SIKU 100 ZA AWAMU YA TANO BALOZI SEFUE ANENA
Picha mbalimbali
zikimuonesha Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue akitoa taarifa ya siku
100 za kwanza za Serikali ya awamu ya tano.
TAARIFA YA SIKU 100 ZA KWANZA ZA SERIKALI YA
AWAMU YA TANO ILIYOTOLEWA NA
BALOZI OMBENI Y. SEFUE, KATIBU MKUU KIONGOZI,
IKULU, TAREHE 12 FEBRUARI, 2016
__________________________
Utangulizi
Serikali
ya awamu ya Tano imetimiza siku 100 tangu iingie madarakani tarehe 5 Novemba,
2015. Japo siku 100 ni chache sana kufanya tathmini ya kina, zinatosha kuonesha
muelekeo wa serikali na kupata kionjo cha uthabiti wa dhamira yake ya
kutekeleza ahadi zake kwa wananchi.
Kumekuwa na shauku kubwa ya wananchi
kujua kilichofanywa na Serikali hii katika siku zake 100 za mwanzo. Ni shauku
ya haki ambayo sisi katika Serikali hii lazima tujaribu tuwezavyo kuikidhi.
Ndio maana kuanzia juzi Mawaziri mbalimbali wanazungumzia mafanikio katika hizo
siku 100, kila mmoja akienda kwa undani kwenye sekta yake. Nawaomba wananchi
wafuatilie kwa karibu yale ambayo Mawaziri hawa wanayatolea taarifa kwenu ikiwa
ni sehemu ya uwajibikaji wao kwa wananchi.
Mimi pia, kwa nafasi yangu ya Katibu
Mkuu Kiongozi, ambaye ni Katibu wa Baraza la Mawaziri na Mkuu wa Utumishi wa
Umma, nimepokea maswali mengi ya waandishi wa habari na wananchi wengine kuhusu
siku 100 za kwanza za uongozi wa Rais, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
Maeneo yanayohusu sekta mbalimbali yatazungumzwa na Mawaziri wanaohusika.
Lakini nimeona baadhi ya maswali yanaweza kujibiwa tu na ofisi hii, yaani
Ikulu.
Nimeyaweka maswali hayo katika
makundi matano na nitayazungumzia kwa ujumla:
·
Yapo maswali yanayohusu uongozi wa Rais wetu;
·
Yapo maswali yanayohusu sifa binafsi za Rais wetu;
·
Yapo maswali yanayohusu utendaji wake;
·
Yapo maswali yanayohusu mahusiano yake na sekta
binafsi kwenye utawala wake; na
·
Yapo maswali yanayohusu mwelekeo wake kwenye mambo
ya nje na diplomasia ya Tanzania.
Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano Ukoje?
Wahenga
walisema, “Nyota njema huonekana asubuhi.” Naam! Katika siku 100 za kwanza,
Rais Magufuli amethibitisha kwa uwazi zaidi kuwa yeye ni kiongozi bora na wa
kupigiwa mfano. Taarifa tunazoletewa na wananchi ni kuwa kwa kauli, matendo na
dhamira yake, wananchi wengi wamemwelewa, wamemkubali na wanamwamini. Katika
hizi siku 100, Rais amewathibitishia Watanzania kuwa yeye ni kiongozi, mwenye sifa muhimu za uongozi.
Sifa hizo ni pamoja na:
·
Kiongozi bora
lazima awe na dira, maono na malengo kuhusu anakotaka Taifa liende. Katika siku
100 za kwanza Rais Magufuli amedhihirisha kuwa ana sifa hiyo.
·
Lakini dira
bila mkakati ni ndoto. Kiongozi bora lazima awe na mikakati ya kutekeleza dira
na maono yake, pamoja na kufikia malengo katika vipindi tofauti. Katika siku
100 za kwanza Rais Magufuli amedhihirisha anayo sifa hiyo.
·
Kiongozi bora
lazima aheshimike na awe na mvuto wa kuwafanya wananchi wamwamini, na kumfuata.
