BAADHI YA WABUNGE WA CCM WAWA WATETEZI WA WAKWAPUAJI FEDHA ZA IPTL BUNGENI



BAADHI ya wabunge wa Chama cha Mapinduzi (CCM), jana waliungana kuitetea Serikali katika kashfa ya uchotwaji wa zaidi ya Sh 300 bilioni zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, huku wakiiponda ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
Hata hivyo wabunge wa upinzani waliendelea kusisitiza viongozi waliohusika katika kashfa hiyo wawajibike.
 Wakichangia hoja hiyo jana jioni, wabunge hao wa CCM walisema baadhi ya mapendekezo kwenye ripoti ya PAC yametofautiana kwa kiasi kikubwa na yale ya CAG.
Baadhi yao walisema mjadala huo umelenga kuwachafua baadhi ya watu na kuwa hakuna waziri atakayewajibika bali watendaji.
Wabunge hao walihama kabisa kwenye suala la kashfa hiyo na kusema kilichopo ni jambo la kodi tu ambalo Serikali inaweza kuifuatilia.
Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde, alisema kamwe viongozi hao hawawezi kuwajibika kwani hakuna sehemu ambapo ripoti ya CAG imewataja kuhusika na uchotwaji wa fedha hizo.
Alisema huenda kamati hiyo ilikuwa na ajenda ya siri ndiyo maana ripoti yake imetoa mapendekezo kwamba baadhi ya mawaziri akiwamo Waziri Mkuu Mizengo Pinda wajiuzulu.
“Hapa hakuna mtu kujiuzulu wala nini, mheshimiwa waziri mkuu endelea na mambo yako kimyakimya, hakuna kujiuzulu hapa,” alisema Lusinde.
Mbali na hilo, pia mbunge huyo alimshambulia Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe akimhusisha na kupata mgawo wa fedha kutoka kwa mmiliki wa Kampuni ya PAP, Seth Sigh.
“Huyu Zitto ni mmoja wa watu ninaowaheshimu sana, na huwa spendi kumshambulia bila sababu, lakini ninataka aliambie Bunge hili hizi fedha alizotuma watu kuzichukua kwa Sigh zilikuwa za kazi gani.
“Maana isiwe anataja wenzake kuchota fedha wakati na yeye alinufaika nazo,” alisema Lusinde.
Mbunge wa Magomeni, Zanzibar, Muhamad Chomboh (CCM), alisema: “Unajua kuna watu wana ashki majununi, inakuWaje umma unaambiwa kitu sicho, fedha za IPTL si za umma, naomba hili litambulike na je katika hili Waziri Mkuu anaingiaje?"
Mbunge wa Viti Maalumu, Mariam Kisangi (CCM), alisema IPTL ilifuata utaratibu wote ikiwamo hukumu ya mahakama.      
   “Barua ziliandikwa mara nne na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, sasa hili linatoka wapi, wote tunajua katika hili la IPTL zile fedha ni zao je, inakuwaje ajiuzulu Waziri Mkuu au Muhongo?” alisema Kisangi.      
Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa (CCM), alieleza kushangazwa na suala la IPTL kumhusisha Naibu Waziri Nishati na Madini, Stephen Masele huku akiitaka PAC kuliangalia suala hilo.
 “IPTL tunaambiwa kampuni feki je, na umeme wao mbona tunautumia? Hili hapana,” alisema Ndassa.
Wakati wabunge hao wakieleza hayo, jana wakati wa maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu, kiongozi huyo wa Serikali alisema haoni sababu ya kujiuzulu.
Pinda alisema pamoja na kuwapo shauku kwa baadhi ya watu ya kutaka jambo hilo litokee, lakini suala hilo linategemea mipango ya Mungu ya kuwa ndiyo au hapana.
Kauli hiyo aliitoa kutokana na swali aliloulizwa na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
Katika swali lake, Mbowe alisema kwa kuwa Pinda ni kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni, je haoni sababu ya kujiuzulu ili kupisha watu wengine wenye uwezo ili wamalizie ngwe iliyobaki ya uongozi.
Akijibu swali hilo, Pinda alisema pamoja na hali hiyo alimtaka Mbowe kutambua kuwa angeweza kufanya hivyo, lakini haoni sababu.
“Mheshimiwa spika, inawezekana mheshimiwa Mbowe una shauku ya kutaka litokee hilo, lakini mambo haya yanategemea kama ndivyo Mungu kapanga au hapana.
 “Najua umeingiza mambo mengi sana kwenye jambo hili, lakini kubwa ni hilo ulilomaliza nalo. Ningeweza nikajaribu kujibu, lakini sina sababu ya kufanya hivyo.
“Sina sababu ya kufanya hivyo kwa sababu suala lenyewe ndiyo Subject (mada) ya mjadala hapa bungeni ambao unaanza leo (jana),” alisema Pinda.
Kafulila
Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), alisema aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basili Mramba aliisababishia hasara Serikali ya Sh bilioni 11 na kwa sasa yuko mahakamani, hivyo haiwezekani watu wengine waliofanya udadali na kuisababishia hasara Serikali ya zaidi ya Sh bilioni 21 waachwe.
