katika shughuli zao
zishughulikiwe kwa kutumia njia zisizohusisha kukamata mali na mitaji yao isipokuwa kwa makosa ya kijinai
na yanayohatarisha usalama.
5.0
UWAJIBIKAJI
WA WATUMISHI WA UMMA
Mahusiano ya Viongozi na Watendaji
54.
Mheshimiwa
Spika, ili
utoaji wa huduma kwa wananchi na utekelezaji wa shughuli za Serikali vifanyike kwa ufanisi, ni muhimu sana kwa viongozi, watendaji na watumishi wote kuwa na
mahusiano mazuri katika dhana hii ya uwajibikaji. Hali hiyo itachangia kuepusha
migogoro na migongano baina ya viongozi, watendaji na watumishi, na hivyo kupunguza
tija katika shughuli za serikali na kuwahudumia wananchi.
55.
Mheshimiwa
Spika, ikumbukwe
kwamba serikali imeanza kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025 na kuanzia
tarehe 01 Julai 2026, Serikali itaanza kutekeleza rasmi Dira 2050 na ndio kwa
mara ya kwanza tuanenda kutekeleza Bajeti ya Kwanza ya Serikali ya Awamu ya
Sita. Hivyo ni wajibu wa kila mmoja kujielekeza katika kuwezesha wananchi
kupata manufaa ya mipango ambayo imesomwa na Waziri wa Mipango. Viongozi waepuke
kuendeleza makundi na makovu ya uchaguzi uliopita na kupanga safu za uchaguzi ujao. Hali hiyo inaweza kuchochea migogoro
itakayosababisha kuchelewesha utekelezaji wa Ilani na kutoa huduma bora kwa
wananchi.
Muda wa Uongozi wa Naibu Meya na Makamu
Mwenyekiti
56.
Mheshimiwa
Spika, katika
usimamizi wa shughuli kwenye mamlaka za serikali za mitaa, kila mwaka serikali
inaingia gharama za uchaguzi ambapo viongozi na watendaji kuwa katika mchakato
wa uchaguzi. Mazingira hayo yanazorotesha utendaji, yanachochea migongano na
kuondoa utulivu kwenye mamlaka za serikali za mitaa.
57.
Mheshimiwa
Spika, ninapenda
kulijulisha Bunge lako tukufu katika mkutano ujao, Serikali itawasilisha
mapendekezo ya marekebisho ya sheria kuhusu nafasi za Naibu Meya na Makamu Mwenyekiti
wa Halmashauri. Tuaondoa uchaguzi kufanyika kila mwaka. Lengo ni kubadilisha
mfumo wa sasa na kuwa na Naibu Meya na Makamu Mwenyekiti kuwa kiongozi kwa
kipindi chote cha uhai wa Baraza la Madiwani. Marekebisho hayo yanatarajia
kuleta utulivu, viongozi wajikite katika kufanya kazi na kujiekeleza kwenye
shughuli za maendeleo ya wananchi katika maeneo yao. Mambo ya safu na kuwaza
uongozi ni ubinafsi.
Utatuzi wa Kero za Wananchi
58.
Mheshimiwa
Spika,
ziara za viongozi wa kitaifa katika maeneo mbalimbali nchini ni sehemu ya
majukumu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa shughuli za serikali ikiwemo utoaji
wa huduma bora kwa wananchi. Katika ziara hizo wananchi wengi wamekuwa
wanajitokeza kuwasilisha kero mbalimbali. Baadhi ya kero hizo, ilitarajiwa ziwe
zimetatuliwa na viongozi waliopo kwenye mamlaka za serikali za mitaa.
59.
