KIKWETE AMKABIDHI KIJITI MAGUFULI


Mwenyekiti wa CCM Mstaafu na Rais Mstaafu Jakaya Kikwete(kushoto) akimkabidhi  Mwenyekiti mpya  Rais Dk. John Magufuli,ripoti ya chama ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka jana baada ya kumtangaza kwenye mkutano Mkuu Maalum wa chama hicho mjini Dodoma
 Wakikumbatiana kwa mara ya mwisho kama mwenyekiti

 Mwenyekiti mstaafu wa CCM,Jakaya Kikwetena Mwenyekiti mpya Rais Dk. John Magufuli (kulia), wakiwapungia wanachama wa chama hicho baada ya kumtangaza kwenye Mkutano Mkuu Maalum Dodoma

Wakikumbatiana na rais wa zanzibar



Magufuli ni wa kuogopwa
*Asema walioimba wana imani na Lowassa kwake yeye wangepotea ndani ya nusu saa
*Asema hana uvumilivu, atangaza kuifumua CCM, awawashia taa nyekundu wasaliti
*Sasa kuihamishia Serikali yake Dodoma ndani ya miaka minne


UNAWEZA kumwelezea Rais John Magufuli kama rais anayetisha, anayepaswa kuogopwa au pengine kuhofiwa kutokana na kauli anazozitoa hadharani kila anapopata fursa ya kuhutubia.
Hali hiyo ilithibitika jana mjini Dodoma saa chache baada ya kutangazwa mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Mkutano Mkuu Maalumu ulioitishwa ili kumkabidhi nafasi hiyo.
Akihutubia Rais Magufuli kwa mara nyingine alitoa kauli nzito na tata ambazo zilikuwa zinapeleka ujumbe si kwa wana CCM tu waliokuwa wakimsikiliza ukumbini humo bali pia kwa watu waliokuwa wakifuatilia Mkutano Mkuu Maalumu huo kupitia vyombo vya habari.
Miongoni mwa kauli hizo ni pamoja na ile aliyoitaja mwanzoni kabisa katika hotuba yake hiyo akieleza kushangazwa na kile alichokiita uvumilivu usiomithilika wa mtangulizi wake Rais mstaafu Jakaya Kikwete.
Akitoa mfano Magufuli alilitaja tukio la  baadhi ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM ambao mwaka jana wakati wa mchakato wa kumtafuta mgombea urais kwa tiketi ya chama hicho kwa njia ya wimbo walitangaza kuwa na imani na aliyepata kuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa.
Kwa maneno yake mwenyewe, Magufuli alisema: “Na mimi kwa kweli najiona nina changamoto kubwa kwasababu moyo wako huo wa uvumilivu sina, hakika mimi sijui kama ninaweza nikavumilia hivyo.
“Na mimi nasema kwa dhati kabisa Mwenyekiti mstaafu, siku ile ulipoingia kwenye mkutano ukakuta watu wanaimba wana imani na mtu fulani, siku hiyo hiyo hata robo au nusu wangepotea. Kwasababu ninajaribu kuuliza moyo wangu na kwa kumtanguliza Mungu kwamba kingetokea hicho kilichotokea kwako, sifahamu,” alisema Rais Magufuli.
Katika hilo, Rais Magufuli aliwaomba wajumbe wa mkutano huo kumuombea ili angalau awe na nusu ya uvumilivu wa Kikwete.
KUIFUMUA CCM
Katika hatua nyingine Rais Magufuli ametangaza kufanya mapinduzi makubwa ya kimfumo ndani ya CCM ikiwa ni pamoja na kukomesha uongozi unaopatikana kwa njia ya rushwa.
Magufuli ambaye amekuwa akijinasibu kupambana na rushwa na ufisadi, alikitaja waziwazi chama hicho kama moja ya taasisi zinazotajwa kuongoza kwa rushwa licha ya kukatazwa katika ahadi ya tatu ya CCM pamoja na kifungu cha 18 cha Katiba ya CCM.
 “Niligombea urais niliyaona huko Iringa wakati wa kutafuta wadhamini, wilaya yote ilikuwa imenunuliwa ilibidi nisafiri kwenda ndani huko vijijini. Fedha imekuwa kigezo cha mtu kupata uongozi…ukitaka urais kiasi fulani, ubunge kiasi fulani, diwani kiasi fulani. Tumekuwa tukipoteza sehemu nyingine kuchagua wenye fedha badala ya anayekubalika,” alisema Magufuli. 
Alisema amedhamiria kukomesha jambo hilo na kwamba mtu atakayetoa rushwa hatachaguliwa wala kupitishwa kwa mujibu wa kanuni ambazo alikabidhiwa jana na Mwenyekiti mstaafu.
Akilisisitiza hilo Rais Magufuli alimwambia Kikwete: “Ulionesha mfano rafiki yako kabisa alipoonesha ufisadi na rushwa ulimchinjia mbali na kama ingekuwa kwa rushwa nisingekuwa rais, sasa ole wao nitakapokuwa Mwenyekiti. Ukijipanga kuchukua uongozi kwa pesa utatumikia pesa zilizokuweka madarakani,” alisema Mwenyekiti huo.
Mwenyekiti huyo aliwataka wana-CCM kuonesha mfano katika uchaguzi wa ndani utakaofanyika mwakani kwa kutotoa takrima.
Kuhusu wasaliti Magufuli alisema ni heri kuishi na mchawi lakini si msaliti huku akisisitiza katika uongozi wake hawana nafasi na kama wapo watubu kuanzia jana vinginevyo wawapishe.