Akichangia mjadala wa taarifa ya PAC kuhusu kashfa ya uchotwaji wa zaidi ya Sh bilioni 300 kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, Kafulia alisema haiwezekani maendeleo ya Watanzania yakwame kwa sababu ya watu wachache.
Alisema  mmiliki wa PAP iliyonunua mtambo wa kufua umeme wa IPTL, Seth Sigh anaweza kuiangusha CCM kama alivyokiangusha chama tawala cha KANU nchini Kenya katika kashfa ya Goldenberg.
Kafulila alisema Sigh alikuwa miongoni mwa waliohusika katika kashfa hiyo iliyokitikisa Serikali ya chama cha KANU.
Alisema kwa sasa jambo ambalo linaumiza vichwa vya wengi ni kwamba fedha hizo ni za umma au za IPTL.
 “Hasara tuliyopata ni zaidi ya fedha za Escrow, hasara ya kwanza ni MCC, hasara ya pili nchi wahisani kupitia bajeti wamegomea dola milioni 500. Katika MCC 1/3 ilikuwa miradi ya umeme, lakini tumepoteza.
“Kwenye hoja hii kinachoumiza vichwa vya wengi ni kwamba fedha ni za umma au za IPTL? Tukumbushane, waziri wa nishati wa madini alikuwa akisisitiza kuwa fedha zilitolewa kwa hukumu ya Jaji Utamwa, nilivyohoji nikaitwa tumbili.
“Hukumu hii hapa kwenye karatasi na hamna sehemu iliyosema fedha hizi ni za Escrow, leo Profesa Muhongo anasema ni kikao cha Kunduchi Beach Hotel cha Oktoba 8 mwaka jana na si hukumu.
“Hatusemi kuwa Muhongo hana  mazuri aliyoifanyia nchi hii, lakini kwenye wizi sheria iko pale pale.
“Hawa jamaa wamekula fedha za Escrow pamoja na VAT, madalali wa wizara ya nishati wamesababisha hasara ya Sh bilioni 21 ambazo zote zimeliwa,” alisema Kafulila.
Aidha mbunge huyo ambaye ndiye alishinikiza sakata hilo bungeni na hatimaye Serikali ikakubali uchunguzi kufanywa, alieleza kushangazwa kwa kitendo cha Profesa Muhongo kuendelea kung’ang’ania kuwa masuala hayo yako sahihi na fedha zilizochotwa ni za watu binafsi.
Mbowe
Akichangia mjadala  wa kikao cha jioni, Mbowe alisema ingawa wabunge wa CCM wameamua kulikumbatia suala hilo, Watanzania watajua na litakuja kuwahukumu.
Alisema kuna ushahidi wa wazi kuwa waziri mkuu aliwajibika juu ya suala hilo na kwa nafasi yake angepaswa kulishughulikia.
“Mtafunika jambo hili mwanaharamu apite, lakini hukumu ipo. Jambo hili limeivua Serikali nguo,” alisema.
Muhongo: Fedha za Escrow si za Serikali
Awali akitoa utetezi wa Serikali juu ya kashfa hiyo, Waziri  Muhongo aliendelea kusisitiza kwamba fedha zilizokuwa katika akaunti ya Tegeta Escrow si za umma bali ni za watu binafsi.
Profesa Muhongo alisema fedha hizo ni mali ya Kampuni ya Kufua Umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), ambapo kama wakala wa kodi anastahili kudaiwa na mwisho kulipa kodi yote ambayo hajalipa.
Akizungumza bungeni jana kujibu hoja za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Profesa Muhongo alisema Tanesco ilikuwa inapata huduma ya umeme bila kulipa moja kwa moja IPTL, lakini ikawa inapeleka fedha hizo katika Akaunti ya Escrow.
“Tanesco ilisimamisha kupeleka malipo kwenye Akaunti ya Escrow na wala kulipa IPTL kuanzia Oktoba 30, mwaka 2010 lakini pamoja na kutokulipa, Tanesco iliendelea kupata huduma ya umeme kwa kadiri ilivyohitaji kutoka IPTL.
“Kulingana na taarifa hiyo ukurasa wa 36 hadi 42 imeonyesha kiasi ambacho kilipaswa kuwekwa kwenye Akaunti ya Escrow kwa mujibu wa ankara za IPTL ni shilingi bilioni 306.68. Hata hivyo, kwa mujibu wa ukaguzi huo fedha zilizokuwa kwenye akaunti wakati wa kuifunga ni Sh bilioni 182.77 na kuwa na  upungufu wa Sh bilioni 123.90 ikiwa ni deni ambalo Tanesco bado wanadaiwa na IPTL.
 “Kwa msingi huo, taarifa ya PAC haisemi ukweli kuhusu fedha zilizowekwa katika Akaunti ya Escrow kuwa ni fedha za umma, na ili kuthibitisha kwamba fedha hizi siyo za umma, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika ukaguzi wake wa hesabu za Tanesco wa Desemba 31, mwaka 2012, alielekeza kutoa fedha za Escrow kwenye vitabu vya hesabu vya Tanesco na kupunguza deni kwa kiasi hicho hicho,” alisema.
Alisema taarifa ya PAC imeeleza kwa mujibu wa mkataba wa PPA, Tanesco na IPTL walipaswa kutumia mtaalamu wa upatanishi katika mgogoro wa gharama za uendeshaji.

Comments

Popular posts from this blog

Je, wajua kwamba Australia ni bara, nchi na kisiwa?

AMANI YETU TUILINDE NAIBU WAZIRI CHANDE AZUNGUMZA KATIKA IJITIMAI JIJINI DODOMA

UNAMKUMBUKA AMINA CHIFUPA WA MPAKANJIAA.