LEO NI SIKU YA TAKWIMU BARANI AFRIKA

 Mkurugenzi wa Taifa ,Uchumi na Sera wa Benki Kuu (BoT), Johnson Nyella, akisoma hotuba kwa niaba ya Gavana wa Benki kuu katika  maadhimisho ya siku ya Takwimu Afrika iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam, hebu fuatilia hotuba hiyo hapa chini


HOTUBA YA MGENI RASMI,
GAVANA WA BENKI KUU TANZANIA,
WAKATI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA TAKWIMU AFRIKA TAREHE 20 NOVEMBA, 2017 KATIKA
UKUMBI WA KIMATAIFA WA MIKUTANO WA MWALIMU JULIUS NYERERE, DAR ES SALAAM
       Mwenyekiti wa Bodi ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu;
Mkurugenzi Mkuu Ofisi ya Taifa ya Takwimu;
Menejimenti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu;
Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi, Zanzibar,
Washiriki kutoka katika Wizara, Idara na Taasisi za Umma na Sekta Binafsi;
Wawakilishi wa Vyuo Vikuu na Taasisi za Utafiti Tanzania;
Wawakilishi wa shule za Sekondari;
Wadau wa Maendeleo;
Wageni Waalikwa;
Waandishi wa Habari;
Mabibi na Mabwana.

Ndugu Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kukutana siku ya leo ili kuadhimisha SIKU YA TAKWIMU AFRIKA KWA MWAKA 2017.  Aidha, natoa shukrani zangu za dhati kwa heshima kubwa mliyonipa ya kuwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho haya muhimu.
         
Ndugu Mwenyekiti, napenda kutumia fursa hii kuwakumbusha Washiriki wenzangu kuwa Siku ya Takwimu Afrika huadhimishwa kila tarehe 18 Novemba ya kila mwaka.  Siku hii hutoa fursa kwa Nchi kutathmini na kufuatilia malengo yaliyofikiwa katika Mipango ya Maendeleo ya ndani na nje ya Nchi. Kama alivyotangulia kusema Mkurugenzi Mkuu, kauli mbali mbali zimekuwa zikijadiliwa kila mwaka tangu mwaka 1990, na kauli mbiu ya mwaka huu ni “Takwimu Bora za Uchumi kwa Maisha Bora”.

Ndugu Mwenyekiti, kabla sijaanza kuzungumzia kaulimbiu hii, naomba nitoe kwanza baadhi ya takwimu za kiuchumi kwa nchi ya Tanzania, kwa miaka ya hivi karibuni.  Takwimu za uchumi ni pamoja na takwimu zinazohusu pato la taifa, mfumuko wa bei, viwanda, ujenzi, kilimo, utalii n.k.  Tanzania ni kati ya nchi za Afrika zenye viwango vya juu vya ukuaji wa uchumi katika kipindi cha muongo mmoja uliopita (2007 - 2016).  Uchumi wa nchi ulikua kwa wastani wa asilimia 6.7. Mwaka 2016,  Pato la Taifa lilikua kwa wastani wa asilimia 7.0, sawa na ilivyokuwa mwaka 2015 na 2014.  Kwa miaka minne mfululizo, mfumuko wa bei wa Taifa umeendelea kupungua na kubaki katika kiwango cha tarakimu moja.  Mwaka 2016, mfumuko wa bei ulipungua na kufikia wastani wa asilimia 5.2 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 5.6 mwaka 2015 na asilimia 6.1 mwaka 2014.