Mheshimiwa
Spika,
ninawakumbusha viongozi na watumishi wote wa umma kwamba utatuzi wa kero za
wananchi ni sehemu ya majukumu yao ya kila siku. Aidha, ziara za viongozi wa
Kitaifa ikiwemo ziara ya Waziri Mkuu siyo mbadala wa kutoa huduma hizo kwa
wananchi. Hivyo ninatoa maelekezo yafuatayo:
Mosi: Wizara, Idara, Sekretarieti
za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa zihakikishe Mifumo iliyopo kwenye
Mamlaka za Serikali za Mitaa kuanzia ngazi ya mtaa/kijiji inatoa huduma kwa
wananchi ipasavyo;
Pili: Viongozi waendelee kutekeleza majukumu yao badala kusubiri teuzi
“PDF/MKEKA”. Suala la uteuzi lisiathiri utendaji kazi na dhamana ambazo
zimetolewa na mamlaka ya uteuzi. Mamlaka inaendelea kufanya tathmini na wote
wasiotimiza wajibu wao ipasavyo ikiwemo kuwahudumia wananchi watachukuliwa
hatua; na
Tatu: Viongozi na watendaji katika kila ngazi wasimamie na kutekeleza
kwa ukamilifu maagizo na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na viongozi wa
kitaifa ikiwemo kwenye ziara ikiwemo kutatua na kusikiliza kero za wananchi. Taasisi
zote zitenge muda wa kusikiliza changamoto za utoaji huduma katika maeneo yao. Ufuatiliaji
unaendelea kufanyika na viongozi
watapimwa kwa namna wanavyotekeleza maagizo hayo.
Wananchi
Kuzingatia Mifumo ya Serikali
60.
Mheshimiwa
Spika,
ninatoa rai kwa wananchi wote kuwa pamoja na uwepo wa ziara za viongozi wa
kitaifa kwenye maeneo yao, waithamini, waiamini na kuitumia mifumo ya kiutawala
iliyopo nchini ili kupata utatuzi wa kero na malalamiko mbalimbali. Ziara
tunazofanya sio mbadala wa mifumo rasmi iliyopo hivyo wasisubiri ziara za
viongozi wa kitaifa.
61.
Mheshimiwa
Spika, Nina
hakika Wizara, Idara, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa
halmshauri na watendaji wengine wanao uwezo wa kutatua kero mbalimbali. Mheshimiwa
Rais amewapa dhamana ya kuwawakilisha kwenye maeneo yaliyopo watimize wajibu
wao.
62.
Mheshimiwa
Spika,
sambamba na mifumo hii ya kiutawala iliyopo, Serikali imeweka mifumo ya
kieletroniki kwa ajili ya wananchi kuwasilisha kero na maoni mbalimbali
Serikalini. Mifumo hiyo ni pamoja na e-mrejesho, e-kiongozi, sema
na waziri (wizara mbalimbali), pamoja na Kituo cha Kitaifa cha
Mawasiliano ya Simu (Call Center).
63.
Mheshimiwa
Spika, nilielekeza
kituo cha mawasiliano ya simu (call center) kuwepo kimeongeza wigo wa kuwafikia
wananchi bila kuingia gharama. Kituo hicho kilichopo chini ya ofisi yangu kunawezesha
wananchi kuwasiliana moja kwa moja na Serikali kwa lengo la kutoa taarifa,
kero, malalamiko na maoni kuhusu huduma zinazotolewa na Wizara, Idara na
Taasisi za Serikali.
64.
Mheshimiwa
Spika, huduma
hiyo ni ya bure na inapatikana kupitia chaguo la pili baada ya kupiga namba 180
na mwananchi anaweza kutuma ujumbe mfupi wa maneno, kuongea na kuambatisha
picha mnato, picha mjongeo (video clip) na nyaraka. Kupitia kituo hiki wananchi
wanapatiwa majibu ya moja kwa moja au kuunganishwa kwenye taasisi husika
kulingana na hoja iliyotolewa.
6.0
MAELEKEZO
MAHSUSI
Kuzingatia Utekelezaji wa Vipaumbele
vya Bajeti Mpya
65.
