WAZIRI WA UCHUKUZI PROFESA MBARAWA AOMBA BAJETI YA SH TRILIONI 2.87 KWA MWAKA 2026 HADI 2027
Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, akiwasilisha bakjeti ya Wizara hiyo leo bungeni jijini Dodoma hebu fuatana naye katika hotuba yake hii. Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, ambayo imechambua
utekelezaji wa Bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2025/26
pamoja na Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa
fedha 2026/27, ninaomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu sasa likubali
kupokea, kujadili na kuidhinisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi
ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2026/27.
2. Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa
rehema kwa kutujalia uhai na kutuwezesha kukutana tena siku ya leo kujadili
maendeleo ya Sekta ya Uchukuzi. Ninamuomba Mwenyezi Mungu atuongoze
vyema katika kujadili Hotuba hii ya Wizara ya Uchukuzi na Bajeti ya Serikali
kwa ujumla ili kufikia malengo ya Dira 2050 katika kuwaletea Watanzania
maendeleo.
3. Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee naomba kumpongeza
Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa ushindi alioupata katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 29
Oktoba, 2025. Ushindi huu unaonesha imani kubwa ambayo Watanzania
1
wameendelea kuwa nayo kwa Uongozi wake wenye maono na unaowaletea
wananchi maendeleo. Aidha, napenda kumpongeza kwa dhati kwa hatua
madhubuti alizochukua katika kutekeleza ahadi alizotoa kwa wananchi ndani
ya siku 100 za mwanzo katika kipindi chake cha awamu ya pili. Utekelezaji
huo umeonesha dhamira ya kweli ya kuhakikisha kuwa Serikali inatekeleza
ahadi zilizotolewa na kuleta matokeo chanya katika sekta mbalimbali nchini.
Tunamtakia Mheshimiwa Rais afya njema, umri mrefu, hekima na mafanikio
zaidi katika kuiongoza nchi yetu ili kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa letu.
4. Mheshimiwa Spika, naomba kutumia fursa hii, kumpongeza Mheshimiwa
Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kwa mchango wake mkubwa wa kumsaidia
Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu ya Serikali. Aidha,
ameendelea kusimamia kikamilifu Masuala ya Muungano na Mazingira.
5. Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa. Dkt. Mwigulu Lameck
Nchemba (Mb.), kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais na kuthibitishwa kwa
kishindo na Bunge hili Tukufu kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Wote ni mashahidi kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu ameonesha
umahiri mkubwa katika kusimamia shughuli za Serikali.
6. Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kukupongeza wewe binafsi kwa
kuchaguliwa kwa kishindo na Waheshimiwa Wabunge kuwa Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nimpongeze pia Mheshimiwa Daniel
Barran Sillo (Mb.), kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge hili Tukufu.
Aidha, nitumie fursa hii kuwapongeza Wenyeviti wa Bunge, Mheshimiwa
Najma Murtaza Giga (Mb.) na Mheshimiwa Philip Mwanyika (Mb.) kwa
kuendelea kuaminiwa kuwa Wenyeviti wa Bunge. Kwa namna ya kipekee
2
nimpongeze Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso (Mb.) kwa kuchaguliwa pia
kuwa Mwenyekiti wa Bunge.
7. Mheshimiwa Spika, naishukuru na kuipongeza sana Kamati ya Kudumu
ya Bunge ya Miundombinu inayoongozwa na Mwenyekiti Mheshimiwa
Selemani Moshi Kakoso (Mb.) ambaye amechaguliwa kwa mara nyingine tena
kuiongoza Kamati hiyo. Napenda pia kuishukuru Kamati hii kwa uchambuzi
uliyoufanya kwenye Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti kwa mwaka
wa fedha 2025/26 na Mpango wa Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa
Mwaka wa fedha 2026/27.
8. Mheshimiwa Spika, vilevile, namshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais, kwa
kuendelea kuniamini na kuniteua katika nafasi hii kwa mara nyingine ya
kuongoza Wizara ya Uchukuzi. Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais ya
kuwa, kwa kushirikiana na Naibu Waziri Mheshimiwa David Kihenzile (Mb.),
tutatekeleza majukumu aliyotukabidhi kwa kufuata miongozo anayotupatia
pamoja na miongozo mingine ya nchi yetu. Pia, tutaendelea kutekeleza
shughuli za Wizara ili kuweza kufikia malengo mahsusi ya kuendeleza Sekta
ya Uchukuzi na kuwa na mchango mkubwa katika kuchochea ukuaji wa
Uchumi wa Taifa. Vilevile, niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri na Naibu
Mawaziri walioaminiwa na kuteuliwa ili kuongoza Wizara mbalimbali.
9. Mheshimiwa Spika, nitumie siku ya leo kuwapongeza Waheshimiwa
Wabunge wote walioteuliwa na waliochaguliwa kuwawakilisha wananchi
katika Bunge hili Tukufu la 13. Niwahakikishie kuwa, Wizara iko tayari
kupokea ushauri na maoni ya Watanzania kupitia kwenu ili kuendelea kutatua
kero na changamoto zilizopo.
3
10. Mheshimiwa Spika, kwa masikitiko makubwa nitoe pole kwa Bunge lako
Tukufu, familia na Watanzania wote kufuatia kifo cha Mheshimiwa Jenista
Joakim Mhagama aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho kilichotokea
tarehe 11 Desemba, 2025; Mheshimiwa Halima Iddi Nassor aliyekuwa
Mbunge wa Viti Maalum kilichotokea tarehe 18 Januari, 2026; na Mheshimiwa
William Vangimembe Lukuvi aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Isimani na Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu
kilichotokea tarehe 25 Machi, 2026. Hakika tutaendelea kuthamini na kuenzi
michango yao katika Bunge hili na Taifa kwa ujumla. Tunamwomba Mwenyezi
Mungu awapumzishe mahali pema peponi, Amina.
11. Mheshimiwa Spika, kabla ya kuendelea na uwasilishaji wangu,
niwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba
(Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa
Prof. Kitila Mkumbo (Mb.), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Mipango na
Uwekezaji kwa hotuba zao ambazo zimefafanua utendaji wa Serikali kwa
mwaka wa fedha 2025/26 na mwelekeo kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Vilevile, nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote waliowasilisha hotuba
zao kabla yangu.
12. Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, naomba sasa uniruhusu
niwasilishe Taarifa ya Mapitio ya Mchango wa Sekta ya Uchukuzi katika
kukuza uchumi wa Taifa; Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara ya
Uchukuzi na Taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2025/26 hadi kufikia Machi,
2026; na Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha
2026/27. Aidha, nitahitimisha kwa kuomba Bunge lako Tukufu liidhinishe bajeti
kwa ajili ya kutekeleza shughuli na miradi ya Wizara ya Uchukuzi (Fungu 62)
kwa mwaka wa fedha 2026/27.
4
B. MCHANGO WA SEKTA YA UCHUKUZI KATIKA KUKUZA UCHUMI WA
TAIFA
13. Mheshimiwa Spika, Sekta ya Uchukuzi imeendelea kutoa mchango
mkubwa katika kuchochea shughuli za uzalishaji na utoaji huduma katika
sekta mbalimbali. Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa ya
mwaka 2024, Sekta ya Uchukuzi ilikua kwa asilimia 4.2 na kuchangia katika
Pato la Taifa kwa asilimia 7.5, ambapo imekuwa ya tano (5) kati ya sekta
kubwa 17 katika kuchangia Pato la Taifa.
14. Mheshimiwa Spika, Sekta ya Uchukuzi imeendelea kuchangia zaidi
katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali yatokanayo na huduma za bandari.
Mathalan, kati ya mwaka wa fedha 2020/21 hadi mwaka wa fedha 2024/25,
mapato yatokanayo na kodi ya forodha za kibandari yalichangia wastani wa
asilimia 40 ya mapato yote yaliyokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania
(TRA). Aidha, mapato hayo yataendelea kuongezeka siku hadi siku.
15. Mheshimiwa Spika, vilevile, Sekta ya Uchukuzi imeendelea kuchangia
katika upatikanaji wa fedha za kigeni kupitia mauzo ya huduma za uchukuzi,
usafirishaji na huduma za kibandari. Taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania ya
mwaka 2025, inaonesha kuwa Sekta ya Uchukuzi ilichangia mauzo ya kiasi
cha Dola za Marekani bilioni 2.79 ikilinganishwa na Dola za Marekani bilioni
2.35 zilichangia
kwa mwaka 2024.
5
16. Mheshimiwa Spika, katika kukuza upatikanaji wa ajira nchini, Sekta ya
Uchukuzi imeendelea kutoa ajira 198,480 wakati wa ujenzi wa miundombinu
pamoja na utoaji wa huduma za uchukuzi.
(Maelezo ya kina kuhusu mchango wa Sekta ya Uchukuzi katika kukuza
Uchumi wa Taifa yameainishwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya
ya 14 hadi 20)
C. UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA WIZARA NA TAASISI
ZAKE KWA MWAKA WA FEDHA 2025/26
17. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2025/26, Wizara ya
Uchukuzi (Fungu 62) iliidhinishiwa jumla ya Shilingi Trilioni 2.746 kwa ajili ya
Matumizi ya Kawaida na utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo. Kati ya fedha
hizo, Shilingi Bilioni 125.438 zilikuwa ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida,
sawa na asilimia 4.57 na Shilingi Trilioni 2.621 zilikuwa kwa ajili ya miradi ya
maendeleo, sawa na asilimia 95.43. Hadi kufikia Machi, 2026 jumla ya Shilingi
Trilioni 1.374 zilikuwa zimetolewa ikiwa ni sawa na asilimia 66.75 ya Shilingi
Trilioni 2.059 zilizotakiwa kutolewa katika kipindi hicho. Kati ya fedha hizo
zilizotolewa, Shilingi Bilioni 99.682 ni fedha za Matumizi ya Kawaida na
Shilingi Trilioni 1.275 ni fedha za miradi ya maendeleo. Baada ya kupokea
fedha hizo, Wizara ya Uchukuzi iliendelea kutekeleza majukumu yake katika
maeneo mbalimbali kama ifuatavyo:-
C:1 UDHIBITI NA UTOAJI WA HUDUMA ZA UCHUKUZI
UDHIBITI WA HUDUMA ZA USAFIRI WA ANGA
6
18. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza majukumu ya udhibiti wa usafiri wa
anga, Serikali kupitia Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA)
imeendelea kusimamia ubora wa viwanja vya ndege nchini. Aidha, Shirika la
Usafiri wa Anga Duniani (ICAO) limeendelea kuikasimisha Tanzania jukumu la
uongozaji ndege zinazoruka na kupita urefu wa futi elfu 25 juu ya anga la nchi
ya Burundi. Sambamba na jukumu hilo, katika kipindi cha Julai 2025 hadi
Machi 2026, jumla ya ndege 189 zilifanyiwa ukaguzi na kupewa vyeti vya
ubora na kuendelea kufanya kazi nchini.
19. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, abiria
waliotumia usafiri wa anga waliongezeka na kufikia abiria Milioni 6.81
ikilinganishwa na abiria Milioni 6.037 katika kipindi kama hicho cha mwaka wa
fedha 2024/25, sawa na ongezeko la asilimia 12.63. Kwa upande wa mizigo
katika kipindi hicho, jumla ya tani 34,750.2 zilisafirishwa ndani na nje ya nchi,
ikilinganishwa na tani 33,112.5 zilizosafirishwa ndani na nje ya nchi katika
kipindi kama hicho mwaka 2024/25.
20. Mheshimiwa Spika, Naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa, Serikali
ya Awamu ya Sita kupitia TCAA imeendelea na ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa
Anga (CATC) Jijini Dar es Salaam ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia
11.3.
(Maelezo ya kina kuhusu udhibiti wa utoaji wa huduma za usafiri wa anga
kupitia TCAA yameainishwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya
24 hadi 38)
UDHIBITI WA USAFIRI ARDHINI
7
21. Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini
(LATRA), imeendelea kutekeleza majukumu ya kusimamia udhibiti wa usafiri
ardhini katika maeneo makuu matatu (3) ya usafiri wa barabara, reli na waya.
Katika kutekeleza majukumu hayo, LATRA katika kipindi cha kuanzia Julai
2025 hadi Machi 2026, ilitoa leseni 388,715 za usafirishaji, ikiwa ni ongezeko
la asilimia 55 kutoka mwaka uliopita. Leseni hizo zilihusisha mabasi ya abiria,
magari ya mizigo na ya kukodi. Vilevile, Serikali kupitia LATRA imeendelea
kudhibiti nauli na ubora wa huduma huku ikihamasisha matumizi ya nishati
mbadala ikiwemo magari ya umeme nchini.
22. Mheshimiwa Spika, Mabasi 13,843 yaliunganishwa kwenye mfumo wa
ufuatiliaji wa VTS na madereva 12,699 walisajiliwa kwa ajili ya kuongeza
usalama wa safari. Aidha, Mfumo wa Tiketi Mtandao (CeTS) umeendelea
kutumika ambapo mabasi 8,126 yaliunganishwa na zaidi ya abiria milioni 21
walitumia mfumo wa tiketi mtandao kununua tiketi hadi kufikia Machi 2026.
(Maelezo ya kina kuhusu udhibiti wa usafiri ardhini kupitia LATRA
yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 39 hadi 57)
UDHIBITI WA USAFIRI MAJINI
23. Mheshimiwa Spika, katika kusimamia udhibiti wa usafiri majini, Serikali
kupitia Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) imeendelea kusimamia
usalama wa vyombo vya usafiri majini; kudhibiti uchafuzi wa mazingira
unaotokana na shughuli za meli katika eneo la Tanzania Bara; na kutoa
huduma ya ugomboaji na uondoshaji wa shehena kwa bidhaa mahsusi.
Udhibiti wa Watoa Huduma za Usafirishaji Majini
8
24. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, jumla
ya watoa huduma 1,794 walisajiliwa na kupewa leseni, ikilinganishwa na
watoa huduma 1,556 waliosajiliwa katika kipindi kama hicho kwa mwaka wa
fedha 2024/25.
25. Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha usalama wa usafiri katika Ziwa
Victoria, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na
Serikali ya Uganda zimeendelea kutekeleza Mradi wa Kikanda wa Kuboresha
Mawasiliano na Uchukuzi katika ziwa hilo. Mradi huo unajumuisha ujenzi wa
Kituo Kikuu cha Uratibu wa Utafutaji na Uokoaji, na ununuzi wa boti mbili (2)
za utafutaji na uokoaji pamoja na boti ya matibabu (Ambulance Boat) ambazo
zimeanza kutoa huduma katika Ziwa Victoria. Vilevile, Serikali imenunua boti
nyingine mbili (2) za kisasa za utafutaji na uokoaji ambazo zimeanza kutoa
huduma katika Ziwa Tanganyika na katika ukanda wa Bahari ya Hindi eneo la
Mkoa wa Tanga.