Katika siku 100 za kwanza za utawala wake, Rais amewafanya hata ambao
hawakumpigia kura, wamwamini, wamwombee na kumfuata.
·
Kiongozi bora
anagawa majukumu, na haogopi kufanya hivyo, lakini anafuatilia. Katika siku 100
za kwanza Rais Magufuli amethibitisha kuwa anayo sifa hiyo.
·
Kiongozi bora
anajua na haogopi kuweka vipaumbele na mpangilio wake wa utekelezaji na
kuvisimamia. Katika hizi siku 100 Rais Magufuli amethibitisha anayo sifa hiyo
muhimu ya uongozi.
·
Kiongozi bora
haogopi kufanya maamuzi magumu. Hakuna mwenye shaka kuwa katika hizi siku 100,
Rais wetu amedhihirisha kwa kauli na kwa vitendo kuwa, anapotetea maslahi ya
Taifa na wananchi, haogopi kufanya na kusimamia maamuzi magumu.
Rais ana Maono na Mikakati pevu ya kutimiza maono
yake
Kama
nilivyosema, sifa mojawapo ya kiongozi bora, ni kuwa na maono pevu na mikakati
madhubuti inayotekelezeka, ya kutimiza maono hayo kwa faida ya wananchi.
Tumeona haya kwa Rais Magufuli na Serikali yake katika siku 100 za kwanza.
Tangu wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu, Rais Magufuli aliweka bayana maono ya
Tanzania anayotaka kuijenga, na nini kifanyike ili kutimiza azma hiyo. Maono na
shauku yake, kama ilivyo kwetu sote, ni kujenga Tanzania mpya yenye uhuru, haki,
neema na fursa mbalimbali kwa wananchi wote; Tanzania yenye amani na utulivu;
Tanzania yenye uchumi imara unaotegemea viwanda; Tanzania ambayo kila mtu
ananufaika na rasilimali tulizonazo; na Tanzania isiyo na rushwa, ufisadi na
dhuluma.
Rais anabadili
utendaji wa Serikali
Mtakumbuka,
kuwa Serikali ya Awamu ya Tano, iliahidi kuendeleza misingi imara ya kiuchumi,
kisiasa na kijamii iliyojengwa na awamu zilizotangulia. Pia iliahidi kuwa,
katika juhudi zake za kuinua uchumi na kuondoa kero zinazowakabili wananchi,
itazingatia vipaumbele vifuatavyo katika kubadili na kuboresha utendaji
Serikalini.
1.
Kupunguza
urasimu ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa maamuzi na miradi ya Serikali;
2.
Kuongeza kasi
ya ukusanyaji mapato na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji wenye maslahi kwa Taifa,
hususan katika sekta ya viwanda;
3.
Kubana matumizi,
kwa kupunguza yale ambayo kwa kuzingatia hali yetu ya uchumi kwa sasa, yanaweza
kuepukika;
4.
Kuimarisha
huduma za jamii, hasa katika maeneo yenye kero zaidi kwa wananchi;
5.
Kuhimiza na
kusimamia utii wa sheria, kurejesha nidhamu ya Serikali, na uzingatiwaji wa
maadili kwa viongozi wa umma na watumishi wote wa Serikali, sekta binafsi na
watu wote kwa ujumla;
6.
Kudumisha
ulinzi na usalama, na kuendeleza mahusiano mazuri na yenye tija baina ya
Tanzania na nchi za nje, mashirika na taasisi za kikanda na kimataifa, pamoja
na wabia wengine wa maendeleo.
Amiri Jeshi
Mkuu
Katika siku hizi 100 za kwanza, Rais
ametekeleza majukumu yake ya Amiri Jeshi Mkuu kwa wepesi na uhodari kama vile
samaki kwenye maji. Amekuwa karibu na Jeshi na viongozi wake. Amekagua vifaa
vya Jeshi na mazoezi ya kijeshi. Ameteua viongozi wa Jeshi, na kutoa kamisheni
kwa Maafisa Wapya. Ametoa maelekezo mahususi ya kuimarisha Jeshi na utendaji
wake.