Mheshimiwa
Spika,
Mkutano wa Tatu wa Bunge la 13 ulikuwa mahsusi kwa ajili ya kujadili na
kupitisha Bajeti na Mipango ya Serikali. Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa 2026/2027
ni nyenzo ya kwanza katika kutekeleza Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa
Miaka Mitano 2026/2027- 2030/2031 ambao unatafsiri kwa vitendo Dira 2050.
66.
Mheshimiwa
Spika,
Bajeti iliyopitishwa na Bunge lako inalenga kuimarisha miundombinu, kuongeza
uzalishaji, kuboresha huduma za kijamii, na kuhamasisha uwekezaji wa ndani ili
kufikia uchumi shindani na ustawi wa wananchi. Ili kufanikisha azma hii, tutaendelea
kusimamia yale ambayo Waziri wa Fedha ameyatolea ufafanuzi.
Wito kwa Wadau Kushiriki Katika
Maandalizi ya Mapokezi ya Wanafunzi Wanaotarajiwa Kujiunga Kidato cha Kwanza
Mwaka 2028.
67.
Mheshimiwa
Spika,
Hili ni badiliko la kihistoria baada ya ya lile la Mwalimu nyerere kuongeza
muda wa elimu ya msingi. Serikali inaendelea na maandalizi muhimu ya kupokea
wanafunzi 3,021,177 wa makundirika mawili yanayotarajiwa kujiunga na elimu ya
sekondari ifikapo mwaka 2028. Takriban kata 315 zimebainika kuwa na changamoto
ya msongamano wa wanafunzi kutokana na uchache wa miundombinu.
68.
Mheshimiwa
Spika, shilingi
trilioni 1.7 zinahitajika kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu kabla ya
Januari, 2028. Hivyo, ninatoa wito kwa wadau wote wa elimu kushiriki kikamilifu
katika kufanikisha maandalizi ya mapokezi ya wanafunzi wa makundirika mawili
mwaka 2028. Kila mmoja wetu anayo nafasi ya kuchangia mabadiliko haya ili
kufikia azma ya kupata miundombinu muhimu na kuweza kuhudumia wanafunzi
tarajiwa.
7.0
USALAMA,
AMANI NA UTULIVU
69.
Mheshimiwa Spika, uwepo wa amani umeendelea kuwa
msingi muhimu wa shughuli za kiuchumi, kijamii na kisiasa, hivyo kuifanya nchi
kuendelea kuvutia uwekezaji na kuimarisha ustawi wa wananchi. Watanzania tunao
wajibu wa kutunza hali hii bila kujali tofauti zetu za kisiasa, kidini au
kikabila.
70.
Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa kila mmoja wetu
kuhakikisha kuwa analinda na kuitunza tunu ya amani na utulivu wa nchi yetu. Nawasisitiza
Watanzania wenzangu tuendelee kulinda amani tuliyoirithi kwa wazee wetu kwa
kuzingatia sheria, kuheshimu haki za wengine na kujiepusha na vitendo
vinavyoweza kusababisha migawanyiko. Tuzingatie matumizi ya lugha ya staha
katika mijadala ya kijamii na kisiasa kwani yana mchango mkubwa katika kuvunja
mshikamano wa kitaifa. Amani ikivunjika, hakuna anayejihakikishia usalama, hasa
hasa wale wanaoishi nje ya Tanzania waituongoze kuvunja amani ya nchi yetu.
Tusidanganyane amani, ulinzi na usalama sio suala la kujadiliwa.
71.
Mheshimiwa Spika, Tanzania imeendelea kusisitiza
umuhimu wa wananchi kushiriki katika masuala ya kisiasa kwa njia ya amani na
ustaarabu. Demokrasia inatoa nafasi kwa watu kutoa maoni yao, kuchagua viongozi
na kushiriki katika maendeleo ya Taifa kwa kufuata sheria na taratibu
zilizowekwa.
72.
