WABUNGE NA MUSWAADA WA KADHI


Baadhi ya wabunge wakiwa wamesimama kupinga hoja za kutaka kuwasilishwa Muswada wa Mahakama ya Kadhi bungeni wakati wa semina ya wabunge iliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma 


Waziri Mkuu Mizengo Pinda(katikati),Waziri wa Sheria na Katiba,Dk. Asha-Rose Migiro(kushoto) na  Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Sheria na Katiba, William Ngeleja wakisiliza hoja za wabunge kupinga kuwasilishwa Muswada wa Mahakama ya Kadhi bungeni katika semina ya wabunge iliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma 


Spika wa Bunge ,Anna Makinda, akijaribu kuwatuliza wabunge kuhusu Muswada wa Mahakama ya Kadhi 
 Mbunge wa Semve, Richard Ndassa, akipinga kuwasilishwa Muswada wa Mahakama ya Kadhi bungeni
 Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini, akipinga kuwasilishwa Muswada wa Mahakama ya Kadhi bungeni katika semina ya wabunge iliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma

Jaji wa Mahakama Kuu, Robert Makalamba, akizungumza katika Semina ya wabunge kuhusu Mahakama ya Kadhi iliyoandaliwa na Ofisi y Waziri Mkuu bungeni mjini Dodoma 


WABUNGE jana nusura wazihape kavukavu baada ya kutofautiana juu ya uanzishwaji wa mahakama ya kadhi nchini.
Hali hiyo ilijitokeza wakati wabunge hao wakiwa kwenye semina Muswada ya Sheria ya Mabadiliko ya Sheria Mbalimbali, ambapo miongoni mwa sheria zilizo ndani yake ni ile ya Mahakama ya Kadhi.
Sakati hilo lilitokea katika Semina kuhusu muswada huo unaotarajiwa kuwasilishwa bungeni keshokutwa iliyofanyika katika Ukumbi wa Msekwa.
Katika semina hiyo, iliyofanyika kwenye ukumbi wa msekwa, licha ya badhi ya baadhi ya wabunge kutaka kunyanyuka kwenye viti vyao na kwenda kupigana, wapo waliokuwa wakirushiana matusi ya nguoni.
Awali semina hiyo ilionekana kwenda shwari ambapo wabunge wote waliokuwa wakisimama bila kujali dini zao ama vyama, walikuwa wakiupinga mswada huo kwa sababu tofautitofaut.
Katika Semina hiyo ambayo wabunge waliopata nafasi ya kuchangia walikuwa takribani 38, waliokubali mswada huo uwasilishwe bungeni ni takribani watano.
Hali ilibadilika baada ya Mbunge wa Kisarawe, Seleman Jafo (CCM), aliposimama na kuchangia ambapo aliunga mkono mswada huo.
Alipokuwa akichangia, baadhi ya wabunge walikuwa wakimshangilia, hali iliyomfanya kususa na kukaa chini huku akiwataka wabunge waisilamu wakutane baada ya semina hiyo.
Hali hiyo ilizua zaidi vurugu ambapo baadhi ya wabunge wa CCM na upinzani walisimama wakipinga kauli hiyo na wengine kutoka nje ya ukumbi huo.
Wabunge waliosimama na kuanza kumpinga Jafo ni pamoja na Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR-Mageuzi), Mbunge wa Viti Maalum, Pauline Gekul (Chadema), Mbunge wa Viti Maalum, Esther Bulaya (CCM) na Mbunge wa Nyamagana, Hezekiah Wenje (Chadema).
Wakati hali hiyo ikiendelea, Mbunge wa Chakwa, Yahaya Kassim Issa (CCM) na  Khatibu Saidi Haji, (CUF) walisimama kwenye viti vyao na kutaka kwenda kumshambulia machali, kabla ya kuzuiwa na wenzao waliokuwa wamekaa nao karibu.
Hali hiyo ya vurugu na makelele iliendelea kwa takribani dakika 10 huku baadhi ya wabunge wakitaka semina ivunjikee.
Wakati vurugu hizo zikimshinda aliyekuwa mwenyekiti wa semina hiyo, William Ngeleja, Waziri Mkuu Mizengo Pinda ambaye alikuwa mgeni rasmi katika semina hiyo,  walimuwa wameketi kwenye viti vyao huku Sipka Amma Makinda akiwa amesimama kuwatuliza wabunge hao.
Baada ya muda alifanikiwa kutuliza vurugu hizo huku akiwataka kujenga utaratibu wa kuheshimiana  na kuwa wanyenyekevu.