Sifa Binafsi za Rais Magufuli
Kundi
la pili la maswali tuliyoletewa linahusu sifa binafsi za Rais Magufuli ambazo
zimedhihirika katika hizi siku 100 za uongozi wake. Nitataja chache.
·
Mkweli
Katika hizi siku 100, Rais wetu amewadhihirishia
Watanzania kuwa ni mkweli, anayechukia ulaghai na unafiki. Anaposema, “Msema
kweli ni mpenzi wa Mungu” anamaanisha hivyo kwa dhati. Wapo watu wanaofikiri
kuwa siasa ni ujanja na ulaghai. Rais wetu amethibitisha kuwa yeye si
mwanasiasa wa aina hiyo. Hakuna tofauti kati ya alivyokuwa akiwa mgombea na
alivyojidhihirisha katika siku 100 za kwanza za Urais. Watanzania wana kila
sababu ya kufurahi kuwa alivyojinadi ndivyo anavyotawala.
·
Anatekeleza ahadi
Katika siku 100 Rais wetu amethibitisha kuwa
anaheshimu ahadi zake na anazitekeleza kadri iwezekanavyo. Tayari ipo mifano
kadhaa. Aliahidi kupunguza ukubwa wa Serikali, na amefanya hivyo kwa kupunguza
idadi ya Mawaziri na Naibu Mawaziri kutoka 55 hadi 35. Amepunguza pia idadi ya
Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu kutoka 56 hadi 50. Aliahidi elimu ya
msingi (mpaka kidato cha nne) bila malipo na ametekeleza. Alipoiahidi Mahakama kuwa
atawapa fedha zao zote za maendeleo, Sh.12.3 bilioni, ndani ya siku tano,
ametekeleza hata kabla siku hizo hazijaisha. Na mifano mingine ipo ya anavyotekeleza
ahadi zake. Kwa ufupi, aliahidi kuwa hatawaangusha Watanzania na kweli
hajawaangusha katika hizi siku 100.
·
Anajali
kwa Dhati Shida na Kero za Wananchi.
Katika siku 100 za kwanza, Rais ameonesha namna anavyoumizwa
na kufadhaishwa na kero zinazowakabili wananchi. Pia amethibitisha dhamira yake
ya dhati ya kuzipatia ufumbuzi, hususan katika upatikanaji wa huduma za jamii
ikiwamo huduma za afya, elimu na maji.
Kasi ya kutatua kero za wananchi imeongezeka sana.
Ndani ya siku hizi 100, tuna mifano mingi ya hatua zilizochukuliwa na Serikali
kuondoa kero, zingine zikiwa za muda mrefu sana. Mmemsikia Waziri wa Ardhi
akizungumzia utatuzi wa mgogoro wa muda mrefu wa shamba la Kapunga katika
Wilaya ya Mbarali (Mbeya), ambapo hekta 1,870 tayari zimerejeshwa kwa wananchi.
Aidha, mmesikia urejeshwaji kwenye miliki ya serikali, kiwanda cha chai cha Mponde,
kilichopo mkoani Tanga, ambacho kilikuwa kero kwa wananchi kwa muda mrefu. Kila
Waziri ataeleza mifano mingine mingi, kwenye kila sekta, kuonesha kasi mpya ya kumaliza
kero na shida za wananchi.
Usimamizi wa Nidhamu bila Uwoga
Sifa
nyingine ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano iliyodhihirika katika kipindi
cha siku 100 za kwanza ni uwezo wa kusimamia nidhamu bila upendeleo ama uwoga. Orodha
ni kubwa ya viongozi na watumishi waliochukuliwa hatua mbalimbali za kisheria
na kinidhamu kwa kushindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo.