Mheshimiwa Spika, sina
shaka mtakubaliana
nami kuwa kuendesha siasa za kistaarabu ni msingi wa kuimarisha amani na
demokrasia. Viongozi wa vyama vya siasa, wafuasi wao pamoja na wananchi kwa
ujumla wanapaswa kujenga utamaduni wa kuheshimu tofauti za mawazo, kuepuka
lugha za uchochezi na kuweka mbele maslahi ya Taifa letu.
73.
Mheshimiwa Spika, unapotaja suala la uendelezaji
wa demokrasia nchini Tanzania, huwezi kuliongelea jambo hili bila kugusia
jitihada binafsi za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Wakati wote amekuwa kinara katika kuimarisha demokrasia, haki za
binadamu na utawala bora. Katika kipindi chote cha uongozi wake, tumeshuhudia
utekelezaji falsafa yake ya 4R yaani maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na
mabadiliko ambayo kwa hakika yamekuwa chachu ya kuimarisha siasa za ndani ya
nchi yetu.
74.
Mheshimiwa Spika, kutokana na utashi wake huo, sote
tumeshuhudia nchi yetu ikiendelea kuwa na mshikamano, amani na umoja wa
kitaifa. Hii ni kutokana na msisitizo wake kuhusu utekelezaji wa masuala ya
haki za binadamu, utawala bora na demokrasia. Isitoshe, tumeshuhudia maboresho
mbalimbali ya upande wa mifumo, sheria na uendeshaji wa shughuli za kisiasa.
75.
Mheshimiwa
Spika,
vilevile, tumeshuhudia uwepo wa fursa zaidi za mijadala na maridhiano miongoni
mwa makundi ya wadau wa demokrasia na masuala ya siasa. Ni lazima tukubali kuwa
kupitia kuimarisha maridhiano baada ya uchaguzi, kuendeleza demokrasia na
kuendesha siasa za kistaarabu, Taifa linaweza kuendelea na kustawi kwa faida ya
vizazi vya sasa na vijavyo.
76.
Mheshimiwa Spika, kabla sijamaliza eneo hili, ninaomba kumnukuu aliyekuwa
Rais wa Afrika Kusini, Hayati Nelson Mandela ambaye katika uhai wake alifafanua
vizuri sana suala la maridhiano kwa maneno yafuatayo:
“In the end,
reconciliation is a spiritual process, which requires more than just a legal
framework. It has to happen in the hearts and minds of people.” Mwisho wa kunukuu.
77.
Mheshimiwa Spika, kwa tafsiri isiyo rasmi, Mzee wetu Mandela alimaanisha
kuwa: “... upatanisho ni mchakato wa kiroho, ambao unaenda ndani zaidi ya
mfumo wa kisheria. Unapaswa kudhihirika katika mioyo na akili za watu.”
78.
Mheshimiwa Spika, ninaendelea kuamini kwamba bila kujali tofauti zetu za
kifikra, kiitikadi na imani zetu na hata kama tukifarakana na kutofautiana
kiasi gani, namna pekee ya kuonesha uzalendo na mapenzi mema kwa nchi yetu ni
pale tunapokubali kuwa tayari kukaa kwenye meza ya mapatano na huo ndiyo
uongozi, uzalendo na ukomavu wa kisiasa. Tunapaswa kuijali nchi yetu kwanza kwa
kukaa kwenye meza ya maridhiano na kutanguliza utaifa wetu kwanza.
79.
Mheshimiwa Spika, amani, utulivu na mshikamano wa Taifa hili si vitu vya
kuchezewa kwani vimejengwa kwa jasho, uzalendo, damu na hekima za waasisi wetu.
Kwa namna yoyote ile hatutaruhusu viharibiwe kwa tamaa za kisiasa au maslahi ya
wachache. Tanzania ni nchi yetu sote, na hatutakuwa tayari kuona mtu yeyote,
kikundi chochote au maslahi yoyote yakilitumbukiza Taifa letu katika
mgawanyiko, vurugu au machafuko.
