VIWANDA VYA SAMAKI MWANZA NOMAA

WAZIRI wa Wizara ya Mifugo, Kilimo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba amefanya ziara ya kushitukiza jijini Mwanza na kubaini madudu  baadhi viwanda vya samaki vilivyopo na kubaini kimoja kimekuwa sugu kwa kuchakata samaki wachanga pia uwepo vituo bubu vya samaki, upotevu wa wa mapato ya mabondo ya samaki.

Dk Tizeba alifanya ziara hiyo hivi karibuni kwa kutembelea Viwanda vya kuchakata na kuuza minofu ya samaki nje ya nchi ili kuangalia hali halisi ya mazao ya samaki yanayofikishwa katika viwanda vya Omega Fish, Tanzania Fish Processor (TFP), Victoria Pech zamani ikijulikana Mwanza Fish, Nile Perch, Tanpech Fish Ltd na baadhi ya sehemu za Kirumba, Mkuyuni na Nyakato zinazotumika kupoza samaki kwenye majokofu.

Waziri alitoa agizo kwa Afisa Mfawidhi wa Uthibiti wa Ubora wa Samaki na Mazao yake Kanda ya Ziwa Victoria, Steven Lukanga kusimamia kufanya ukaguzi wa kila wakati na kuhakikisha samaki waliochini ya sentimita 50 na waliozaidi ya sentimita 85 kilo 207 hawaruhusiwi kuingizwa na kuchakatwa katika viwanda hivyo kama alivyokuta katika kiwanda cha Omega Fish Ltd kilichopo eneo la Ilemela Manispaa.

“Haiwezekani una wakaguzi wa kuangalia uthibiti na ubora wa samaki lakini unakuta kiwanda kinachakata samaki ambao hawaruhusiwi kwa mujibu wa taratibu na sheria za uvuvi endelevu kama kiwanda hiki cha Omega Fish hivyo ni lazima hatua za haraka zichukuliwe kwa maofisa wanaofanya ukaguzi katika viwanda hivi kwa kuwa wameshindwa kutimiza wajibu wao, ”Alisema Waziri.

Aidha aliongeza kuwa suala hilo la hatua za kuchukuliwa dhidi ya kiwanda hicho atamuagiza Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi wa Wizara hiyo kuchukua hatua za haraka ikiwemo kukifungia mara moja kwa mwezi mmoja kuchakata samaki na kuuza minofu ya samaki nje ya nchi hadi hapo serikali itakapojilidhisha kuwa hakitaendelea kufanya uchakataji wa samaki wachanga wasioruhusiwa kuingia viwandani.

Dk Tizeba aliagiza maafisa wa ukaguzi wa samaki na uvuvi Mkoa kufanya ukaguzi kila siku ili kudhibiti wafanyabiashara wanaoshirikiana na wamiliki wa vituo vya makontena ya kupoza samaki wasiweze kupoza samaki wachanga (madegele) ambao amewakuta kwenye makontena yao na kutaka wachukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kuyafungia kufanya kazi hiyo kutokana na kuhujumu rasilimali hiyo.

“Utaratibu upo wazi tumeagiza samaki waliochini ya sentimita 50 na waliozidi sentimita 85 ni marufuku kuingizwa viwandani pamoja na kwenye hivi viwanda bubu (vituo bubu)  vya kupoza samaki kabla ya kusafirishwa kwenye masoko, lakini pia wakiendelea hatua kali za kisheria zichukuliwe haraka na bila kufumbia macho ili kusaidia kulinda uvuvi endelevu ndani ya ziwa Victoria ,”alisisitiza.

Waziri pia alimuagiza Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza (RAS), Clodwig Mteve kuhakikisha anafuatilia taarifa za kuwepo kwa maafisa uvuvi wawili wa kitengo cha Ukaguzi wa samaki cha Nyegezi kudaiwa kupigania rushwa baada ya kukamata samaki wadogo (madegele) katika Meli ya Mv Bigil eneo la Kirumba na kudaiwa kufikishwa kituo cha Polisi Kirumba Wilaya ya Ilemela ili kuwachukulia hatua za kimaadili.

“RAS nikuombe ufikishe taarifa ya agizo langu kwa wakurugenzi wa Manispaa ya Ilemela na Jiji la Mwanza ili kuwaondoa maafisa uvuvi wa Halmashauri hizo katika majukumu yao ikiwemo uhamisho kufatia kuwa chanzo cha kushindwa kudhibiti uvuvi haramu pamoja na kuruhusu samaki wadogo kufikishwa katika masoko bila kuwakamata wafanyabiashara wanaofanya biashara za samaki wachanga (madegele),”alisisitiza Dk Tizeba.

Waziri pia aliwataka wamiliki wa viwanda kutoyauza mabondo ya samaki kwa njia za panya ikiwemo kwa wafanyabiashara wa mabondo wakiwemo wachina kwa kuwa wamekuwa wakikosesha serikali mapato na ushuru wake yanayotoka katika mazao ya samaki na kutaka kufuata utaratibu uliopo wakati wakisubilia taarifa ya Tume iliyoundwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo ili kutoa mrejesho mzuri wa biashara hiyo.

Naye Afisa Uvuvi Mkoa wa Mwanza, Lameck Mongo alisema kwamba ofisi yake itaendelelea kufunga maeneo ya mazalia ya samaki ndani ziwa Victoria hasa kwenye maji ya kina kifupi ili samaki waweze kuzaliana ambapo alifafanua kuwa kuanzia Januari hadi Juni kila mwaka hufungwa na kuanzia mwezi Julai hadi Desemba huruhusiwa kuvuliwa samaki wasiochini ya sentimita 50 na zaidi ya sentimita 85.

Mongo alikiri kuwepo baadhi ya wavuvi wasiowaaminifu wanaoendelea kufanya uvuvi haramu na kushirikiana na wafanyabiashara ambao ni walanguzi kuchukua samaki hizo kwa lengo la kupeleka katika viwanda vya kuchakata samaki na sehemu za makontena ya kupozea samaki, hivyo kikosi cha doria cha maafisa uvuvi Mkoa na Kanda ya Ziwa wataendelea na jukumu la kuwasaka na kuwakamata ikiwemo kuwafikisha kwenye sheria.

MWISHO.
 
 

Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.