MAPAMBANO YA DAWA ZA KULEVYA BANGI YAONGOZA KUKAMATWA NCHINI======PROFESA KABUDI
Rais huyu ameimalisha utekelezaji wa mikakati ya Kitaifa kupambana na dawa za kulevya pale alipoiwezesha tume hiyo kuendesha oporesheni zake za mara kwa mara kudhibidi ukamataji na uteketezaji wa mara kwa mara unapojitokeza. Mwaka 2025 jumla ya tani 1,074.74 za dawa za kulevya zilikamatwa katika oporesheni zilizofanyika katika maeneo mbalimbnali nchini. Hebu soma taarifa hiyo ya waziri ujionee mwenyewe,TAARIFA YA WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA,
BUNGE, URATIBU NA WENYE ULEMAVU) MHE. PROF.
PALAMAGAMBA J.A KABUDI (MB), KWA VYOMBO VYA HABARI
KUHUSU HALI YA DAWA ZA KULEVYA KWA MWAKA 2025.
TAREHE: 29 MEI, 2026
MAHALI: DODOMA
Ndugu waandishi wa habari,
Leo nimewasilisha bungeni Taarifa ya Hali ya Dawa za Kulevya nchini ya
Mwaka 2025. Uwasilishaji wa taarifa hii ni utekelezaji wa Kifungu cha 66 cha
Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015,
inayoiagiza Serikali kuandaa na kuwasilisha bungeni taarifa hiyo kila mwaka.
Lengo ni kuonesha uwajibikaji wa Serikali kwa wananchi kupitia Bunge,
pamoja na kutoa tathmini ya utekelezaji wa mikakati ya udhibiti wa dawa
hizo kwa mwaka husika. Pia, taarifa hii inatoa nafasi kwa Bunge kutoa
ushauri kwa Serikali kuhusu namna bora ya kukabiliana na tatizo la dawa za
kulevya nchini.
Ndugu waandishi wa habari,
Taarifa niliyoiwasilisha leo inaonesha namna Serikali ya Awamu ya Sita, chini
ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ilivyowekeza na kuweka
nguvu kubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya. Kupitia Mamlaka
ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, vyombo vya ulinzi na
usalama, wadau wa ndani na nje ya nchi pamoja na jamii kwa ujumla,
serikali imepata mafanikio makubwa katika kudhibiti biashara na matumizi
ya dawa za kulevya.
1
Ndugu waandishi wa habari,
Mwaka 2025, bangi iliendelea kuwa dawa ya kulevya iliyokamatwa kwa
kiwango kikubwa zaidi ambapo jumla ya tani 1,017.26, zilikamatwa. Hata
hivyo, kiasi kilichokamatwa kilipungua kwa asilimia 55.97 ikilinganishwa na
mwaka 2024. Hii ni kutokana na uteketezaji wa mashamba makubwa ya
bangi uliofanyika mwaka 2024 na kuimarika kwa udhibiti ikiwemo utoaji elimu
kwa jamii inayojihusisha na kilimo cha bangi kuhusu madhara ya kilimo cha
zao hilo.
Jumla ya tani 26.36 za mirungi zilikamatwa. Kiasi hiki kiliongezeka kwa
asilimia 42.88 ikilinganishwa na mwaka 2024. Ongezeko hili linaashiria
kuimarika kwa operesheni za ufuatiliaji na udhibiti hususan katika maeneo ya
mipaka na njia zinazotumika kusafirisha dawa hizo
Kwa upande wa dawa za kulevya za viwandani, Serikali ilifanikiwa kukamata
methamphetamine kilogramu 907.18, heroin kilogramu 672.23, cocaine
kilogramu 4.89, MDMA gramu 178 na MDA gramu 7.82.
Aidha, kwa mara ya kwanza, mwaka 2025 Serikali ilikamata tani 29.52 za
aina mpya ya dawa za kulevya aina ya Kratom itokanayo na mmea unaoitwa
Mitrogyna speciosa. Dawa hii iliingizwa nchini kama mbolea, baada ya
uchunguzi ilibainika kuwa ni dawa za kulevya.