80.
Mheshimiwa Spika, umoja wa Watanzania si
jambo la mjadala; ni msingi wa uwepo wa Taifa letu na ni wajibu wa kila mmoja
kuutunza. Hivyo, tuipende, tuilinde na kuipigania nchi yetu na tusikubali
kugawanyika kwa misingi ya rangi, ukabila, dini au ukanda ili tuendelee kuwa na
amani na kufikia kiwango cha juu cha ustawi na maendeleo.
81.
Mheshimiwa Spika, suala la usalama, amani na utulivu
ni kipaumbele namba moja na hakuna mjadala katika hilo. Niwahakikishie
waheshimiwa wabunge na wananchi kwa ujumla, vitendo vya uvunjifu wa amani,
uchochezi na fujo za aina yoyote havitavumiliwa na mamlaka husika. Hatua
stahiki zitachukuliwa kwa mujibu wa sheria za nchi.
82.
Mheshimiwa Spika, ninawasihi Watanzania wote kuheshimu misingi ya utawala
bora na kuhakikisha shughuli mbalimbali za kijamii, kiutamaduni, kidemokrasia
na kisiasa zinaendelea kufanyika kwa kuzingatia sheria, taratibu, mila, desturi
na Katiba ya nchi yetu. Aidha, Serikali
iko Imara na itaendelea kutimiza kikamilifu wajibu wa kulinda mipaka ya nchi
yetu, usalama wa raia, mali na tunu za Taifa ikiwemo umoja, amani, mshikamano
na muungano.
8.0
MICHEZO
83.
Mheshimiwa
Spika, kutokana na umuhimu wa sekta ya michezo, serikali ya
awamu ya sita imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali na kuchukua hatua
mahsusi za kuinua sekta hii muhimu kwa uchumi wa Taifa letu. Baadhi ya mikakati hiyo ni pamoja na
kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Michezo, kuanzisha Tuzo za Michezo za Baraza la
Michezo la Taifa kwa lugha nyingine “National Sports Council Sports Awards”,
Kuziwezesha Timu za Taifa kushiriki mashindano mbalimbali, kuimarisha
miundombinu ya michezo na kutenga fedha kupitia bajeti.
84.
Mheshimiwa
Spika, Serikali imeendelea kuratibu mashindano ya UMMISETA
na UMITASHUMTA kwa lengo la kuinua vipawa vya watoto na kuendelea kuvilea.
Hatua hiyo inatekelezwa sambamba na kuwekeza kwenye akademia za michezo,
kuwezesha makundi maalum kushiriki katika mashindano mbalimbali pamoja na
kuhamasisha mashindano ya michezo kuanzia ngazi za chini kuratibu na kuwezesha
mashindano ya kimataifa kwa timu chini ya miaka 18.
85.
Mheshimiwa
Spika, licha ya kutoa burudani, sekta ya michezo imekuwa na
mchango mkubwa katika kutoa ajira kwa vijana, kujenga umoja wa kitaifa,
kuitangaza nchi yetu na kuvutia utalii, kuimarisha uchumi endelevu na kuchangia Pato la Taifa. Vilevile, inao
mchango mkubwa katika kuimarisha afya lakini pia, kupunguza gharama za matibabu
kwa maradhi yasiyoambukiza. Kutokana na umuhimu huo sekta ya michezo imeendelea
kuwa moja ya sekta za kipaumbele cha serikali.
86.
Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine, mafanikio ya sekta
ya michezo yametokana na uwepo wa utashi mkubwa wa kuendeleza michezo wa
Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania. Wakati wote
mwelekeo wake ni kwamba michezo si burudani pekee bali ni nyenzo muhimu ya
maendeleo endelevu na diplomasia ya nchi. Mwelekeo huu unaifanya Tanzania kuwa
miongoni mwa mataifa yenye sekta ya michezo imara Barani Afrika.