Siku
100 za kwanza za Serikali ya Awamu ya Tano zimepambanua wazi ni aina gani ya
uongozi na utumishi wa umma unatakiwa katika serikali hii. Imedhihirika wazi
kuwa Serikali ya Awamu ya Tano haitamvumilia kiongozi au mtumishi yeyote wa
umma atakayeshindwa kutekeleza wajibu wake ipasavyo, au kufanya maamuzi
yanayolenga kumnufaisha yeye binafsi. Na tayari mrejesho tunaoupata kutoka kwa
wananchi ni kuwa nidhamu kwenye utumishi wa Umma imeongezeka na wananchi
wanahudumiwa kwa haraka zaidi, na kwa heshima zaidi.
Tumedhamiria
kurejesha nidhamu ya kazi na kutokomeza utamaduni wa kufanya kazi kwa mazoea na
kujinufaisha. Katika tafsiri pana zaidi, hatua hizo zinalenga kukuza utamaduni
wa uadilifu, uwajibikaji na kufanya kazi kwa uhodari, bidii na ufanisi mkubwa,
kunakoendana na kauli mbiu ya “Hapa Kazi Tu”. Na ndio maana Rais aliwalisha
kiapo cha Uadilifu Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu wote aliowateua.
Kamwe Watumishi wa Umma wasisahau kuwa wao ni watumishi, sio mabwana, wa
wananchi. Wawatumikie kwa ufanisi, kwa uaminifu na kwa heshima.
Ukaribu na Wananchi na Uungwaji Mkono
Siku
100 za kwanza za Utawala wa Awamu ya Tano zimethibitisha ukweli wa usemi usemao
“imani, hujenga imani.” Ndani ya siku hizi 100, Serikali imefarijika kuona
namna wananchi wengi, bila kujali itikadi zao, walivyoonesha imani kubwa kwa
Mheshimiwa Rais na Serikali yake na jinsi wanavyoiunga mkono. Kwa upande
mwingine tumeshuhudia jinsi Mheshimiwa Rais na serikali yake ilivyo karibu na
wananchi na namna wananchi wanavyozidi kumfurahia Rais wao.
Na
wanafanya hivyo kwa vile wamemkubali kama kiongozi wao, na wanamwamini. Hivyo
moja ya mafanikio makubwa katika hizi siku 100 ni vile ambavyo Rais ameweza
kujijengea imani kubwa miongoni mwa wananchi wenzake, na kuwaunganisha katika kutafuta
ufumbuzi wa matatizo yao bila kuangalia vyama, dini, kabila na rangi zao.
Utekelezaji wa Vipaumbele
Moja
ya mambo makubwa tuliyojifunza kutoka kwa Rais wetu katika siku 100 za kwanza
za Serikali yake ni umuhimu wa kupambanua na kuelekeza rasilimali zetu katika
maeneo ya vipaumbele zaidi. Serikali ya Awamu ya Tano imewawezesha wananchi
wote kufahamu kuwa, nchi yetu haiwezi kupiga hatua kubwa kimaendeleo,
itakayotuwezesha kumaliza kero zinazotukabili na kufikia hadhi ya nchi ya
uchumi wa kati ifikapo 2025, bila ya kuwa na vipaumbele. Si kwamba dhana ya
vipaumbele ni mpya. La hasha. Tulikuwa tunaizungumzia siku zote. Lakini Rais
huyu ameitekeleza kwa namna iliyovuta hisia za Watanzania na watu wengine wengi
barani Afrika na duniani. Mifano ni kama ifuatavyo:
·
Badala ya
sherehe za Uhuru, tumefanya usafi ili kupambana na kipindupindu, na fedha
zilizookolewa zinajenga sehemu ya barabara iliyokuwa kero kubwa kwa wananchi.
·
Badala ya Rais
na Wabunge kujipongeza kwa sherehe kubwa, fedha zilizookolewa zimetatua tatizo
la vitanda kwa wagonjwa.
·
Badala ya
sherehe za siku ya UKIMWI, fedha zimekwenda kununua dawa za kufubaisha makali
ya UKIMWI.
·
Badala ya
semina elekezi ya Mawaziri, fedha zake zitakwenda kutekeleza mradi wa kufunga
vifaa vya kisasa vya kuchunguza magonjwa katika hospitali 37 kote nchini.