Ndugu Mwenyekiti, katika kipindi hicho, sekta ya viwanda ilikua kwa wastani wa asilimia 7.5 na kuchangia wastani wa asilimia 6.5 katika Pato la Taifa.  Kiwango cha ukuaji wa shughuli za kiuchumi za kilimo kwa mwaka 2016, kilipungua na kuwa asilimia 2.1 ikilinganishwa na asilimia 2.3 mwaka 2015.  Mwaka 2014 ukuaji wa shughuli za kiuchumi za kilimo ulikua kwa asilimia 3.4. Shughuli za kiuchumi za kilimo zilichangia asilimia 29.0 ya Pato la Taifa mwaka 2015 na 2016. Mapato yatokanayo na biashara ya utalii yaliongezeka hadi dola za Marekani milioni 2,073 kutoka dola za Marekani milioni 1,901.9 mwaka 2015, sawa na ongezeko la asilimia 9.0.  Ongezeko hilo lilitokana na kuongezeka kwa idadi ya watalii waliotembelea nchini kwa asilimia 12.9 kutoka watalii 1,137,182  mwaka 2015 hadi watalii 1,284,279  mwaka  2016.

 Ukuaji wa uchumi kwa kiasi kikubwa uliendana na kasi ya kupungua kwa umaskini. Umaskini ulipungua kutoka asilimia 34.4 mwaka 2007 hadi asilimia 28.2 mwaka 2012.  Kwa kipindi cha miaka 15 umaskini ulipungua kwa asilimia 4.6.  Kwa kipindi cha miaka mitano ya karibuni umaskini ulipungua kwa asilimia 6.2.    

          Ndugu mwenyekiti, takwimu bora za uchumi ni muhimu katika kupanga mipango ya maendeleo na utungaji wa sera kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi. Wakati nchi mbali mbali duniani ikiwemo Tanzania zimeanza kutekeleza Agenda ya Maendeleo Endelevu ya Mwaka 2030, mahitaji ya takwimu bora za uchumi yanahitajika sana. Tathmini ya utekelezaji wa malengo haya italeta changamoto kubwa hasa kwa nchi zinazoendelea kutokana na mahitaji makubwa ya takwimu bora.  Njia mojawapo ya kutatua changamoto hizi ni kwa wadau mbalimbali wa takwimu kufanya kazi kwa ushirikiano.  Wadau hao ni pamoja na wazalishaji na watumiaji wa takwimu, taasisi za elimu ya juu, sekta binafsi na asasi za kiraia.    

          Ndugu Mwenyekiti, takwimu bora za kiuchumi zinasaidia kuongeza tija serikalini katika kupanga mipango ya maendeleo na kukabiliana na changamoto kadri zinavyojitokeza.  Aidha, takwimu bora zinasaidia watunga sera na watekelezaji wa programu mbali mbali na kupanga mikakati mipya ya kuboresha maisha ya wananchi.  

          Ndugu Mwenyekiti, Serikali kwa kupitia Ofisi ya Taifa ya Takwimu inaimarisha Mfumo wa Takwimu nchini kwa lengo la kupata takwimu bora za kiuchumi na kijamii kwa ajili ya uimarishaji wa utungaji wa sera na tathmini za mipango yetu ya maendeleo kama vile Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/17-2020/21.  

Ndugu Mwenyekiti, Sote kwa ujumla wetu tunafahamu umuhimu wa viashiria vya uchumi jumla katika kuwavutia wawekezaji hapa Nchini na hususani katika Viwanda vyetu; ukizingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ya kuiwezesha Tanzania kufikia hadhi ya nchi zenye uchumi wa kipato cha kati unaoongozwa na uchumi wa viwanda.  Hivyo, Serikali inahitaji kupata kwa wakati takwimu za uchumi zenye ubora unaozingatia Kanuni zilizowekwa na Ofisi ya Takwimu ya Umoja wa Mataifa.

Ndugu Mwenyekiti, niruhusu nitoe ufafanuzi kuhusu Sheria ya Takwimu Na. 9 ya Mwaka 2015 ili kuondoa mkanganyiko uliojitokeza kutokana na maudhui ya sheria husika.  Sheria hii haina lengo la kuzuia taasisi au watu binafsi kufanya tafiti zao hapa nchini, ila inalenga kuweka misingi inayotakiwa kuzingatiwa na wadau katika utoaji wa takwimu rasmi.  Kuanzishwa kwa sheria hii kunalenga kutoa miongozo kwa taasisi za Serikali, mashirika na watu binafsi wanaotoa takwimu rasmi nchini kuendesha shughuli za ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji unaozingatia weledi na taratibu zinazokubalika.