87.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hatua hizo,
vilabu vyetu vimeendelea kung’ara katika mashindano mbalimbali kikanda na
kimatifa na kuliwezesha Taifa letu kuwa na mvuto wa kipekee katika tasnia ya
michezo. Licha ya vilabu, wanamichezo wetu wameendelea kufanya vizuri katika
mashindano mbalimbali. Nitumie nafasi hii kutoa pongezi nyingi kwa wanamichezo
wetu waliofanya vizuri na kuibuka kidedea katika mashindano hayo.
88.
Mheshimiwa spika, ninatoa pongezi kwa Timu ya Taifa
ya Wanawake chini ya miaka 20 (Tanzanite Queens) kwa kufuzu kihistoria
kushiriki Kombe la Dunia la FIFA la Wanawake litakalofanyika nchini Poland
kuanzia tarehe 5 hadi 27 Septemba, 2026. Vilevile, Timu ya Taifa ya Mpira wa
Miguu wanawake “Twiga Stars” imefuzu Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake
(WAFCON 2026) yatakayofanyika mwezi Julai, 2026 nchini Morocco.
89.
Mheshimiwa Spika, vilevile, ninaipongeza timu ya Taifa
ya Vijana ya Tanzania chini ya umri wa miaka 17 (Serengeti Boys) kwa
kufanikiwa kufuzu Fainali za Kombe la Dunia za FIFA 2026 zitakazofanyika nchini
Qatar kuanzia tarehe 19 Novemba hadi 13 Desemba 2026. Timu hiyo pia ilimaliza
mshindi wa pili katika Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Vijana (AFCON
U-17) zilizomalizika Juni 2026 nchini Morocco. Mafanikio hayo ni kielelezo cha
uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika kuwekeza kwenye ukuzaji wa
vipaji vya michezo kuanzia ngazi za chini.
90.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mchezo wa ngumi,
ninatoa pongezi kwa Bondia Ibrahim Class ambaye amefanikiwa kutwaa mikanda
miwili mikubwa ya WBC. Mikanda hiyo ni WBC International
Silver Belt na WBC International Gold Belt katika uzito wa Super Featherweight.
Mikanda hiyo imeweka historia kubwa kwenye nchi yetu.
91.
Mheshimiwa Spika, sambamba na ushindi katika michezo hiyo, Klabu ya Mpira wa Kikapu ya
Dar City ilifuzu na kushiriki mashindano ya Basketball Africa League
(BAL) kwa mara ya kwanza yaliyofanyika Mwezi Mei 2026 Kigali, Rwanda. Timu hiyo
ilifanikiwa kutinga hatua ya robo fainali ya michuano hiyo.
9.0
SHUKRAN
NA KUTOA HOJA
92.
Mheshimiwa Spika, leo tunapoenda
kuhitimisha Mkutano wa Tatu wa Bunge la 13, nimshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt,
Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Jihn Nchimbi, Makamu wa Rais,
Mheshimiwa Dkt. Huseni Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na mwenyekeiti wa Baraza la
Mapinduzi. Pia nikushurkuru wewe mwenye Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wa
Bunge.
93.
Mheshimiwa Spika, nina kila sababu
ya kuwashukuru wote waliowezesha kufanikisha kwa njia moja au nyingine majukumu
yangu kwa mujibu wa ratiba iliyokuwa imepangwa. Kwa dhati ya moyo wangu ninawashukuru
viongozi na watendaji wote wa Serikali kwa kazi kubwa waliyoifanya.
94.
Mheshimiwa Spika, kipekee
nimshukuru Mheshimiwa Prof. Palamagamba Aidan Mwaluko Kabudi, Mbunge wa Kilosa
na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye
Ulemavu); Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Kwela na Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano); Mheshimiwa Prof. Riziki Silas
Shemdoe, Mbunge wa Lushoto na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI)
pamoja na Naibu Mawaziri wote. Hakika nyote mmekuwa msaada mkubwa kwangu wakati
wote nilipokuwa nikitekeleza majukumu ya serikali.