·
Badala ya
safari za nje fedha zilizookolewa zitatumika kwenye miradi ya maendeleo. Zaidi
ya Sh.7 bilioni ambazo zingeweza kutumika kwa safari za nje zimeokolewa katika
siku 100 na zitatumika kwenye miradi hiyo ya maendeleo.
Hatua
hizo, na nyingine nyingi, zimevuta hisia za watu mbalimbali kote duniani.
Mnaofuatilia mitandao ya kijamii mnajua hivyo, na wapo wameonesha wazi kutamani
tungewaazima Rais wetu kwa muda.
Mapato
Katika
siku 100 za kwanza Serikali imefanikiwa kuongeza makusanyo ya kodi na mapato yasiyo
ya kodi. Katika kipindi cha siku 100 za kwanza, mapato ya kodi yameongezeka
hadi kufikia Shilingi trilioni 3.34, ikilinganishwa na makusanyo ya Shilingi
trilioni 2.59 kwa kipindi kama hicho kwa mwaka wa fedha 2014/15, ikiwa ni
ongezeko la Shilingi bilioni 746.31. Hali kadhalika, kwa mapato yasiyo na kodi,
makusanyo yameongezeka hadi kufikia Shilingi bilioni 281.68, kutoka Shilingi
bilioni 224.03 katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2014/15, ikiwa ni ongezeko
la Shilingi bilioni 57.65. Nyote mmesikia, baada ya kashikashi pale Hospitali
ya Taifa Muhimbili, mapato yao yameongezeka maradufu na kuwapa uwezo mkubwa
zaidi wa kuhudumia wananchi. Hali ni hiyo pia kwenye Halmashauri.
Ukusanyaji
huu wa mapato, umeiwezesha Serikali kugharamia baadhi ya miradi yake kwa fedha
za ndani, mathalan, kuwalipa wakandarasi, kutenga fedha kwa ajili ya miradi ya
maji, miundombinu, umeme, kilimo, uwezeshaji wa vijana na kadhalika. Naamini
kasi iliyopo sasa itaongezeka kwa siku zijazo na kutupatia uhuru zaidi wa
utekelezaji wa mipango yetu. Kwa msingi huo nawasihi wananchi wadumishe
uzalendo kwa kulipa kodi kwa kila bidhaa wanazonunua, kwani mapato hayo ni kwa
ajili ya kuwahudumia. Pia msisite kutoa taarifa za wakwepa kodi, ambao
watashughulikiwa ipasavyo kwa mujibu wa sheria.
Ushirikiano na Sekta Binafsi
Serikali
ya Awamu ya Tano imedhamiria kuongeza kasi ya maendeleo na ukuaji wa uchumi
unaolenga kumnufaisha kila Mtanzania. Aidha, inaamini kuwa sekta binafsi ni
muhimili muhimu katika kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi, ukiwemo wa viwanda. Ndiyo
maana, hata kabla hajaunda Baraza la Mawaziri, Mheshimiwa Rais alikutana na
wafanyabiashara na wawekezaji wa sekta binafsi, katika juma la kwanza tu, baada
ya kuingia madarakani ambapo, pamoja na mambo mengine, aliwahakikishia utayari
na dhamira ya Serikali yake kuipa ushirikiano sekta hiyo.
Aidha,
alibainisha kuwa Serikali iko tayari kuendelea kuboresha mazingira wezeshi kwa
ajili ya kuongeza kasi ya uwekezaji endelevu na wenye tija kwa Serikali na
Wananchi, mathalan miundombinu ya nishati, reli na barabara, viwanja vya ndege,
bandari, maji, mawasiliano na upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya viwanda.
Pia aliwataka wazingatie wajibu wao wa kulipa kodi na kuheshimu sheria, kanuni
na taratibu za nchi katika shughuli zao za uwekezaji na biashara.