(Maelezo ya kina kuhusu udhibiti wa usafiri majini kupitia TASAC
yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 58 hadi 69)
UDHIBITI NA UTOAJI HUDUMA ZA HALI YA HEWA
26. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania
(TMA) imeendelea na utoaji na udhibiti wa huduma za hali ya hewa nchini.
27. Mheshimiwa Spika, katika kuboresha huduma za hali ya hewa
zinazotolewa kwa sekta ndogo ya usafiri wa anga, TMA imekamilisha ufungaji
wa mitambo miwili (2) ya uangazi wa hali ya hewa katika viwanja vya ndege
9
vya Mpanda na Pemba. Aidha, TMA imeendelea na ujenzi wa miundombinu
ya hali ya hewa ikiwemo maabara ya uhakiki wa vifaa vya hali ya hewa
(Calibration Center) Dar es Salaam ambayo ujenzi wake umefikia asilimia 46.
(Maelezo ya kina kuhusu udhibiti na utoaji huduma za hali ya hewa kupitia
TMA yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 70 hadi
83)
C:2 UTOAJI WA HUDUMA ZA UCHUKUZI
HUDUMA ZA BANDARI
28. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari
Tanzania (TPA), inaendelea kusimamia bandari za mwambao wa Bahari ya
Hindi na Maziwa Makuu kwa kuendeleza miundombinu na utoaji wa huduma
za kibandari kwa viwango vinavyokubalika kikanda na kimataifa. Katika kipindi
cha Julai, 2025 hadi Machi 2026, TPA ilihudumia jumla ya tani milioni 29.66 za
shehena, ikilinganishwa na tani milioni 23.18 zilizohudumiwa katika kipindi
kama hicho cha mwaka wa fedha 2024/25, sawa na ongezeko la asilimia
27.96. Aidha, shehena iliyosafirishwa kwenda nchi jirani imeongezeka hadi
kufikia tani milioni 10.93, ikilinganishwa na tani milioni 8.24 zilizohudumiwa
katika kipindi kama hicho kwa mwaka wa fedha 2024/25, sawa na ongezeko
la asilimia 32.64. Ongezeko hilo limetokana na uboreshaji wa miundombinu
na ushirikishwaji wa Sekta Binafsi.
29. Mheshimiwa Spika, tangu kupata uhuru, nchi yetu imekuwa na
changamoto ya kuhifadhi mafuta. Serikali ya awamu ya Sita imeamua
kulifanyia kazi suala hilo kwa vitendo, ambapo TPA imeanza ujenzi wa
miundombinu ya kupokelea na kuhifadhi mafuta (Single Receiving Terminal –
SRT) unaohusisha ujenzi wa matenki 15 ya mafuta (tank farms) yenye uwezo
10
wa kuhifadhi mita za ujazo 378,000, ambapo utekelezaji umefikia asilimia 42
na unatarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2026.
30. Mheshimiwa Spika, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi Mkuu wa
2025, imeainisha umuhimu wa kujenga Bandari ya Bagamoyo. Napenda
kulitaarifu bunge lako Tukufu kuwa, Serikali kupitia TPA inakamilisha
maandalizi ya kuanza utekelezaji wa mradi huo wa kimkakati. Bandari hiyo
itahusisha ujenzi wa gati lenye urefu wa kilomita 1.32 pamoja na
miundombinu wezeshi ya kuhudumia meli kubwa za kisasa aina za Megamax
ambazo haziwezi kuhudumiwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwa sasa.
Katika kutekeleza awamu ya kwanza ya Mradi huo, tayari mitambo kwa ajili ya
uchimbaji wa kina cha maji imepatikana na kazi hiyo inatarajiwa kuanza rasmi
katika mwaka wa fedha 2026/27.
31. Mheshimiwa Spika, ili kupunguza msongamano katika Bandari ya Dar es
Salaam, Serikali imeendelea kuhimiza matumizi ya bandari kavu nchini
ikiwemo Bandari Kavu ya Kwala iliyopo Mkoa wa Pwani ambayo imeendelea
kutoa huduma, ambapo hadi kufikia mwezi Machi, 2026 bandari hiyo
ilihudumia makasha 14,460. Katika hatua nyingine, mwezi Machi, 2026 TRC
ilianza usafirishaji wa shehena kwenda katika Bandari Kavu ya Isaka.
32. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha bandari katika
Maziwa Makuu nchini ambapo hadi kufikia mwezi Machi, 2026 uboreshaji wa
Bandari za Bukoba na Kemondo umekamilika na uboreshaji wa Bandari ya
Mwanza North umefikia asilimia 75. Serikali inaendelea na Mradi wa
Uboreshaji wa Bandari ya Kigoma ambao umefikia asilimia 13. Kwa upande
wa bandari ya Mbamba Bay umefikia asilimia 49. Ushirikishwaji wa Sekta
11
Binafsi Katika Shughuli za Uendelezaji na Uendeshaji wa Bandari ya Dar es
Salaam
33. Mheshimiwa Spika, Kama inavyokumbukwa, mwaka 2023 Serikali ya
Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu
Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ilifanya uamuzi wa
kimkakati wa kushirikisha Sekta Binafsi katika shughuli za uendelezaji na
uendeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam kwa lengo la kuongeza ufanisi,
ushindani na tija katika utoaji wa huduma za kibandari nchini.
Kutokana na uamuzi huo, Serikali kupitia Wizara ya Uchukuzi iliingia mikataba
na waendeshaji mahiri wa bandari wenye uzoefu mkubwa kimataifa. Hatua
hiyo imeendelea kuzaa matokeo chanya na manufaa makubwa kwa Taifa,
ikidhihirisha dira sahihi ya Serikali katika kuimarisha uchumi wa buluu na
nafasi ya Tanzania kama lango kuu la biashara kwa ukanda wa Afrika
Mashariki na Kati.
Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na yafuatayo:-
i. Kuongezeka kwa shehena inayohudumiwa katika Bandari ya Dar es Salaam
kutoka tani milioni 16.27 mwaka wa fedha 2020/21 hadi kufikia tani milioni
27.76 mwaka 2024/25, sawa na ongezeko la asilimia 70.62;
ii. Kuongezeka kwa wastani wa shehena ya makasha yanayohudumiwa kwa
mwezi kutoka makasha TEUs 61,000 hadi TEUs 102,000, sawa na ongezeko
la asilimia 67.21;
iii. Kupungua kwa gharama za uendeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam
kutoka Shilingi bilioni 652.83 mwaka 2023/24 hadi Shilingi bilioni 308.95
mwaka 2024/25;
12
iv. Kuongezeka kwa makusanyo ya mapato ya TPA yatokanayo na ada za
huduma za kibandari kutoka Shilingi bilioni 896.95 mwaka 2020/21 hadi
kufikia Shilingi trilioni 1.30 mwaka 2024/25;
v. Kupungua kwa muda wa kuhudumia meli za makasha gatini kutoka wastani
wa siku 10 hadi siku 3; na
vi. Kupungua kwa muda wa meli kusubiri nangani kutoka wastani wa siku 46
hadi wastani wa siku 7 kwa meli za mizigo mchanganyiko na kichele, Hatua
za Serikali Kukabiliana na Ongezeko la Shehena katika Bandari ya Dar es
Salaam
35. Mheshimiwa Spika, Kutokana na kuongezeka kwa ufanisi wa Bandari ya
Dar es Salaam pamoja na kuimarika kwa imani ya watumiaji wa bandari hiyo
ndani na nje ya nchi, kumekuwepo na ongezeko kubwa la shehena ya mizigo
inayohudumiwa bandarini. Ili kuhakikisha bandari inaendelea kutoa huduma
kwa ufanisi, ushindani na viwango vinavyokidhi mahitaji yanayoongezeka,
Serikali inaendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kimkakati zifuatazo:-
i. Kukamilisha ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR inayoingia moja kwa moja
bandarini (Port Link), ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 99.7 na
majaribio ya usafirishaji wa mizigo kwa treni yanaendelea. Sambamba na hilo
TRC, inaendelea kujenga eneo maalum (loading platform) la kupakilia mizigo
kwenye treni za SGR ndani ya eneo la bandari kwa lengo la kuongeza kasi,
na ufanisi katika utowaji wa mizigo Bandarini;
ii. Kuendelea na upanuzi wa eneo la Kurasini lenye ukubwa wa mita za mraba
220,000 kwa ajili ya kuhudumia makasha 700,000 kwa mwaka. Awamu ya
kwanza ya mradi huo inatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2026 na kuhudumia
13
makasha 150,000 kwa mwaka, huku Awamu ya Pili ikitarajiwa kukamilika
mwezi Julai 2027;
iii. Kujenga kituo cha kisasa cha mizigo katika Stesheni ya SGR Morogoro
chenye ukubwa wa mita za mraba 68,000 na uwezo wa kuhudumia makasha
600 kwa siku, kwa ajili ya kuhudumia mizigo inayosafirishwa kwa njia ya
barabara kuelekea mikoa mbalimbali na nchi za jirani.
(Maelezo ya kina kuhusu huduma za bandari, yameainishwa katika Kitabu cha
Hotuba yangu kuanzia Aya ya 84 hadi 110).
HUDUMA ZA USAFIRI WA RELI
Huduma za Usafiri kupitia Reli za MGR na SGR
36. Mheshimiwa Spika, Wizara inaishukuru Serikali kwa kuchukua hatua za
kuboresha Shirika la Reli Tanzania (TRC), zoezi lililoanza mwaka 2017. Tangu
kuanzishwa kwa Shirika hili, Serikali imekuwa ikitoa ruzuku ya mishahara.
Naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa, katika mwaka 2026/27, TRC
haitatengewa tena ruzuku kwa ajili ya mishahara kutoka Serikalini.
37. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TRC, imeendelea na ujenzi na
uendeshaji wa reli ya SGR pamoja na kuboresha mtandao wa reli ya MGR
yenye urefu wa takriban kilomita 2,707. Ujenzi wa reli ya SGR unatekelezwa
kwa awamu mbili ikihusisha kilomita 1,219 za njia kuu kwa awamu ya kwanza
kutoka Dar es Salaam – Mwanza; na kilomita 1,590 za awamu ya pili
ikijumuisha vipande vya Tabora – Kigoma na Uvinza – Musongati. Kukamilika
kwa awamu hizo mbili za reli ya SGR kutaifanya Tanzania kuwa na mtandao
wa jumla ya kilomita 2,809 za reli ya SGR.
14
Uendelezaji na Uendeshaji wa Reli ya Kisasa ya SGR
38. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TRC imeendelea na ujenzi wa Reli ya
SGR ambapo hadi kufikia mwezi Machi, 2026 ujenzi wa kipande cha kwanza
Dar es Salam – Morogoro (km 300) na kipande cha pili Morogoro –
Makutupora (km 422) umekamilika kwa sehemu kubwa. Aidha, TRC
inaendelea na utoaji wa huduma ya usafiri wa treni kwa vipande husika. Kwa
kipande cha Mwanza – Isaka (km 341), ujenzi unaendelea na umefikia
asilimia 68.77.
39. Mheshimiwa Spika, Hadi kufikia mwezi Machi 2026, ujenzi wa reli ya
SGR katika kipande cha tatu: Makutupora – Tabora (km 368) na kipande cha
nne: Tabora – Isaka (km 165) unaendelea ambapo kazi mbalimbali
zinazoendelea kutekelezwa. Kwa ujumla ujenzi wa vipande hivi 2 umekuwa
na changamoto kwa muda mrefu, ambazo zilisababisha utekelezaji wake
kuwa na kasi ndogo. Hata hivyo, Serikali tayari imepata suluhisho la
kukamilisha ujenzi wake kwa kupata mkopo wenye masharti nafuu wa
thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.277, sawa na takriban Shilingi trilioni
3.32.
Usafirishaji wa Abiria na Mizigo kwa Reli za SGR na MGR
40. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TRC imeendelea na usafirishaji wa
abiria kati ya Dar es Salaam na Dodoma kupitia reli ya SGR. Usafirishaji
kupitia reli hiyo umezidi kuimarika ambapo katika kipindi cha Julai, 2025 hadi
Machi, 2026 jumla ya abiria milioni 2.51 walisafirishwa ikilinganishwa na abiria
15
millioni 2.05 waliosafirishwa katika kipindi kama hicho kwa mwaka wa fedha
2024/25 sawa na ongezeko la asilimia 22.40.
41. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia Julai, 2025 hadi kufikia
mwezi Machi 2026, TRC ilisafirisha jumla ya tani 102,452 za mizigo ikiwa ni
utekelezaji wa ahadi ya Serikali ya kuanza usafirishaji wa mizigo kupitia reli ya
SGR.
42. Mheshimiwa Spika, Katika hatua za kuunganisha miundombinu ya reli ya
SGR na MGR, Serikali imeendelea na uunganishaji wa reli hizo katika eneo la
Ruvu ili kuwezesha usafirishaji wa mizigo kutoka Bandari za Dar es Salaam
na Tanga, ambapo utekelezaji wake umefika asilimia 85. Aidha, ujenzi wa
kuunganisha reli za MGR na SGR unaendelea katika eneo la Bahi kwa lengo
la kuwezesha uhamishaji wa mizigo (transhipment) kati ya reli hizo 2 na
unaendelea vizuri.
43. Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuboresha Reli ya MGR kwa
kubadilisha reli nyepesi na kuweka nzito, pamoja na kuongeza uwezo wa
madaraja. Ukarabati huo unaendelea kupitia Mfuko wa Reli, ambapo hadi
Machi 2026, kipande cha Kaliua–Mpanda kilikuwa kimekamilika kwa asilimia
32.72.
44. Mheshimiwa Spika, Kukabiliana na mafuriko yanayoathiri Reli ya MGR
katika eneo la Kilosa–Kidete–Igandu, Serikali imekamilisha ujenzi wa njia ya
reli yenye urefu wa km 6.2 na daraja katika eneo la Godegode–Gulwe
ambapo ujenzi umefikia asilimia 99. Aidha, kupitia Mradi wa TIRP II Wizara ya
Uchukuzi kwa kushirikiana na Wadau, inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa
mabwawa sita (Kidete, Kimagai, Buigiri, Ikowa, Hombolo na Dabalo) katika
16
Mto Kinyasungwe. Mabwawa hayo yatapunguza mafuriko na kuboresha
uendeshaji wa reli mwaka mzima.
Huduma za Usafiri kupitia Reli ya TAZARA
45. Mheshimiwa Spika, Serikali ya Tanzania na Zambia zimeendelea
kushirikiana katika kusafirisha mizigo na abiria kwa kutumia Mamlaka ya Reli
ya Tanzania na Zambia (TAZARA). Lakini, kwa muda mrefu reli hii imekuwa
na ufanisi mdogo kutokana na uchakavu wa miundombinu na uhaba wa
vitendea kazi.
46. Mheshimiwa Spika, utakumbuka kuwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Hotuba yake
wakati wa kufungua Rasmi Bunge la 13, tarehe 14 Novemba 2025, alilitaarifu
Bunge lako Tukufu kuwa Serikali yake kwa kushirikiana na nchi mwanahisa
imeanza mkakati mahsusi wa kufanya maboresho makubwa ya reli ya
TAZARA. Napenda kulitaarifu Bunge lako kuwa, uzinduzi wa mradi wa ufufuaji
wa reli ya TAZARA ulifanyika tarehe 20 Novemba, 2025 jijini Lusaka nchini
Zambia. Uzinduzi huo ulifanyika kufuatia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Zambia mnamo tarehe 29 Septemba,
2025 kusaini mkataba wa uendeshaji (Concession Agreement) na Kampuni ya
CCECC kutoka nchini kwa ajili ya kuboresha reli ya TAZARA. Kampuni hii
itawekeza jumla ya Dola za Marekani bilioni 1.4, ambayo ni sawa na takriban
Shilingi trilioni 3.6. Maboresho ya reli hii yanatarajiwa kuongeza uwezo wa
kusafirisha mizigo milioni 2.4 kwa mwaka na kuzalisha ajira mpya 100,000.
17
(Maelezo ya kina kuhusu huduma za usafiri wa reli na utekelezaji wa miradi ya
miundombinu ya reli kupitia TRC na TAZARA yameoneshwa katika Kitabu cha
Hotuba yangu kuanzia Aya ya 111 hadi 145).
HUDUMA ZA UCHUKUZI KATIKA BAHARI NA MAZIWA MAKUU
Huduma za Usafiri na Usafirishaji katika Maziwa Makuu
47. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TASHICO imeendelea kusimamia
ujenzi wa meli mpya na ukarabati wa meli zilizopo ili kuimarisha usafiri wa
abiria na usafirishaji wa mizigo. Kwa kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026
TASHICO ilisafirisha abiria 128,191 na tani 71,796.25 za mizigo ikiwa ni sawa
na ongezeko la asilimia 22.51 ukilinganisha na kipindi kama hicho kwa
mwaka uliopita.
48. Mheshimiwa Spika, Serikali imekamillisha ujenzi wa Meli ya MV. New
Mwanza katika Ziwa Victoria. Serikali pia imeendelea na ukarabati wa meli
katika Ziwa Victoria, ambapo ukarabati wa meli ya uokozi ya MT. Ukerewe
umefikia asilimia 79. Vilevile, Serikali kupitia TASHICO imeanza maandalizi
ya ujenzi wa meli yenye uwezo wa kubeba tani 3,000 za mizigo katika ziwa
hilo.
Mikakati ya Serikali ya Awamu ya Sita Kutumia Fursa zilizopo ukanda wa Ziwa
Tanganyika
49. Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa ukanda wa Ziwa
Tanganyika, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt.
Samia Suluhu Hassan, imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo:
18
Ujenzi wa meli nne (4) za mizigo katika Ziwa Tanganyika zinazojengwa na
TPA kwa kushirikiana na Sekta Binafsi ambazo zina uwezo wa kubeba tani
2,000 za mizigo kila meli moja na kwa sasa meli hizo zimekamilika; kuanza
ujenzi wa meli mpya ya Abiria, kuanza ujenzi wa karakana ya ujenzi wa meli;
Kuanza ujenzi wa magati mawili (2) ya kisasa katika Bandari ya Kigoma,
ambao hadi Machi, 2026 utekelezaji wake umefikia asilimia 13; Kuendelea na
ukarabati wa meli ya MV. Liemba ambao umefikia asilimia 64.
(Maelezo ya kina kuhusu huduma za uchukuzi katika bahari na maziwa
makuu kupitia TASHICO yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu
kuanzia Aya ya 146 hadi 156)
HUDUMA ZA VIWANJA VYA NDEGE
50. Mheshimiwa Spika, katika uendelezaji na uendeshaji wa miundombinu
ya viwanja vya ndege nchini, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA)
imeendelea kusimamia na kuendeleza viwanja vya ndege vya Serikali.
51. Mheshimiwa Spika, katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi
Mkuu wa mwaka 2025, Serikali imeahidi kukipandisha hadhi Kiwanja cha
Ndege cha Mwanza kuwa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa. Wizara kwa
kushirikiana na TAA tayari imekamilisha Upembuzi Yakinifu na Usanifu wa
Kina wa Mradi wa Ujenzi wa Jengo Jipya la abiria litakalokuwa na uwezo wa
kuhudumia abiria milioni 2.5 kwa mwaka pamoja na miundombinu wezeshi.
Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kufanyika kwa ushirikiano Kati ya TAA
na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
19
Hadi kufikia Machi 2026, Wizara kupitia TAA imeendelea na uboreshaji wa
Kiwanja cha Ndege cha Arusha ambapo ufungaji wa mfumo wa taa za
kuongozea ndege umefikia asilimia 65 na ujenzi wa tabaka la juu la lami la
barabara ya kuruka na kutua kwa ndege katika kiwanja hicho unaendelea.
52. Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza viwanja vya ndege vya mikoa,
Wizara kupitia TAA inaendelea na uboreshaji wa Kiwanja cha Ndege cha
Musoma na Kiwanja cha Ndege cha Moshi. Pia, kwa upande wa Mradi wa
ujenzi wa Kiwanja Kipya cha Ndege cha Mkoa wa Kagera, kazi ya Upembuzi
Yakinifu na Usanifu wa Awali zinaendelea.
53. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TAA imeendelea na utekelezaji wa
maboresho ya Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA)
ikiwemo: ukarabati wa barabara ya kuruka na kutua ndege; ufungaji wa
mfumo wa taa za kuongozea ndege (AGL), na ujenzi wa eneo la kuhifadhia
mizigo mikavu (dry cargo) ambao umefikia asilimia 5 yanaendelea. Aidha,
wakandarasi wa ujenzi wa Jengo Jipya la Watu Mashuhuri (New VIP Terminal)
wamepatikana na maandalizi ya ujenzi yanaendelea.
(Maelezo ya kina kuhusu huduma za viwanja vya ndege kupitia TAA
yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 157 hadi 167)
HUDUMA ZA USAFIRI WA ANGA
54. Mheshimiwa Spika, Tangu mwaka 2015, Serikali imeendelea kuifufua
Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL), ambapo idadi ya ndege imeongezeka
kutoka ndege 1 mwaka 2016 hadi ndege 16 mwaka 2026. Mafanikio
yaliyopatikana ni pamoja na ongezeko la abiria kutoka 107,166 mwaka
20
2016/17 hadi 1,178,025 mwaka 2024/25, mapato kuongezeka kutoka Shilingi
bilioni 23 hadi bilioni 595.7, pamoja na mapato ya fedha za kigeni kupanda
kutoka Dola milioni 9.85 hadi milioni 157.7.
55. Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, ATCL
ilisafirisha abiria 1,072,528 sawa na ongezeko la asilimia 22.38 ikilinganishwa
na kipindi kama hicho mwaka uliopita, huku tani 4,129.72 za mizigo
zikisafirishwa.
56. Mheshimiwa Spika, Licha ya mafanikio hayo, kampuni bado inakabiliwa
na changamoto ya mtaji mdogo na mfumo wa umiliki wa ndege unaoathiri
mizania ya kifedha. Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuboresha mfumo
huo ili kuimarisha ufanisi na Mizania wa kihesabu ya ATCL.
(Maelezo ya kina kuhusu huduma za usafiri wa anga kupitia ATCL
yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 168 hadi 180
C:3 VYUO VYA MAFUNZO VYA KISEKTA NA MASUALA MTAMBUKA
57. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Uchukuzi inasimamia uendeshaji wa vyuo
vya mafunzo ya kisekta vilivyo chini yake ili kuhakikisha sekta ya usafirishaji
na usafiri nchini inakuwa na wataalam wa ndani wakutosha.
Chuo Cha Taifa Cha Usafirishaji (NIT) na Chuo cha Bahari Dar es Salaam
(DMI)
58. Mheshimiwa Spika, katika kuendelea kukijengea uwezo Chuo cha NIT na
DMI Serikali imeendelea kutekeleza Miradi ya Kuboresha Miundombinu na
21
Vifaa vya Kufundishia. Na hii imeongeza udahili kwa kozi mbalimbali kwa kiasi
kikubwa kama inavyoonyeshwa kwenye kitabu changu cha hotuba ya bajeti
kuanzia Aya ya 181 hadi 206.
C:5 MAFANIKIO, CHANGAMOTO NA HATUA ZILIZOCHUKULIWA
C:5:1 MAFANIKIO
59. Mheshimiwa Spika, Naomba niainishe kwa muhtasari mafanikio
makubwa yaliyopatikana katika mwaka wa fedha 2025/26, hadi mwezi Machi,
2026 kama ifuatavyo:-
1.
Kuendelea na Ujenzi wa Reli ya SGR kwa Awamu zote Mbili
60. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na ujenzi wa Reli ya SGR kwa
awamu zote mbili (2) na utekelezaji wake upo katika hatua mbalimbali kama
ilivyoainishwa katika Kitabu changu cha Hotuba.
2.
Kuendelea kwa Ufanisi wa Usafirishaji wa Abiria kupitia Reli
ya SGR
22
61. Mheshimiwa Spika, Sote ni mashuhuda kuwa, usafirishaji wa abiria na
mizigo kupitia reli ya SGR umeendelea kuimarika kati ya Dar es Salaam na
Dodoma ambapo takriban wastani wa abiria 280,000 husafiri kwa mwezi,
sawa na abiria 9,300 kwa siku. Kwa mwenendo huu, inakadiriwa kuwa, zaidi
ya abiria milioni 3 watakuwa wamesafirishwa kufikia mwishoni mwa mwaka
wa fedha 2025/26, ikilinganishwa na wastani wa abiria 400,000 wanaosafiri
kwa reli ya MGR kwa mwaka. Kutokana na uendeshaji huo, katika kipindi cha
kuanzia Julai, 2025 hadi Machi 2026, jumla ya Shilingi bilioni 82.77
zimekusanywa. Aidha, takwimu hizo zinafanya Serikali kuwa imekusanya
jumla ya Shilingi bilioni 169.37 tangu kuanza kwa safari za SGR nchini mwezi
Juni, 2024.
3.
Kuanza Usafirishaji wa Mizigo kwa Reli ya SGR
62. Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya mwaka wa fedha 2025/26,
niliahidi kuanza huduma ya usafirishaji wa mizigo kupitia reli ya SGR.
Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa, mwezi Julai, 2025 TRC ilianza
rasmi usafirishaji wa mizigo kupitia Reli ya SGR kati ya Dar es Salaam na
Dodoma (Ihumwa).
4.
Serikali
TRC kuanza Kujiendesha bila Ruzuku kutoka Mfuko Mkuu wa
63. Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa kuanzia
Januari, 2026 TRC imefanikiwa kuanza kujitegemea kwa upande wa
Mishahara na Matumizi Mengineyo (OC) bila uwezeshaji kutoka Mfuko Mkuu
23
wa Serikali. Kwa kipindi cha takriban miaka 10, kiasi cha Shilingi bilioni 12.92
kila mwaka kilikuwa kinatolewa na Serikali kwa TRC kwa ajili ya mishahara.
5.
Shehena
Kuongeza Uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam Kuhudumia
64. Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuiongezea uwezo Bandari ya Dar es
Salaam katika kuhudumia shehena, Serikali inaendelea na upanuzi wa eneo
la Kurasini (Kurasini Port Extension) lenye ukubwa wa mita za mraba 220,000
kwa ajili ya kuhudumia makasha 700,000 kwa mwaka.
6.
Ufanisi wa Ushiriki wa Sekta Binafsi katika Bandari ya Dar es
Salaam na Kuongezeka kwa Shehena kwa Bandari zote Nchini
65. Mheshimiwa Spika, kutokana na kuendelea kwa utaratibu wa
kushirikisha Sekta Binafsi katika uendeshaji wa bandari nchini hususan
Bandari ya Dar es Salaam, kwa kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026
shehena iliyohudumiwa katika Bandari ya Dar es Salaam ilifikia tani milioni
27.83 ikilinganishwa na tani milioni 19.31 zilizohudumiwa katika kipindi kama
hicho mwaka 2024/25, sawa na ongezeko la asilimia 29.83. Aidha, inatarajiwa
kuwa shehena ya mizigo itakayohudumiwa na Bandari hii itaongezeka hadi
kufikia wastani wa tani milioni 40.839 na kwa Bandari zote shehena ya mizigo
inategemewa kufikia Milioni 59.768 kwa mwaka 2030/31.
7.
Kuimarisha usafiri katika Maziwa Makuu
24
66. Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha ujenzi wa Meli ya MV. New
Mwanza katika Ziwa Victoria. Aidha, ukarabati wa meli ya MT. Sangara
umekamilika na sasa imeanza kutoa huduma. Vilevile, Serikali kupitia TPA
kwa kushirikiana na Sekta Binafsi imekamilisha ujenzi wa meli nne (4) za
mizigo katika Ziwa Tanganyika zenye uwezo wa kusafirisha tani 8,000 za
mizigo.
8.
Kuongezeka kwa Mtandao wa Vituo vya Usafiri wa Anga
Vinavyohudumiwa na ATCL
67. Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi za Serikali katika kuimarisha
utendaji, Kampuni ya ATCL imeongeza vituo vya huduma ya usafiri wa anga
ambapo hadi kufikia Machi, 2026 ina jumla ya vituo 33 ikilinganishwa na vituo
23 vilivyokuwepo mwaka 2020/21. Kati ya vituo hivyo, vituo 16 ni vya ndani ya
nchi vituo (14) vya kikanda na vituo 3 vya nje ya Bara la Afrika.
9.
Kuimarika kwa Ukusanyaji wa Mapato Yatokanayo na Huduma
za Usafiri wa Anga kupitia ATCL
68. Mheshimiwa Spika, Kampuni ya ATCL kwa mwaka 2024/25 ilikusanya
mapato ya Shilingi bilioni 626.5 ikilinganishwa na Shilingi bilioni 175.69
zilizokusanywa mwaka 2020/21.
10. Kuimarika kwa Huduma za Viwanja vya Ndege
69. Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha huduma za usafiri wa anga nchini,
Serikali imekamilisha ukarabati wa viwanja vya ndege vya Sumbawanga,
Songea, Shinyanga na Tabora. Aidha, ukarabati mkubwa wa jengo la
25
kuhifadhi mizigo inayoharibika haraka (perishables) katika Kiwanja cha Ndege
cha KIA umekamilika na hivyo kuchochea kuimarika kwa mnyororo wa
usafirishaji.
11. Kuanza Kutolewa kwa Mafunzo ya Urubani Nchini
70. Mheshimiwa Spika, kama nilivyoahidi katika Hotuba yangu ya mwaka
2025/26 kuwa Serikali itaanza rasmi kutoa mafunzo ya urubani katika Chuo
cha Taifa cha Usafirishaji (NIT). Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa,
Serikali kupitia Chuo cha NIT imeanza rasmi kutoa mafunzo ya urubani mwezi
Julai 2025, ambapo wanafunzi 22 wamedahiliwa na wanaendelea na
masomo. Mafanikio hayo yamewezesha kupunguza gharama za masomo nje
ya nchi kwa kozi za urubani. Kuanza kutolewa kwa mafunzo hayo ni
utekelezaji wa maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha usafiri wa anga.
(Maelezo ya kina kuhusu mafanikio yaliyopatikana hadi kufikia Machi, 2026
yameoneshwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 223 hadi 252)
C:5:2 CHANGAMOTO NA HATUA ZILIZOCHUKULIWA
71. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Uchukuzi imekabiliwa na changamoto
mbalimbali katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mwaka 2025/26.
Changamoto hizo na mikakati ya kuzitatua zimeoneshwa katika Kitabu cha
Hotuba yangu kuanzia Aya ya 253 hadi 254.
D. MPANGO NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA
WA FEDHA 2026/27
26
72. Mheshimiwa Spika, katika Mpango na Bajeti ya mwaka wa fedha
2026/27, Wizara imezingatia Dira 2050, Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya Chama
cha Mapinduzi ya Mwaka 2025, Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka
Mitano (FYDP IV 2026/27 – 2030/31), Mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa
mwaka 2026/27, Mpango Mkakati wa Wizara wa Miaka Mitano (2026/27 –
2030/31) pamoja na maelekezo ya Viongozi Wakuu wa Serikali.
73. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2026/27, Wizara ina vipaumbele
mbalimbali ambavyo ni pamoja na:
1.
Kuendelea na ujenzi na uendeshaji wa Reli ya Kisasa ya SGR;
2.
TAZARA;
3.
4.
5.
6.
7.
8.
Kuendelea na ukarabati na uboreshaji wa Reli za MGR na
Uboreshaji wa miundombinu na huduma katika Bandari;
Kuendelea na uboreshaji wa usafiri wa anga;
Kuendelea na ujenzi na ukarabati wa meli;
Kuendelea kuboresha huduma za hali ya hewa;
Kuboresha udhibiti, ubora na usalama wa huduma za uchukuzi; na
Kuendelea na uboreshaji wa vyuo vya mafunzo vya kisekta.
74. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Uchukuzi (Fungu 62) katika mwaka wa
fedha 2026/27 imetengewa jumla ya Shilingi Trilioni 2.872 ambapo kati ya
fedha hizo, Shilingi Bilioni 126.04 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida, sawa
na asilimia 4.38 ya bajeti, na Shilingi Trilioni 2. 746 ni kwa ajili ya utekelezaji
wa Miradi ya Maendeleo, sawa na asilimia 95.62.
75. Mheshimiwa Spika, Kati ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya Matumizi ya
Kawaida, Shilingi Bilioni 100.135 ni kwa ajili ya Mishahara ya watumishi na
27
Shilingi Bilioni 25.906 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo (OC) kwa Wizara na
Taasisi zinazopokea Ruzuku. Vilevile, kati ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya
utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Shilingi Trilioni 2.452 ni fedha za ndani
na Shilingi Bilioni 294.184 ni fedha za nje.
(Vipaumbele na bajeti iliyotengwa katika mwaka wa fedha 2026/27
vimeainishwa katika Kitabu cha Hotuba yangu kuanzia Aya ya 255 hadi 259)
D:1 MIRADI YA MAENDELEO ITAKAYOTEKELEZWA KATIKA MWAKA
2026/27
76. Mheshimiwa Spika, Miradi ya kielelezo na kimkakati itakayotekelezwa
kwa mwaka wa fedha 2026/27 kama ifuatavyo:
Miradi ya Uboreshaji wa Miundombinu ya Bandari na Huduma za Usafiri
Majini
77. Mheshimiwa Spika, miradi itakayotekelezwa katika eneo hili ni:
1.
Mradi wa Uboreshaji wa Bandari ya Dar es Salaam (DMGP);
Miradi mingine ya uboreshaji wa bandari itatekelezwa kupitia mapato ya
ndani ya TPA ikiwemo uboreshaji wa bandari za mwambao wa Bahari ya
Hindi: Bandari ya Bagamoyo, Bandari ya Mtwara (Kisiwa Mbao) na bandari za
28
Maziwa Makuu: Bandari ya Mwanza North, Mbamba Bay, na Mradi wa
Uboreshaji wa Bandari ya Kigoma; na
78.
Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Bandari ya Dar es Salaam kupitia
sekta binafsi, DP World inaendelea na mpango mkubwa wa uwekezaji katika
vifaa vya kisasa vya kuhudumia mizigo, lengo likiwa ni kuongeza ufanisi, kasi
na ushindani wa huduma za bandari. Kufikia mwaka 2025/2026, kampuni
tayari imevuka zaidi ya nusu ya lengo la uwekezaji la dola milioni 250 sawa na
shilingi bilioni 650 ndani ya miaka mitano, ikiwa ni mafanikio makubwa ndani
ya miaka miwili ya kwanza ya utekelezaji.
Katika mwaka wa fedha 2026/2027, maboresho yataendelea kupitia upanuzi
wa miundombinu, uboreshaji wa mifumo ya utendaji, na kuimarisha uwezo wa
kuhudumia mizigo kwa viwango vya kisasa. Miongoni mwa mipango hiyo ni
ununuzi wa mitambo ya kisasa ya upakuaji na upakiaji (cranes), ujenzi wa
mageti mawili yanayounganisha bandari na Barabara ya Nelson Mandela,
pamoja na uwekezaji katika mitambo ya kushughulikia shehena za kichele
(dry bulk) utakaoongeza uwezo kwa asilimia 65 hadi takriban tani milioni 5.5.
Aidha, uwezo wa kuhudumia mizigo mchanganyiko utaongezeka kwa asilimia
25, huku sekta ya usafirishaji wa magari (PCC na PCTC) ikitarajiwa kukua
kwa asilimia 30 kutokana na maboresho ya sera na miundombinu. Hatua hizi
pia zitaongeza ufanisi wa bandari za Tanga na Mtwara.
Kwa ujumla, ifikapo mwaka 2028, sekta ya bandari inatarajiwa kuwa imepiga
hatua kubwa ya mageuzi, ikiwa na uwezo wa juu zaidi wa kuhudumia mizigo,
kasi ya huduma, na ushindani wa kimataifa, hivyo kuifanya Tanzania kuwa
kitovu muhimu cha biashara katika ukanda mzima.
29
2. Miradi ya kuboresha Usafiri wa Anga na Hali ya Hewa Nchini
79. Mheshimiwa Spika, Miradi hiyo ni pamoja na:
1.
Ununuzi wa Ndege na Uimarishaji wa Kampuni ya ATCL;
2.