95.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia, kuwashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri, Naibu Mawaziri wa kisekta kwa kazi
nzuri mliyoifanya ya kujibu maswali yote yaliyoulizwa na kutoa ufafanuzi wa
hoja mahsusi zilizowasilishwa wakati wote wa Mkutano huu wa tatu na mijadala ya
bajeti. Vilevile, ninatoa shukrani kwa Wakuu wote wa Mikoa, kwa
ushirikiano mkubwa mlionionesha wakati wa kutekeleza majukumu yangu.
Ninawapongeza pia, Makatibu Tawala wa Mikoa yote ambao mlikuwa mkifanya kazi
bega kwa bega na Wakuu wa Mikoa kuhakikisha majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu
yanatekelezwa kikamilifu.
96.
Mheshimiwa Spika, ninatoa shukrani
zangu za dhati kwa watendaji wakuu na watumishi wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu.
Nikianza na Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, na Wafanyakazi
wote kwa ushirikiano mkubwa wanaonipatia katika kutekeleza majukumu ya Ofisi ya
Waziri Mkuu.
97.
Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana
Balozi Dkt. Moses Mpogole Kusiluka, Katibu Mkuu Kiongozi, kwa
ushirikiano wake wakati wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali na amekuwa
kiungo muhimu kwenye kutekeleza majukumu ya Serikali. Ninawashukuru pia,
Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu wa Wizara zote pamoja na wakuu wote wa
taasisi Wakurugenzi wa Halmashauri na
Wakuu wa Mashirika, Wakala na Idara Zinazojitegemea kwa ushirikiano mkubwa
walionipatia kwa kipindi chote cha Mkutano huu.
98.
Mheshimiwa Spika, kipekee
ninamshukuru sana Mheshimiwa Hamza Saidi Johari, Mwanasheria Mkuu wa Serikali,
kwa ushauri wake wa kisheria ambao umewezesha miswada yote ya kisheria
kukamilishwa kwa weledi wa hali ya juu.
99.
Mheshimiwa Spika, ninatoa shukrani
za dhati kwa Ndugu Baraka Ildephonce
Leonard, Katibu wa Bunge kwa kuhakikisha kuwa shughuli zote za
ratiba ya Mkutano wa tatu zimekamilishwa kama sote tunavyoshuhudia leo.
Ninawashukuru pia, wafanyakazi wote wa Ofisi ya Bunge kwa kuhudumia vema
Mkutano huu. Sina shaka Waheshimiwa Wabunge mtakubaliana nami kwamba Mkutano
huu umeendeshwa kwa weledi wa hali ya juu.
100.
Mheshimiwa Spika, ninatoa pongezi
kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vikiongozwa na Mwenyekiti wao CDF
Jenerali Jacob John Mkunda na Wakuu wengine wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama. Ni
jambo la faraja na la kujivunia kuona kuwa sote tumekuwa salama katika kipindi
chote cha Mkutano huu. Amani na utulivu tulioupata wakati wa kutekeleza majukumu
ya Bunge ni kwa kuwa wapo wenzetu waliofanya kazi usiku na mchana kuhakikisha
usalama wetu. Kwa
dhati ya moyo wangu ninawashukuru sana.
101.
Mheshimiwa
Spika,
nimpongeze pia Mheshimiwa George Mcheche Masaju, Jaji Mkuu wa Tanzania kwa
kutekeleza msingi ya uwajibikaji katika utoaji haki. Kadhalika, ninawapongeza
watendaji wote wa Mahakama kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kuwahudumia
wananchi na kuhakikisha haki inapatikana kwa wote.
102.