Awali katika mchango wake, Jafo aliwashangaa wakristo kujifanya wazungumzaji wakubwa kuhusu suala hilo la Mahakama ya Kadhi wakati jambo hilo haliwahusu.
“Nataka niwaambie Serikali msije mkafanya masihara Muswada huu usiingie bungeni, muswada uje tutafanya ‘amendment’ (marekebisho) huko, na naitahadhalisha Serikali iwe makini katika hili,” alisema Jafo.
 Mbunge wa Sumve, Richard Ndasa (CCM), alisema katika katiba Ibara ya 19 ilishaweka wazi kuhusu suala la uhuru wa kuabudu kwamba jumuiya zote za kidini zitakuwa nje ya mamlaka za nchi.
Mwenyekiti wa kikao hicho (Ngeleja) alimtaka Ndasa avute subira kusikia maudhui ya semina hiyo huku akisisitiza kwamba hakuna kipengele chochote cha Katiba kilichovunjwa.
Mbunge wa Ngara, Deogratius Ntukamazina (CCM), alisema yeye kama mjumbe wa Kamati ya Bunge Katiba na Sheria walikutana na makundi 11 ya mashehe lakini yaliukataa muswada huo.
“Waislamu hawa walisema wao hawaitambui Bakwata (Baraza Kuu la Waislamu Tanzania), naiomba Serikali kwa jambo hili kubwa la Mahakama ya Kadhi hamuwezi  kulileta kwa marekebisho madogo kama haya.
“Kama mkitaka leteni muswada maalumu wa kuanzisha Mahakama ya Kadhi baada ya waislamu wenyewe kukubaliana, mimi natambua uhumimu wa mahakama hii ambazo hata sisi tunazo ila hatutaki Serikali izitambue,” alisema.
Mbunge wa Viti Maalum, Rukia Kassim Isssa (CUF) alipinga kitendo cha mahakama hiyo  kuanzishwa chini ya Bakwata akidai kwamba Bakwata ni taasisi ya mtu binafsi iliyosajiliwa na Rita kama zilizovyo taasisi nyingine.
“Suala hili halikubaliki, kwa nini Mahakama ya Kadhi iundwe chini ya Mufti, au Waziri Mkuu anataka tu kuundwa kwa mahaama ya Kadhi kwa kuwa alishaahidi, msitakake kuipasua hii nchi.
“Kama Waziri Mkuu yeye aliahidi kwa ajili ya kuutafuta urais shauri yake ila ni marufuku kuwalazimisha watu kuwa chini ya Bakwata, kufanya hivyo ni kukiuka Katiba.
“Huyu Mufti anapatikana kwa mujibu wa Katiba ya Bakwata, na Bakwata ni taasisi tu, Waziri Mkuu anajua suluhisho la jambo hili.
“Tume ya watu 25 iliundwa kulishughulikia, baadae ikawaundwa ya watu watano kupanga muundo wa Mahakama ya Kadhi, lakini leo hii anawapa Bakwata, Waziri Mkuu ndio chanzo cha yote haya, suala hili halikubaliki na tutalipinga,” alisema.
Mbunge wa Kasulu Mjini,Moses Machali (NCCR-Mageuzi) alisema wabunge hao wanakosea kulijadili suala hilo na kwamba tayari limeleta mgawanyiko baina ya waislamu wenyewe.
“Inawezekana Waziri Mkuu aliahidi jambo hili kwa malengo ya urais, na kama muswada utaingizwa ndani ya Bunge, na sisi wakatoliki tutaleta mabadiko yetu ya Canon Laws, huko Mbeya na wenyewe madhehebu yao yote wataleta mabadiliko yao,” alisema.
Mbunge wa Sumve, Richard Ndasa (CCM), aliitaka Serikali kusoma alama za nyakati wasiuleta muswada huo bungeni
“Kama Serikali imeamua kuanzisha  taasisi ya kidini itambue kuwa inakiuka misingi waliyotuachia wassisi wa taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere na Abei Aman Abeid Karume, hawa waliposema Serikali haina dini hawakuwa na akili.
“Hili jambo ni jema lakini nashauri muswada huu urudishwe ili ukaboreshwe ili uje kwa mapana kuliko kuja hapa kufanya marekebisho,” alisema.
Mbunge wa Tarime, Nyambari Nywangwine (CCM) pamoja na kusema kwamba jambo hilo ni zito alisema  taasisi za dini ziliukataa katika Kamati ya Bunge na kwamba Bakwata walitoa masharti kwamba Serikali igharamie.
“Wakristo wakataka waislamu wenyewe wakakae kwanza wakubaliane , mimi sina dini ni mpagani nikitaka kuleta sheria zangu mtazikubali,” alisema.
Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema) alisema Serikali isipokuwa makini Bunge linaweza kuingia katika historia ya kuivuruga nchi.
“Mimi hapa sitaki kuwa sehemu ya historia hiyo, jambo hili limeligawa Taifa, hakuna ambaye hawasikii maaskofu wanasema nini na kama hamuwasikii kwani usalama wa Tiafa hawaambii?
“Tusifungue jini kwenye chupa lililofungiwa na waasisi wetu halafu baadae likaja kutusumbua,semina hii mnayotupatia mlipaswa kuwapa maaskofu ambao wana hofu juu ya kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi.
“Kwanza Serikali inatenda dhambi kuwatumia waislamu kutafuta kura, acheni hili jambo nchi hii itakuwa vipandevipande,” alisema.