Ndugu Mwenyekiti, kabla ya kuhitimisha naomba nitoe wito kwa jamii ya watakwimu.  Kutokana na mahitaji makubwa ya takwimu kwa matumizi mbalimbali, ni muhimu kuimarisha mbinu za uzalishaji wa takwimu kwa kutumia teknolojia za kisasa.  Matumizi ya teknolojia yataipunguzia Serikali gharama za uzalishaji wa takwimu na kuongeza ubora.

Pili; hakikisheni kuwa wadau wote waliopo kwenye mfumo wa utoaji na utumiaji wa takwimu mnashirikiana katika uzalishaji wa takwimu ili kupunguza “kukosekana kwa ulinganifu wa takwimu (data inconsistencies)” na duplications effort.

Tatu; endeleeni kuongeza nguvu zaidi katika kuelimisha umma kuhusu matumizi ya takwimu bora katika kupanga, kufuatilia na kutathmini mipango ya maendeleo ya Afrika na Nchi yetu kwa ujumla. Waelimisheni Wahariri wa Vyombo vya Habari ili watusaidie kutoa elimu ya matumizi bora ya takwimu kwa wadau wote ndani na nje ya Nchi.

          Ndugu Mwenyekiti, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana, kabla sijahitimisha hotuba yangu ninapenda kutambua michango mbalimbali ya wadau wote wanaounga mkono juhudi za serikali katika kuboresha tasnia ya Takwimu hapa Nchini.  Wadau hawa ni pamoja na Benki ya Dunia, DFID, Jumuia ya Ulaya, JICA, IMF, USAID, SIDA, CANADA, Mashirika ya Umoja wa Mataifa – UNICEF, UNFPA, UNDP, FAO, Irish Embassy na wadau wengine wote wa Maendeleo.

Aidha, nishukuru Vyombo vya Habari kwa ushirikiano mkubwa waliouonesha katika juhudi za kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa Takwimu katika kupanga na kutathimini mipango ya maendeleo. Niwaombe wadau wote wa Takwimu nchini, hasa wananchi, kuendelea kutoa ushirikiano katika mazoezi mbalimbali ya ukusanyaji wa Takwimu yanayofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kutoa taarifa sahihi. Taarifa hizo zinaiwezesha Serikali kujipima na kuandaa mipango ya kuboresha maisha ya wananchi.

Baada ya kusema haya, napenda nitumie fursa hii kutamka rasmi kuwa MAADHIMISHO YA SIKU YA TAKWIMU AFRIKA 2017 yamefunguliwa rasmi.  Mwenyezi Mungu awabariki.

Ahsanteni kwa kunisikiliza.





Wageni waalikwa katika maadhimisho hayo wakisikiliza hotuba 



Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dk. Albina Chuwa, akizungumza na waandishi wa habari katika maadhimisho ya siku ya Takwimu Afrika, yaliyofanyika jijini Dar es salaam leo. Hebu fuatilia hotyuba yake hapo chini=,.




MAELEZO MAFUPI YA MKURUGENZI MKUU WA
OFISI YA TAIFA YA TAKWIMU,  DKT. ALBINA CHUWA
WAKATI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA TAKWIMU AFRIKA TAREHE 20 NOVEMBA, 2017 KATIKA UKUMBI WA KIMATAIFA WA MIKUTANO WA MWALIMU NYERERE,
DAR ES SALAAM













Ndugu Mgeni Rasmi;
Mwenyekiti wa Bodi ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu;
Menejimenti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu;
Watakwimu na Wachumi kutoka katika Wizara, Idara na Taasisi za Umma na Sekta Binafsi;
Wawakilishi wa Vyuo Vikuu, Asasi za kiraia na Taasisi za Utafiti;
Wawakilishi wa Shule za Sekondari;
Wadau wa Maendeleo;
Wageni Waalikwa;
Waandishi wa Habari;
Mabibi na Mabwana.