Mheshimiwa
Spika,
nitumie nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa wananchi wa Jimbo la
Iramba Magharibi kwa mambo mengi sana. Kwanza, kwa kuendelea kuniunga mkono
wakati wote ninapotekeleza majukumu yangu. Pili, kwa uvumilivu mkubwa walionao
kwa kipindi chote ninapokuwa katika maeneo mengine nikiwahudumia Watanzania.
Kadhalika, kwa kuendelea kutoa ushirikiano na kuonesha mshikamano na viongozi
wote wanaonisaidia kutekeleza majukumu yangu jimboni.
103.
Mheshimiwa
Spika, kwa
moyo wa upendo ninatoa shukrani kwa familia yangu. Ama kwa hakika wamekuwa
chanzo kikuu cha utulivu wakati ninapotekeleza majukumu yangu. Ninamshukuru mke
wangu mpendwa Bi. Neema Mwigulu Nchemba pamoja na watoto wetu Joshua, Gracious,
Isaac na Bernice kwa upendo wanaoendelea kuuonesha kwangu. Ahsanteni sana nami
ninawapenda sana.
104.
Mheshimiwa
Spika, ninatoa
shukrani kwa viongozi wote wa madhehebu ya dini. Sina shaka Waheshimiwa Wabunge
wote mtakubaliana nami kuwa tumefika hatma ya Mkutano huu muhimu kwa ustawi wa Taifa
letu kwa kuwa wapo waliokuwa wanaomba kwa ajili yetu. Ahsanteni sana nami
ninawasihi sana endeleeni kutuombea.
105.
Mheshimiwa
Spika, ninatoa
shukrani kwa wananchi wote wa Tanzania kwa ushirikiano wanaoendelea kuuonesha
kwa serikali ya awamu ya sita. Pia, ninawashukuru sana kwa kuendelea kushiriki
kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali kwa maendeleo ya Taifa letu.
106.
Mheshimiwa
Spika,
ninatoa shukrani kwa vyombo vya Habari, mitandao ya kijamii pamoja na
wanahabari wote waliokuwa mstari wa mbele kuhakikisha umma wote unapata taarifa
sahihi ya masuala muhimu yaliyojiri hapa bungeni. Kundi hili limefanya kazi
kubwa na nzuri kwa kuwa licha ya kutangaza limefanya uchambuzi na kuwezesha
umma kuelewa kwa mapana zaidi kuhusu bajeti inayohusu maisha yao ya kila siku.
107.
Mheshimiwa Spika, nikamilishe salamu
zangu za shukrani kwa watumishi wote wa sekta ya umma na sekta binafsi kwa
hakika mmefanya kazi kubwa na nzuri katika kuhakikisha Mkutano huu
unahitimishwa kwa mafanikio makubwa. Ninawasihi sana endeleeni kufanya kazi kwa
bidii, weledi na uadilifu, ninyi ni nguzo muhimu ya utekelezaji wa mipango na
mikakati ya serikali, Ahsanteni sana.
108.
Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo
wa fadhila kama sitatambua kazi kubwa iliyofanywa na madereva kwa kipindi chote
cha mkutano huu. Ahsanteni sana kwa kufanya kazi kwa weledi na nidhamu ya hali
ya juu.
109.
Mheshimiwa Spika, baada ya
kusema hayo, ninaomba sasa Bunge lako tukufu liahirishwe hadi tutakapokutana
tena tarehe 25 Agosti, 2026 saa tatu kamili asubuhi hapa katika Ukumbi
wa Bunge Jijini Dodoma.
110. Mheshimiwa Spika, ninaomba
kutoa hoja.
Mbunge wa Bagamoyo Subnira Mgalu akiuliza mwongozo kuhusu mafuta
Waziri Ndejembi akijibu mwongozo wa Mgalu akisema mafuta yatashuka bei hivi karibuni
Waziri Katambi akipiga mafruku mikutano ya vyama vya kisiasa ikiwemo CCM
Makofi ya Waziri Katambi wakati akizungumza
Comments
Post a Comment