TANZANIA, ALGERIA KUKUZA USHIRIKIANO KATIKA SEKTA YA VIWANDA VYA DAWA
Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mobhare Matinyi (kushoto pichani), leo amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Viwanda vya Dawa wa Algeria, Dkt. Wassim Kouidri, katika ofisi za wizara hiyo jijini Algiers. Mazungumzo hayo yalihusu namna ya kuimarisha ushirikiano zaidi katika sekta ya viwanda vya dawa ambayo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeazimia kuiendeleza ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani Tanzania na la ukanda wa Afrika. Balozi Matinyi alimweleza Waziri Kouidri kwamba Serikali ya Tanzania hivi sasa imeweka vivutio maalum kwa ajili ya uwekezaji katika sekta ya viwanda vya dawa nchini na tayari kuna viwanda vitano vinavyoendelea kujengwa na vingine zaidi vinatarajiwa. “Serikali imedhamiria kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha viwanda vya dawa na vifaa vya tiba katika ukanda wa nchi za mashariki, kati na kusini mwa Afrika wenye watu takriban milioni 350,” alisema Balozi Matinyi. Naye Waziri Kouidri aliahidi ushirikiano kwa Tanzania kutoka Serikali ya Jamhuri ya Ki...