3.
Ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga;
Ujenzi, ukarabati na uboreshaji wa viwanja vya ndege vya
Mwanza,
Arusha, Mtwara, Serengeti, Kagera, Kilimanjaro (KIA) na Julius
Nyerere (JNIA); na
4.
Viwanja vya ndege vya mikoa: Moshi, Lindi, Njombe, Musoma na
Singida.
3. Miradi ya Uendelezaji wa Miundombinu ya Reli
80. Mheshimiwa Spika, miradi itakayotekelezwa ni:
1.
Ujenzi wa reli ya SGR na ukarabati na uboreshaji wa reli za MGR
na reli ya TAZARA.
2.
ambapo
3.
Ujenzi wa Reli ya Treni ya Mjini katika Jiji la Dar es Salaam
Upembuzi Yakinifu utafanyika mwaka 2026/27; na
Ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Mafunzo ya Reli.
4. Miradi ya Uboreshaji wa Vyuo vya Mafunzo ya Kisekta
81. Mheshimiwa Spika, miradi itakayotekelezwa katika eneo hili ni
1. Ujenzi wa Miundombinu na Ununuzi wa Vifaa vya Kufundishia katika
Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT);
2. Mradi wa Uanzishwaji wa Kampasi ya Lindi katika Sekta ya Usafiri
Majini, Mafuta na Gesi; na
30
3. Mradi wa East Africa Skills for Transformation and Regional Intergration
(EASTRIP).
(Maelezo ya kina kuhusu miradi itakayotekelezwa kwa mwaka 2026/27 na
fedha zilizotengwa kwa kila mradi yameainishwa katika Kitabu cha Hotuba
yangu kuanzia Aya ya 260 hadi 286)
D:2. SHUGHULI NYINGINE ZITAKAZOTEKELEZWA KWA MWAKA 2026/27
82. Mheshimiwa Spika, kazi nyingine zitakazotekelezwa na Wizara kupitia
Mapato ya Ndani ya Taasisi zilizo chini yake katika udhibiti, utoaji huduma za
Uchukuzi, na masuala ya kisera na mtambuka zimeanishwa katika Kitabu cha
Hotuba yangu Aya ya 287 hadi 314.
E. SHUKRANI
83. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara kwa
Mwaka 2025/26, umeleta mafanikio makubwa. Mafanikinio ambayo Wizara
imeyapata yasingewezakana kutokea bila ya ushauri na usimamizi wa Bunge
Lako Tukufu. Kutokana na mafanikio hayo, naomba nitoe shukrani za kipekee
kwako wewe binafsi Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge wenzangu
kwa ushauri na michango yenu ambayo imewezesha Wizara kufikia mafanikio
hayo. Aidha, niwashukuru wananchi na wadau wengine kwa kuendelea kutoa
michango ya hali na mali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja
na kuendelea kushirikiana na Serikali katika kulinda miundombinu ya
usafirishaji ambayo Serikali imewekeza kiasi kikubwa cha fedha za Umma.
31
84. Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kuwapongeza na kutambua
michango inayotolewa na viongozi wanaonisaidia katika utekelezaji wa
majukumu ya Wizara, kwa kuanza na Naibu Waziri, Mheshimiwa David
Mwakiposa Kihenzile (Mb.); na Katibu Mkuu, Prof. Godius Walter Kahyarara.
Vilevile, niishukuru Menejimenti ya Wizara; Wakuu wa Taasisi za Wizara;
pamoja na Watumishi wote wa Wizara na Taasisi kwa juhudi zao katika
utekelezaji wa majukumu ya Wizara na Taifa kwa ujumla.
85. Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee nishukuru Taasisi na
Mashirika ya Kitaifa na Kimataifa ambayo yameshirikiana na Wizara katika
uendelezaji wa Sekta ya Uchukuzi nchini. Ninaomba kutaja baadhi ya
Mashirika ya Kitaifa kama ifuatavyo: Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya NSSF na
PSSSF; Taasisi za kifedha za CRDB, NMB, AZANIA BANK, NBC na TCB na
Asasi mbalimbali za kiraia. Aidha, Mashirika ya Kimataifa/Wadau wa
Maendeleo wanaoendelea kushirikiana na Wizara ambao ni pamoja na: Trade
Mark Africa (TMA); Shirika la Bahari Duniani (IMO); Shirika la Kimataifa la
Usafiri wa Anga (ICAO); Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO); Benki ya
Maendeleo ya Afrika (AfDB); Benki ya Dunia (WB); Shirika la Kimataifa la
Maendeleo la Japan (JICA); Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Korea Kusini
(KOICA); Foreign Commonwealth and Development Office (FCDO); Shirika la
Maendeleo la Ufaransa (AFD); Shirika la Nchi Zinazouza Mafuta ya Petroli Nje
ya Nchi zao (OPEC); Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU); Benki ya Uwekezaji
ya Ulaya (EIB); Shirika la Chakula Duniani (WFP); na Shirika la Biashara na
Maendeleo la Marekani (USTDA).
86. Mheshimiwa Spika, Wizara pia inashukuru ushirikiano kutoka nchi za
kikanda kupitia Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na
Sekretarieti ya Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC). Vilevile, kutoka
32
Nchi za Urusi; Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE); Uingereza; China;
Sweden, Denmark; Korea Kusini; Jamhuri ya Czech; na Uturuki. Na mwisho si
kwa umuhimu nishukuru Sekta Binafsi, hususan wafanyabiashara na watoa
huduma za uchukuzi kwa kuendelea kutoa huduma za uchukuzi.
(Maelezo ya kina ya shukrani yameainishwa katika Kitabu cha Hotuba yangu
kuanzia Aya ya 315 hadi 319).
F. MUHTASARI WA MAOMBI YA FEDHA YA WIZARA YA UCHUKUZI
KATIKA MWAKA WA FEDHA 2026/27
87. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2026/27, Wizara ya
Uchukuzi inaliomba Bunge lako Tukufu kuidhinisha bajeti yenye jumla ya
Shilingi 2,872,738,082,000. Kati ya fedha hizo, Shilingi 126,041,236,000 ni
kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi 2,746,696,846,000 ni fedha za
Miradi ya Maendeleo.
88. Mheshimiwa Spika, pamoja na Hotuba hii, nimeambatisha majedwali
mbalimbali yenye taarifa na takwimu kwa ajili ya kutoa uelewa zaidi kwa
Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kuhusu Sekta ya Uchukuzi. Naomba
majedwali hayo ambayo yameainishwa katika Kitabu cha Hotuba yangu
kuanzia ukurasa 198 hadi ukurasa 247 yachukuliwe kama sehemu ya hotuba
hii.
Hotuba hii pia inapatikana katika tovuti ya Wizara (www.uchukuzi.go.tz).
89. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
Wakuu wa Taasisi zilizopo chini ya wizara hiyo na wenyeviti wa bodi zake wakisikiliza hotuba ya bajeti hiyo leo
Wanafunzi wa Shule ya Kiislamu ya Ira ya Kondoa, wakishuhudia hotuba ya waziri Profesa Mbarawa ndani ya ukumbi wa Bunge
Wakuu wa Taasisi zilizopo chini ya wizara hiyo na wenyeviti wa bodi zake wakisikiliza hotuba ya bajeti hiyo leo
Wanafunzi wa Shule ya Kiislamu ya Ira ya Kondoa, wakishuhudia hotuba ya waziri Profesa Mbarawa ndani ya ukumbi wa Bunge
Comments
Post a Comment