Vile
vile katika hizi siku 100, Rais amethibitisha nia yake ya kutoa fursa sawa kwa
sekta binafsi. Ameonesha kuwa wenye fedha wasiwe na kiburi cha fedha,
wakifikiri wana leseni ya kufanya watakavyo au kuonea wengine. Bali kila
mfanyabiashara ambaye ni mtiifu, anayetenda haki na kufuata sheria, atamwona Rais
Magufuli kuwa ni mbia wake katika kukuza uchumi wa Taifa letu.
Sera ya Mambo ya Nje
Tanzania
tunajivunia msingi imara wa diplomasia na mahusiano mazuri ya kimataifa,
uliowekwa na Viongozi wetu, kuanzia Awamu ya Kwanza iliyojikita katika ukombozi
wa Mwafrika na jamii nyingine zinazotawaliwa duniani, hadi Awamu ya Nne
iliyoendeleza diplomasia ya uchumi.
Hata
hivyo, Rais wa Awamu ya Tano, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, anatambua
pia kwa nadharia ya diplomasia na mahusiano ya kimataifa inabainisha kuwa sera
ya mambo ya nje inaakisi sera za ndani ya nchi. Foreign policy is an extension of domestic policy.
Tofauti
na wanaomlaumu Rais kwa kutosafiri nje ya nchi, Rais wetu anafahamu na
kushukuru sana kuwa Marais waliomtangulia wamefanya kazi kubwa na nzuri sana ya
kujenga mahusiano yetu na nchi za nje na kuimarisha diplomasia yetu. Lakini
Rais anatambua kuwa ili ailinde sifa hiyo, na kuikuza, lazima anyooshe mambo
kadhaa ndani ya nchi. Iwapo Tanzania itabaki kuwa maskini, yenye rushwa,
ujangili, madawa ya kulevya, na kadhalika hiyo sifa nzuri nje ya nchi
itaporomoka. Hivyo ameamua kujipa muda kuimarisha uchumi na maendeleo ndani ya
nchi, na kupambana na matatizo mengine yanayoharibu sifa yetu, ili iwe rahisi
kudumisha sifa ya Tanzania nje ya nchi.
Wengi
mtakubaliana nami kwamba hatua anazochukua Rais Magufuli kuimarisha mifumo na
utendaji wa humu ndani, umeipa sifa kubwa Tanzania huko nje pamoja na kwamba
yeye binafsi hajasafiri kwenda nje ya nchi tangu achaguliwe kuwa Rais. Hii
inadhihirisha wazi kuwa mambo yetu ya ndani yasiposhughulikiwa ipasavyo,
kusafiri tu kwa Rais nje siyo kigezo cha kudumisha heshima na urafiki mwema.
Napenda
niwahakikishie wananchi wote kuwa dunia inafuatilia yanayotokea nchini, na
wanashahuku ya kuona matokeo yake. Kila kona hivi sasa, nchi zinazungumzia
mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano ndani ya siku 100. Hili ni jambo la
kujivunia katika mahusiano yetu na nchi za nje na ni jambo kubwa kidiplomasia.Rais
amefanya kazi ya kutangaza Tanzania na kujenga sifa yake bila haja ya kusafiri.
Atakapokuwa tayari atasafiri tu.
Hitimisho
Siku
100 za kwanza za Serikali ya Awamu ya Tano, zimethibitisha kuwa Serikali yetu
ni makini na imedhamiria kutekeleza ahadi zake kwenu. Katika kutekeleza
majukumu yake ya kuwatumikia wananchi wote, Serikali imezingatia msingi
uliowekwa na serikali za awamu zilizotangulia. Na imedhamiria kutekeleza wajibu
wake kwa Taifa na wananchi. Ushindi ni lazima.
Nikitakiwa
kuelezea kwa maneno machache sana siku 100 za utawala wa Rais Magufuli
nitasema, ametuletea aina mpya ya uongozi, unaojenga juu ya msingi wa waliomtangulia,
lakini unaoweka Tanzania katika gia mpya (new
trajectory) kuelekea uchumi wa kipato cha kati ulioahidiwa na Dira ya
Maendeleo 2025.
Tumuunge
mkono. Hapa Kazi Tu!
Asanteni kwa kunisikiliza.
Comments
Post a Comment