Mafanikio haya yametokana na kazi kubwa iliyofanywa na Mamlaka ya
Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kwa kushirikiana na vyombo
vyetu vya ulinzi na usalama katika kudhibiti mitandao na njia za usafirishaji
wa dawa za kulevya kupitia Nchi kavu, anga na majini.
2
Aidha, Serikali iliendelea kuimarisha ukaguzi katika vituo vya forodha,
vyombo vya usafiri, kampuni za usafirishaji vifurushi na kwenye kampuni
zinazojihusisha na biashara ya kemikali bashirifu na dawa tiba zenye asili ya
kulevya kwa lengo la kudhibiti uchepushwaji. Kupitia ukaguzi huo, jumla ya
tani 31.76 na lita 183.500 za kemikali bashirifu pamoja na kilogramu 2.36 na
mililita 160 za dawa tiba zenye asili ya kulevya zilikamatwa.
Kwa upande wa makosa ya dawa za kulevya, mwaka 2025, jumla ya mashauri
1,124 yalifunguliwa katika Mahakama mbalimbali nchini. Pamojana
mashauri yaliyokuwa yakiendelea katika Mahakama mbalimbali nchini,
mashauri 1,373 yalitolewa hukumu na Jamhuri ilishinda mashauri 1,058.
Kadhalika, mali zenye thamani ya zaidi ya Tsh. bilioni 3.3 zilizohusishwa na
makosa ya dawa za kulevya zilitaifishwa.
Ndugu waandishi wa habari,
Sambamba na hatua za udhibiti, Serikali iliendelea kutoa huduma za tiba na
utengamao kwa watu wenye uraibu wa dawa za kulevya. Mwaka 2025, jumla
ya watu 85,425 wenye uraibu wa dawa za kulevya walipata tiba kwenye
vitengo vya afya ya akili katika hospitali za rufaa za mikoa na Kanda, kliniki
za MAT na nyumba za upataji nafuu nchini.
Elimu kuhusu madhara ya dawa za kulevya iliendelea kutolewa kwa Umma
kupitia kampeni mbalimbali za uelimishaji katika jamii, taasisi za elimu na
vyombo vya habari ili kuijengea jamii uelewa, maamuzi sahihi na uwezo wa
kujilinda dhidi ya matumizi na biashara ya dawa za kulevya.
3
Katika kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa, Serikali
imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi katika
kubadilishana taarifa za kiintelijensia, kujenga uwezo wa kitaasisi pamoja na
kuendesha operesheni za pamoja dhidi ya mitandao ya usafirishaji na
biashara ya dawa za kulevya.
Ndugu waandishi wa habari,
Matokeo chanya katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya yanatokana na
dhamira thabiti, maono na uongozi mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwani chini ya uongozi wake
amewekeza kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha mapambano dhidi ya tatizo
la dawa za kulevya Nchini.
Naipongeza Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya,
vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama, wataalamu wa afya, wadau katika
mapambano na wananchi kwa ushirikiano wao uliosaidia kuyafikia mafanikio
niliyoyaeleza.
Ushirikiano ni silaha muhimu katika vita dhidi ya dawa za kulevya kwani
mafanikio ya kweli yanahitaji juhudi jumuishi kati ya Serikali, taasisi binafsi,
wadau wa kimataifa na jamii kwa ujumla.
Pamoja na hayo, naomba wananchi waendelea kutoa taarifa pale wanapohisi
au kushuhudia viashiria vya biashara au matumizi ya dawa za kulevya kwa
vyombo husika ili kuifanya nchi yetu kuwa mahali salama na huru dhidi ya
matumizi na biashara dawa za kulevya.
Wakiwaonyesha wanahabari lipoti iliyowasilishwa bungeni leo
Comments
Post a Comment