Ndugu Mgeni Rasmi, napenda kuungana na Watakwimu na Washiriki wote mliokusanyika siku ya leo kwa lengo la kuadhimisha SIKU YA TAKWIMU AFRIKA KWA MWAKA 2017.  Pia nitumie fursa hii, kutoa shukrani zangu za dhati kwako pamoja na wageni wote mlioalikwa, kwa kuweza kuhudhuria maadhimisho haya pamoja nasi.  Mwenyezi Mungu awabariki.

Ndugu Mgeni Rasmi, kila tarehe 18 Novemba ya kila mwaka  Tanzania huungana na nchi zingine za kiafrika kuadhimisha Siku ya Takwimu Afrika .  Madhumuni makubwa ya kuadhimisha siku hii ni kuongeza uelewa wa umma juu ya umuhimu wa takwimu katika nyanja zote za kimaisha ya kijamii na kiuchumi.  Kauli Mbiu ya mwaka huu ni “Takwimu bora za uchumi kwa maisha bora" na inalenga kusisitiza umuhimu wa takwimu za kiuchumi katika kuleta maendeleo endelevu, na hivyo kuboresha maisha ya wananchi barani Afrika.

Ndugu Mgeni Rasmi, tangu mwaka 1990, maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika huwa yanaandaliwa kutokana na kaulimbiu mbali mbali zinazohusiana na umuhimu wa takwimu katika kupanga maendeleo na kutunga sera katika Bara la Afrika.  Kati ya kaulimbiu ambazo zimeshajadiliwa tangu mwaka 1990 ni pamoja na usawa wa jinsi, hali ya mazingira, takwimu huria, ulemavu na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika uzalishaji wa takwimu.

Ndugu Mgeni Rasmi, kaulimbiu hizi huandaliwa na Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi ya Afrika  (UNECA) kwa kushirikiana na Ofisi za Takwimu za Afrika.  Nchi za Afrika zilikubaliana kuwa kaulimbiu “Takwimu Bora za Uchumi kwa Maisha Bora” iadhimishwe mwaka huu kwa sababu ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa takwimu za uchumi, unahitaji weledi mkubwa hususani katika kipindi hiki cha utekelezaji wa Agenda ya Afrika ya mwaka 2063 na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Mwaka 2030.  Hapa Nchini kaulimbiu ya mwaka huu inaenda sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na Mpango wa Pili wa Maendelo wa Taifa (2016/17  hadi 2020/21).  Kama mnavyofahamu Programu zote hizi zinalenga kukuza uchumi na kupunguza umaskini hapa Nchini.

Ndugu Mgeni Rasmi, ili takwimu zitumike kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi, zinahitajika kuwa takwimu bora na za kuaminika.  Takwimu bora ni takwimu zilizo sahihi, zinazotolewa kwa wakati, linganifu na za kina na zinazozalishwa mara kwa mara na zenye ufanisi. Sifa hizi zote zinaendana na Kanuni za msingi za takwimu rasmi za Umoja wa mataifa na Mkataba wa takwimu wa Afrika ambazo nasi tumeridhia.  Pia, takwimu bora ni lazima ziweze kupatikana kirahisi na kutumika na watumiaji wa aina mbalimbali na ziwe kwenye wigo mpana kuweza kukidhi mahitaji ya watunga sera na jamii kwa ujumla.   