Mbunge wa Viti Maalum, Marry Mwanjelwa (CCM) alisema Nyerere na Karume hawakuwa wajinga waliposema nchi haina dini na kutahadharisha kuwa Serikali isopokuwa makini inaweza kuliingiza taifa kwenye machafuko ambayo hayajawahi kutokea na kwamba yeye hata kubali hilo litokee.
Mbunge wa Viti Maalum, Christowaja Mtinda (Chadema) alisema suala la kuitambua Mahakama ya Kadhi kutaingiza nchi katika machafuko.
“Hao maaskofu na wachungaji mnaokutana nao sio hao, sasa hivi tunakwenda kwenye uchaguzi msitake kuwagombanisha wabunge na wapiga kura wao,” alisema.
Mbunge wa Gando, Khalifa Seuleiman Khalifa (CUF) alisema Serikali haikujipanga kuleta muswada huo bungeni na kwamba inatafuta wingi wa waislamu.
“Kama kweli wana nia na wanawapenda waislamu walete muswada kalimi na sio kufanya haya marekebisho, huu mnaoufanya ni unafiki ambao Mungu hapendi.
 “Serikali iende ikajiande upya  na kama suala ni hofu ya gharama za kuendesha mahakama hizo waislamu watalipia au hata wafadhili kwani nyie mangapi mnafadhiliwa, hapa sasa hivi tutawanyike tukafanye mengine,” alisema.
Mbunge wa Mbozi Magharibi, Davi Silinde (Chadema) alimshukia Waziri Mkuu kwa kulileta jambo hilo kubwa kuahidi kulileta bungeni.
“Huwezi ukamlazimisha mtu aamini kinyume na imani yake, wakristo tumekaa hapa tunajadili waislamu ‘non of our business’ tuwaache wajadili mambo yao hii ni ‘non sense’ na ndio maana suala la imani limevuka mipaka ya vyama.
“Mnataka kutuvurugia nchi hii kwa kutafuta kura, tumeishi pamoja kwa miaka 50 sasa, mnataka kutupelekea wapi, juzi Rais Kikwete alisema Serikali haitaanzisha Mahakama ya Kadhi  bali itaanzishwa na waislamu wenyewe,” alisema.
Mbunge wa Mwanakwerekwe Haji Juma Sereweji (CCM), alitaka muswada huo uwasilishwe bungeni na  kwamba wabunge watapewa nafasi ya kupendekeza marekebisho yao.
“Sioni sababu ya kwanini muswada usipelekwe bungeni, yule ambaye anaona haufai siku hiyo wasije bungeni au watoke nje.
“Karuume alikubali Mahakama ya Kadhi ndio maana Zanzibar ipo, Nyerere alishauri kuanzishwa kwa Bakwata ili waislamu wawe na sehemu yao ya kusemea, sheria hii iletwe ili waislamu wasimamie mambo yao,” alisema.
Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu (CCM) alitaka muswada uwasilishwe bungeni na kwamba wabunge watapata fursa ya kufanya marekebisho.
“Mimi binafsi sikubaliani na Mufti kuchagua makadhi kwa sababu cheo cha kadhi ni kikubwa kuliko cha Mufti, tusisukumwe na makundi ya kisiasa na imani zisizokubalika na Mungu. 
Mangungu aliwataka wabunge wasiwasemee wananchi kwa kuwa wao kama hawautaki muswada huo haina maana kwamba Watanzania wote hawautaki.
Hata hivyo mbunge huyo alirushiana vijembe na Mbunge wa Viti Maalum,Esther Bulaya baada kumzonga  pale alipowaita wabunge kwamba ni wanafiki kutokana na michango yao waliyokuwa wanaitoa.
Mbunge wa Chwaka, Yahya Kassim Issa (CUF) alisema ni wakati muafaka muswada huo uwasilishwe bungeni na kwamba wanachotaka waislamu ni kutambulika kwa hukumu zinazotolewa na Mahakama ya Kadhi.
“Sasa hawa wenzetu pilipili wasoila inawawashia nini, milishaambiwa mahakama hii haitajihusisha na masuala ya jinai isipokuwa masuala ya ndoa, mirathi, talaka na wakfu,’ alisema.
Mbunge wa Igunga, Dk Dalay Kafumu (CCM) aliitaka Serikali  kutoa elimu kwa viongozi wa dini wakiwemo maaskofu kuhusu mahakama hiyo kwa kuwa bado hawana uelewa.
Awali akifungua semina hiyo, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alisema baada ya Serikali kuwashirikisha wadau mbalimbali ikaamua kuuleta muswada huo ambao utatambu Mahakama ya Kadhi.
Alisema mahakama hizo zilianzishwa tangu mwaka 212  na kwamba zipo kesi zinashughulikiwa huko na kwamba hakuna mkono wa Serikali katika kugharamia mahakama hizo.
“Wenzetu wanataka mahakama zetu zitambue hukumu zinazotolewa na Mahakama za Kadhi, na mahakama hizi hazishighulikii masuala ya jinai isipokuwa masauala ya Ndoa, miradhi, talaka na wakfu,” alisema.
Alisema mabadiliko hayo hayavunji Katiba kama ambavyo watu wengi walikuwa na hofu hiyo na kwamba Katiba inayopendekezwa hakuna kipingele kinachozungumzia mahakama hiyo.
Mtoa mada katika semina hiyo iliyoandaliwa na Wizara ya Katiba na Sheria alikuwa ni Jaji Robert Makaramba

Kwa upande wa Harubu Shamsi, alisema licha ya kuhitajika kwa mahakama hiyo, siyo sahihi kwani wameshindwa  kusimamia haki za msingi ikiwamo kuuza aridhi.
“Mkiwapa na hii watavunja ndoa za watu ili waowe wake zao” alisema.
Alisema muswada haukidhi mahitaji ya waisilamu na kuwa ni sawa danganya toto.
Mbunge wa Nkasi Kasikazini, Alli Kesy, alisema hakubaliani na suala la mahakama ya kadhi kwani siyo kati ya nguzo kuu za waisilamu.
Alisema baadhi ya wabunge wanaotaka mahakama hiyo hawaheshimu nguzo muhimu ya dini hiyo ambayo ni kuswali na badala yake hutumia muda mrefu kunywa pombe.
Naye Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, alisema serikali inasema haita hudumia mahakama hiyo lakini kuna nyaraka za kamati ndoyo ya serikali ambayo pamoja na mambo mengine inaonyesha kwamba Serikali itasaidia uanzishwaji wa mahakama hiyo kwenye hatua za awali.
Alisema nyaraka hiyo ambayo iliwasilishwa pia kwenye kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria, inasema sehemu ya vitu vitakavyotolewa na serikali ni pamoja na mafunzo na majengo.
Pinda
Akifunga warsha hiyo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda,  alisema baada ya kusikiliza wabunge hao alitambua kuwa ndani ya waisilamu wenyewe hakuna maelewano juu ya uanzishwaji wa mahakama hiyo.
Alisema kuwa, baada ya kuona hali hiyo serikali itaona kama jukumu lake kurekebisha  hiyo hali ama laa.
Alisema pia ameona kuwa, baadhi ya watu wanafikiri kwamba sheria iliyotungwa na serikali ni kilemba cha ukoka kwa waisilamu.
“Kwamba baadhi ya waisilamu hatujawafikisha pale wanapotaka, lakini hiki ni matokeo ya mjadala ulioibuka ndani ya bunge la katiba,” alisema.
Alisema wasiwasi mwingine ni ule wa kuona kwamba, yawezekana kuna kilichojificha nyuma ya muswada huo na kwamba baada ya kupitishwa kwa sheria hiyo mambo mengine yaingizwe kimiakimia.

w

Comments

Popular posts from this blog

AJIRA MPYA 41,500 SERIKALINI ZATANGAZWA KATIBU MKUU UTUMISHI JUMA MKOMI

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

WALIOPITA KURA ZA MAONI CCM HAWA HAPA