 “Hatuhitaji CCM pandikizi, CCM masilahi, nahitaji CCM ambao siku zote usiku, mchana, mvua ikinyesha, njaa wapo…sihitaji ndumilakuwili, masalia ambao wako kwa ajili ya mtu, nahitaji watu watakaotulia…nataka kuona CCM ya watu wote wakiwemo wanyonge, nataka kuona CCM inayojitegemea si inayotegemea wafadhili,” alisisitiza.
Awali Rais Magufuli mara baada ya kuchaguliwa alikabidhiwa vitabu vinne na Mwenyekiti mstaafu Kikwete ambavyo alisema vimebeba uchunguzi walioufanya baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka jana.
Alisema vitabu hivyo vimeeleza walivyofanikiwa na pale waliposhindwa na waliowaangusha.
Pamoja na hilo, Rais Magufuli aliahidi kukifumua na kukiunda upya chama hicho kwa kuondoa vyeo visivyokuwa na tija hasa katika zama hizi za ushindani wa kisiasa.
Magufuli alilitaja kundi ambalo litaathirika kuwa ni pamoja na chipukizi ambao alisema hawana sababu ya kujihusisha na masuala ya chama kutokana na umri wao wa miaka 8-15 unaowaruhusu zaidi kuwa shuleni.  
“Chipukizi kuitumikia CCM badala ya kusoma, kama akiwepo chipukizi wa CCM akianzishwa wa Ukawa, UDP, TLP, NCCR na umri wake ni miaka 8-15 hawa watoto watasoma? Najaribu kutoa changamoto,” alisema Magufuli.
Kundi lingine ambalo alisema litaondoka ni Makamanda wa vijana ambao alidai wanapatiwa uongozi ni wale wenye pesa.
Vyeo vingine ambavyo alisema vitaondolewa ni pamoja na walezi wa Umoja wa Wanawake (UWT), washauri ndani ya Jumuiya ya Wazazi akidai kuwa vyeo hivyo vinachochea migogoro badala ya kuitatua.
Alisema kumekuwa na mrundikano wa vyeo ndani na nje ya CCM ambapo unakuta Waziri lakini bado ni Kamanda wa vijana.
“UWT, Umoja wa Vijana na Jumuiya ya Wazazi tutaziimarisha sasa, masilahi ya wafanyakazi ndani ya CCM nitayaangalia. Sitapenda wawe ombaomba na wanapokwenda kuomba ndio hao wenye safari za matumaini huingia huko,” alisema Mwenyekiti huyo.
Akizungumzia mali za CCM, Magufuli alisema kitaundwa kikosi kuzihakiki huku akimpa jukumu hilo Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana ambaye alimtangaza kuendelea naye hadi hapo atakapoamua vinginevyo.
Alisisitiza kuwa chini ya Kinana, makatibu wote wa ngazi za chini waorodheshe mali za chama hicho.
Pamoja na hilo, Rais Magufuli aliibua hoja ya wanachama wa CCM kulipa ada akiwataka kufanya hivyo tena kwa njia ya kielektroniki pamoja na kuondoa wafanyakazi hewa na kuongeza idadi ya wanachama hasa kundi la vijana kwa zaidi ya iliyopo sasa ambayo ni milioni 8.7.
Serikali kuhamia Dodoma
Magufuli pia alitumia mkutano huo kueleza azma yake ya kuihamishia Serikali Dodoma.
Mwenyekiti huyo mpya ambaye alipata asilimia 100 ya kura za ndio katika kura zaidi ya 2,000 zilizopigwa na wajumbe hao, aliahidi kuwa atahakikisha anahamishia Serikali yake Dodoma ndani ya miaka minne iliyobaki.
Akisisitiza suala hilo lililowashinda marais wote wanne waliopita alisema yeye mwenyewe atakuwa wa kwanza kuhamia Dodoma na kwamba Makamu wake wa Rais na Waziri Mkuu hawatakuwa na jinsi nao itabidi wamfuate.
“Wale wateule wangu na mimi mwenyewe tujipange kuhamia Dodoma, tusitafute kisingizio, kama wajumbe wote wa CCM wanalala Dodoma wanakula na kunywa, Bunge liko Dodoma sioni sababu kukaa Dar, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote watakuja huku,” alisema Rais Magufuli.
Alisema pia sherehe za Mapinduzi mwakani zitafanyika mjini Dodoma na kwamba Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere hakukosea kuamua Makao Makuu ya nchi kuwa huko.
Rais Magufuli alitumia mkutano huo kuwaeleza wajumbe hao mambo ambayo Serikali yake imeyafanya ikiwemo kutoa elimu bure, kuagiza ndege mbili zitakazowasili Septemba, kujenga Reli ya Kati kutoka Dar es Salaam hadi Kigoma na Rwanda na kwamba tayari fedha kiasi cha Sh trilioni 1 zimetengwa.
Pia alisema tayari mpango wa maendeleo wa taifa umepitishwa na umeanza kufanya kazi mwaka huu wa fedha kwa kutumia kiasi cha Sh trilioni 29.5 huku asilimia 40 ikienda kwenye maendeleo.
MWISHO

Comments

Popular posts from this blog

AJIRA MPYA 41,500 SERIKALINI ZATANGAZWA KATIBU MKUU UTUMISHI JUMA MKOMI

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

WALIOPITA KURA ZA MAONI CCM HAWA HAPA