Ndugu Mgeni Rasmi, takwimu bora za uchumi kwa nchi yetu ni za muhimu sana, hasa wakati huu ambao Serikali yetu inaimarisha Uchumi wa Viwanda, ili Tanzania iweze kuwa Nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025 na hivyo kuboresha zaidi maisha ya wananchi.  Takwimu hizi za uchumi ni pamoja na takwimu za kilimo, viwanda, ujenzi, usafirishaji, nishati, biashara, mazingira, mfumuko wa bei na uwekezaji.
            Ndugu Mgeni Rasmi, kwa kutumia takwimu, tunaweza kujua muundo wa kisekta na mwenendo wa uchumi na kwa hiyo sera zinazochochea ukuaji wa uchumi zinaweza kutungwa au kupitiwa upya. Kwa mfano, sekta ya kilimo huchangia sehemu kubwa ya shughuli za kiuchumi katika nchi zinazoendelea, inatengeneza ajira nyingi na hivyo inaboresha maisha ya wananchi. Mwaka 2016 sekta ya kilimo hapa nchini ilichangia asilimia 29.1 katika pato la Taifa. Takwimu za kilimo hutoa taarifa za pembejeo na kipato kutokana na kilimo, pia inajumuisha uzalishaji wa mazao, bidhaa za mifugo, misitu na bidhaa za uvuvi, matumizi ya ardhi, mitambo ya kilimo, matumizi ya maji, mbolea, na dawa. Maendeleo ya takwimu za kilimo ni muhimu kwa ufuatiliaji wa kupunguza umasikini, usalama wa chakula, utunzaji wa mazingira, na kuboresha maisha ya wananchi. 
 
            Ndugu Mgeni Rasmi, takwimu za nishati zinasaidia kuelewa hali ya nishati nchini, asilimia ngapi ya nishati mbadala kama vile umeme jua, biogas, na vyanzo vingine vya nishati bora na endelevu inatumika Nchini. Pia hutumika kusaidia kuelewa jinsi gani na ni wapi nishati husambazwa, kiasi gani cha nishati kilichopotea wakati wa usambazaji kwenye gridi ya taifa na athari zake juu ya upatikanaji na uhakika wa usambazaji wa nishati nchini. Ugavi endelevu wa nishati na ufanisi wa usambazaji huhakikisha kuwa nchi inaweza kutoa nishati bora kwa wakazi wake. Hapa Tanzania mwaka 2016, shughuli za kiuchumi za usambazaji umeme zilikua kwa asilimia 8.5 ikilinganishwa na ukuaji halisi wa asilimia 5.8 mwaka 2015.
            Ndugu Mgeni Rasmi, maendeleo ya viwanda ni kipaumbele cha nchi katika kufikia uchumi wa kati. Katika kipindi cha mwaka 2007 – 2016, takwimu zinaonesha sekta ya viwanda ilikua kwa wastani wa asilimia 7.5 na kuchangia wastani wa asilimia 6.5 katika pato la taifa. Sekta hii inaajiri wastani wa asilimia 3.1 ya nguvu kazi na kuna fursa ya kuongeza ajira, kupunguza umaskini, kuongeza mapato ya mauzo nje na kukuza uchumi.
 
            Ndugu Mgeni Rasmi, Utalii ni kichocheo muhimu kwa biashara, hutoa ajira, chanzo cha fedha za kigeni, pia hutoa mahitaji ya ziada nje ya uchumi wa ndani. Takwimu za utalii husaidia kuelewa wapi watalii hutoka na wapi wanapenda kwenda ndani ya nchi; kutambua kama kuna "utalii zaidi" ambao unahitaji kusimamiwa ili kuwa wa kudumu; na ni maeneo gani yanayohifadhiwa kwa ajili ya utalii. Mwaka 2016, jumla ya watalii 991,593 walitembelea hifadhi za Taifa ikilinganishwa na watalii 930,205 mwaka 2015, sawa na ongezeko la asilimia 6.6. Kati ya hao watalii 551,083 walitoka nje ya nchi na watalii 440,510 walitoka ndani ya nchi. 

Ndugu Mgeni Rasmi,  kwa unyenyekevu mkubwa naomba kuhitimisha maelezo yangu kwa kuwashukuru Wadau wa Maendeleo ambao wameendelea kutoa misaada ya raslimali fedha pamoja na masuala ya kitalaam katika uzalishaji wa takwimu rasmi nchini,  nikianza na Benki ya Dunia, DFID, Jumuiya ya Ulaya, CANADA, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na wadau wengine wote wa Maendeleo. 

Ahsanteni kwa kunisikiliza.



Picha ya pamoja na wanafunzi wa shule za Sekondari mkoa WA dAR ES salaam

Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA