MKAPA NA WAPUMBAVU NA MAFALA



Haya yalikuwa matusi ya Mkapa au ya CCM?
KWA mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu (TUKI) toleo la tatu la mwaka 2014, maana ya neno mpumbavu ni juha, fala, zuzu na mbumbumbu. Kwa ufupi mpumbavu ni mtu asiyetumia akili.
Na neno lofa lina maana kuwa  mtu anayezururazurura asiye na kitu wala kazi.
Rais wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, juzi Jumapili alipopata wasaa wa kuhutubia maelfu ya wanachama wa CCM waliokuwa wanazindua kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu katika viwanja vya Jangwani   Dar es Salaam, alirusha kijembe kwa wapinzani na kusema   wanaosema wanatafuta ukombozi ni wapumbavu na malofa.
Kwamba miongoni mwa wagombea urais wanane waliopitishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), hakuna mwingine mwenye sifa nzuri kama Dk. John Magufuli.
Kwamba haitoshi kuchukia umaskini, bali inatakiwa mtu aeleze ni namna gani ataweza kupambana na tatizo hilo.
Tunasema sawa; na ni vema Mkapa kama miongoni mwa makada waandamizi wa CCM kukipigia chapuo chama chake  kiweze kushinda Uchaguzi Mkuu kwa sababu kila chama cha siasa jukumu lake kuu ni kushika hatamu za dola.
Lakini katika kujenga hoja yake, Mkapa aliyewahi kuongoza nchi hii alitakiwa aonyeshe njia kwa kutumia lugha yenye staha na si matusi, kwani maana ya tusi ni neno chafu la kumuudhi mtu.
Turudi nyuma kidogo tupate somo maridhawa. Wakati wa uzinduzi wa kampeni za CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995 katika viwanja vya Jangwani (Dar es Salaam), Baba wa Taifa, Mwalimu  Nyerere, aliiasa CCM kufanya kampeni kwa kutumia hoja kuntu (authentic) na kwa lugha nzuri na ya heshima.
Aliasa kuwa “…hata kama Mzee Kifimbo akisema mambo ya ovyo…mnaweza mkamkosoa…mzee mtu nzima anasema mambo ya ovyo…lakini si matusi…”. Haya yalikuwa maneno ya busara ya Mwalimu Nyerere, mwasisi wa Taifa letu la Tanzania.
Lakini hizo zilikuwa enzi za Mwalimu, enzi za kuheshimiana zikichagizwa na umoja wa taifa. Enzi hizi inaonekana ni enzi za vijembe, matusi, udini na kila aina ya mmomonyoko wa maadili katika mchakato mzima wa kampeni za kuwania nafasi mbalimbali za uongozi nchini!
Lakini ni kitu gani kimetufikisha hapa? Inatosha  kusema  tu kuwa hivi sasa nchi inakwenda arijojo, yakiwamo matusi mbele kwa mbele katika medani ya siasa yakivihusisha vyama vyote vya siasa, hata ndani ya Bunge! Na haya hayajaanza leo.

Katika Jimbo la Arumeru Mashariki wakati wa kampeni za  kumnadi mgombea wa CCM, Sioi Sumari, CCM iliwatumia makada wake, wakiwamo aliyekuwa mweka hazina, Mwigulu Nchemba, Mbunge wa Bunda, Stephen Wassira, Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde, Waziri Mkuu wa zamani aliyelazimika kujiuzulu, Edward Lowassa (sasa mgombea urais kupitia Chadema) na hata Rais wa zamani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Benjamin Mkapa.
Miongoni mwa makada hawa kuna waliojipambanua katika kuakisi siasa za bei rahisi (cheap politics), za uongo na matusi, tena mengine ya nguoni! Lakini Lusinde ndiye aliyetia fora!

Kwa upande wake, Mkapa aliwaita wapinzani ‘vifaranga’ na kuteleza kidogo alipolivalia njuga suala la mbunge wa Musoma Mjini, Vincent Nyerere, kuwa si wa ukoo wa Mwalimu Nyerere badala ya kunadi sera za CCM!

Wakati Wasira akisema kuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa, aliiba fedha wakati wa ziara ya Papa John Paul wa II miaka ya 90, Lusinde alisema   Dk. Slaa alishindwa upadre akafukuzwa na kutoa matusi mengine, yakiwamo ya nguoni!

Uongozi wa Kanisa Katoliki uliamua kutoa tamko kukanusha taarifa ya Wasira.

Ni katika mazingira haya tunavisihi vyama vyote vya siasa vijenge hoja wakati huu na kuonyesha vitawafanyia nini Watanzania badala ya kurusha vijembe na matusi ambayo hayana tija kwao na kwa Taifa kwa ujumla.
Tunasema haya yataepusha shari huko tunakokwenda ili Uchaguzi Mkuu uiache nchi ikiwa moja na salama. Mtu mzima.......

Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA